Mke wa Waziri mkuu wa Tanzania Mama Tunu Pinda amewaasa Makatibu Muhtasi na kuwataka
wazingatie maadili ya taaluma yao ya uhazili ili kuongeza ufanisi wa majukumu ya kazi
zao.
Ametoa wito huo Mei 16, 2013 wakati akifungua Kongamano la Tatu la Makatibu
Muhtasi (Tanzania Personal Secretaries Association - TAPSEA) kwenye ukumbi wa Mikutano
wa Kimataifa Arusha (AICC), Jijini Arusha.
Kongamano hilo la siku mbili, limehudhuriwa
na Makatibu Muhtasi zaidi ya 1,500 kutoka mikoa yote nchini Tanzania na baadhi ya
wawezeshaji kutoka Kenya, Uganda na Rwanda.
“Umuhimu wa taaluma ya uhazili
katika taasisi tunazofanyia kazi unatokana na nafasi kubwa ya makatibu muhtasi kama
wasimamizi wa ofisi na wasaidizi wa watendaji wakuu. Nafasi yenu inawapa fursa ya
kuandaa na kutunza nyaraka mbalimbali za kiofisi zinazohusu menejimenti ya taasisi
hizo. Niwaombe makatibu muhtasi wote mzingatie maadili ya kazi ya uhazili katika kutekeleza
majukumu yenu,” alisisitiza.
Aliwataka waongeze jitihada za kukimarisha Chama
cheo ili hatimaye TAPSEA iweze kuenea Mikoa yote na kuwa Chombo kitakachosimamia miiko
na maadili ya fani ya Uhazili.
Alisema majukumu ya makatibu muhtasi siyo kupiga
chapa pekee na kuongeza kwamba, kama chama cha kitaaluma, TAPSEA lazima iendeleze
jitihada za kubadili mtazamo huo ili jamii iweze kutambua umuhimu wa nafasi ya makatibu
muhtasi katika taasisi mbalimbali za umma na za sekta binafsi.
“Hata hivyo,
napenda ieleweke kwamba kazi ya kuleta mabadiliko ya kimtazamo inaanzia kwa katibu
muhtasi mwenyewe. Nawashauri wanachama wote wa TAPSEA wawe mstari wa mbele katika
kubadilika kifikra na kujiendeleza kila wakati ili kujijengea uwezo wa kuzikabili
ipasavyo changamoto za taaluma ya uhazili katika mazingira ya sasa,” alisema.
Mama
Tunu Pinda alisema kuwekeza katika teknolojia ni jambo muhimu lakini teknolojia pekee
haiwezi kuleta mabadiliko chanya katika kuboresha huduma na kuongeza tija. “Jambo
hili ni lazima liende sambamba na uwekezaji katika rasilimali watu kwa watumishi kusoma
zaidi na kupatiwa fursa za mafunzo zaidi ndani na nje ya nchi,” alisisitiza.
Mama
Tunu Pinda pia alizindua TAPSEA SACCOS na kuwataka makatibu muhtasi hao wajiunge kwa
wingi ili kutunisha mfuko wa chama chao.
Mapema, akimkaribisha kuzungumza na
washiriki wa mkutano, Mlezi wa TAPSEA Dk. Mary Nagu ambaye pia ni Waziri wa Nchi,
Uwekezaji na Uwezeshaji aliwataka wawe waaminifu katika kuijenga TAPSEA SACCOS ili
hatimaye ifikie hatua ya kuwa benki yao maalum kama ilivyo kwa Chama cha Walimu nchini.
Naye
Naibu Waziri wa Katiba na Sheria, Bi. Angela Kairuki ambaye pia mshauri wa Kisheria
wa TAPSEA aliwataka washiriki wa kongamano hilo kuzingatia maadili kwa kutunza siri
za ofisi wanazozitumikia.
“Inasikitisha kuona kila mara kunakuwa na taarifa
ambazo zinavuja lakini ukifuatilia wapi taarifa hizo zimetokea utabaini kuwa chanzo
ni makatibu muhtasi... ninawaomba sana mjitahidi kutunza siri za taasisi zenu,” alisisitiza.