2013-05-16 08:34:40

Kumbu kumbu ya miaka 1,700 ya Uhuru wa Kidini!


Katika Maadhimisho ya Kumbu kumbu ya miaka 1,700 ya Azimio la Milano, Baba Mtakatifu Francisko ametuma ujumbe wa matashi mema kwa Kardinali Angelo Scola wa Jimbo kuu la Milano, Kaskazini mwa Italia. Maadhimnisho haya yanapambwa na uwepo wa Patriaki Bartholomeo wa kwanza wa Kanisa la Kiorthodox la Costantinopoli.

Baba Mtakatifu katika ujumbe ulioandikwa kwa niaba yake na Kardinali Tarcisio Bertone, Katibu mkuu wa Vatican anamtakia kheri na baraka, Yeye pamoja na wageni wote wanaoshiriki katika Maadhimisho haya. Azimio hili, ulikuwa ni mwanzo wa uhuru wa kidini kwa Wakristo, ukiwa pia ni mwanzo wa Injili ya Kristo kupenya katika maisha na hivyo kuwa ni chachu ya mwanzo wa utamaduni wa wananchi wa Bara la Ulaya.

Kwa namna ya pekee, Baba Mtakatifu Francisko anawaalika Wakristo kwa pamoja kutolea ushuhuda wao wakiongozwa na Roho Mtakatifu, ili Ujumbe wa Habari Njema ya Wokovu uweze kuenea Barani Ulaya na sehemu nyingine za dunia. Ni matumaini ya Baba Mtakatifu kwamba, uhuru wa kuabudu utaheshimiwa na Serikali husika ili kutoa nafasi kwa waamini kushuhudia imani yao hadharani pamoja na kuendelea kuchangia katika mchakato wa maisha ya mwanadamu kiroho na kimwili.

Baba Mtakatifu anahitimisha ujumbe wake kwa kuwahakikishia wajumbe wote kwamba, yuko pamoja nao kwa njia ya sala na sadaka yake.

Itakumbukwa kwamba, Maadhimisho haya yaliyofanyika Jumatano tarehe 15 Mei 2013 yanaongozwa na kauli mbiu "tena mtaifahamu kweli, nayo hiyo kweli itawaweka huru". Tukio hili limehudhuriwa pia na viongozi mbali mbali wa Kanisa na Serikali kutoka ndani na nje ya Jimbo kuu la Milano.







All the contents on this site are copyrighted ©.