2013-05-17 09:41:21

Kanisa linapaswa kuwa ni kielelezo cha huduma ya upendo kwa watu wa Mungu!


Baba Mtakatifu Francisko, Alhamisi tarehe 16 Mei 2013 mara baada ya Maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kikanisa cha Domus Sanctae Marthae kilichoko mjini Vatican amekutana na kuzungumza na Kamati kuu ya Shirikisho la Mashirika ya Misaada ya Kanisa Katoliki Kimataifa, Caritas Internationalis inayoendelea na mkutano wake wa mwaka hapa mjini Vatican chini ya uongozi wa Kardinali Oscar Andres Rodriguez Maradiaga, Rais wa Caritas Internationalis.

Baba Mtakatifu amewaambia wajumbe hao kwamba, Mashirika ya Misaada ya Kanisa Katoliki ni kielelezo cha upendo wa Kanisa kwa wahitaji, jambo ambalo linabubujika kutoka katika undani na asili ya Kanisa lenyewe. Baba Mtakatifu alipata fursa pia ya kusikiliza ushuhuda kutoka sehemu mbali mbali za dunia kuhusu kazi na utume unaotekelezwa na Caritas Internationalis ambayo mwaka huu inatarajia kuzindua kampeni dhidi ya baa la njaa duniani.

Baba Mtakatifu anasema kwamba, Kanisa linaweza kuonesha ukuu wa Mungu si kwa kutenda miujiza, bali kwa kushirikishana na kumegeana upendo ambao Mwenyezi Mungu amekwisha umimina katika mioyo ya waja wake. Baba Mtakatifu anasema, Jumuiya ya Kimataifa kwa sasa inakumbana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa ambao kimsingi unagusa nyanja mbali mbali za maisha ya mwanadamu: kitamaduni na hata kiimani.

Mambo yote haya anasema Baba Mtakatifu yana madhara makubwa katika maisha ya mwanadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Caritas inapaswa kutambua kwamba, inatumwa kuwajengea watu matumaini kwa kuwasaidia kuboresha hali ya maisha ya wale wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Kuna kinzani nyingi zinazojionesha katika masuala ya fedha na uwekezaji kiasi cha kugumisha maisha ya mwanadamu na waathirika ni watoto, wanawake na wazee.

Inasikitisha kuona kwamba, licha ya utajiri mkubwa wa rasilimali ya dunia, lakini bado kuna watu wanateseka kutokana na: umaskini, magonjwa, baa la njaa, wakati huo huo wengine wanatumia maendeleo ya sayansi kwa ajili ya kukumbatia utamaduni wa kifo. Hizi ni dalili za kumong'onyoka kwa misingi ya maadili na utu wema.

Baba Mtakatifu amegusia pia umuhimu wa Caritas kuwa ni chombo cha faraja kwa wahanga wa vita na mamillioni ya wakimbizi na wahamiaji wanaolazimika kutoka katika maeneo yao kwa kutafuta hifadhi ya maisha. Mama Kanisa anachangamotishwa kuwahudumia kwa moyo wa upendo na mshikamano wa dhati: kwa kujitoa bila ya kujibakiza katika huduma ya afya, elimu na maendeleo endelevu, kwa kutambua kwamba, Kanisa halina budi kuchukua ile sura ya Msamaria mwema ambaye kimsingi ni Kristo mwenyewe ili kuwajengea watu uwezo wa kujiletea maendeleo yao wenyewe!

Baba Mtakatifu anasema, watakatifu mbali mbali ndani ya Kanisa walijitahidi kusoma alama za nyakati na kutafuta njia ya kuweza kuyapatia ufumbuzi matatizo yaliyokuwa yanawasibu ndugu zao katika Kristo. Huu ndio msingi wa tasaufi ya upendo inayomsukuma mwamini kujitosa bila ya kujibakiza kwa ajili ya huduma kwa Mungu na jirani. Huduma kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii ni jambo ambalo linapaswa kupewa kipaumbele cha pekee katika maisha na utume wa Kanisa.

Mwishoni, Baba Mtakatifu Francisko amegusia hali ya wakimbizi kutoka sehemu mbali mbali za dunia, lakini kwa namna ya pekee kutoka Syria ambako hadi sasa inakadiriwa kwamba, kuna zaidi ya wakimbizi millioni moja. Kuna wahamiaji wanaoteseka na kudhulumiwa kwa kufanyishwa kazi za suluba kwa ujira kidogo. Haya ni maeneo ambayo yapaswa kufanyiwa kazi na Mama Kanisa katika huduma ya upendo.







All the contents on this site are copyrighted ©.