2013-05-15 12:12:23

Roho Mtakatifu anawawezesha waamini kumwendea Yesu na analiongoza Kanisa katika Ukweli!


Katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani, Baba Mtakatifu Francisko ameendelea na Katekesi kwa kuchambua Kanuni ya Imani, ambayo kimsingi ni muhtasari wa Imani ya Kanisa. Roho Mtakatifu ni Nafsi ya Tatu ya Fumbo la Utatu Mtakatifu. Yesu anamwita Roho Mtakatifu kuwa ni Roho wa Ukweli.

Baba Mtakatifu amechambua kazi za Roho Mtakatifu kwa kusema kwamba, katika ulimwengu mamboleo watu wana mashaka kuhusu ukweli, lakini Kanisa lina amini kwamba, ukweli upo na unapatikana kwa njia ya imani kwa Yesu Kristo, Neno wa Mungu aliyefanyika mwili.

Roho Mtakatifu anawawezesha waamini kumwendea Yesu; anayeliongoza Kanisa katika utimilifu wa ukweli. Ni msaidizi aliyetumwa kutoka kwa Yesu Mfufuka, ili kuwakumbusha yale yote aliyofundisha Yesu wakati akiwa bado hapa duniani pamoja na kuwaimarisha waamini ili kuchuchumilia kweli za wokovu.

Baba Mtakatifu anaendelea kusema kwamba, Roho Mtakatifu ni chemchemi ya maisha mapya katika Kristo anayewawezesha waamini kuwa na "jicho la imani" linalowawezesha kujishikamanisha na Neno la Mungu, pamoja na uelewa wa kina wa maana yake ili kuweza kuumwilisha katika uhalisia wa maisha ya kila siku.

Baba Mtakatifu Francisko anawaalika waamini kujiuliza swali la msingi, ikiwa kama wako wazi kwa nguvu za Roho Mtakatifu kama alivyokuwa Bikira Maria. Hata leo hii Fumbo la Utatu Mtakatifu linaendelea kukaa katika mioyo ya waamini. Baba Mtakatifu anawaalika waamini kumwomba Roho Mtakatifu ili aweze kuwaongoza katika ukweli pamoja na kuwasaidia kukuza urafiki na Kristo kila siku ya maisha kwa njia ya: Sala, Tafakari ya Neno la Mungu na Maadhimisho ya Sakramenti za Kanisa.

Baba Mtakatifu anawatakia waamini wote heri na baraka katika Maadhimisho ya Siku kuu ya Pentekoste. Ni matumaini yake kwamba: mapaji ya hekima, furaha na amani yatawaongoza waamini pamoja na familia zao katika njia ya ufuasi makini wa Kristo. Anawataka waamini kuendelea kuungana na Bikira Maria kusali kwa ajili ya faraja na nguvu ili kuimarisha imani kwa Kristo na Kanisa lake. Anawataka wawe mashahidi wa Kristo katika hija ya maisha yao hapa duniani. Kila mwamini ajitahidi kumfahamu Kristo na Ukweli huku wakidumu katika Ukristo wao kwani Ukristo si jambo la mpito!

Kwa namna ya pekee, Baba Mtakatifu Francisko alitambua uwepo wa waamini na mahujaji kutoka Jimbo la Arezzo-Cortona-San Sepolcro, Chieti- Vasto, Pitigliano-Savona- Orbetello waliomiminika kwa wingi kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, wakisindikizwa na viongozi wao wa Kanisa. Amewataka kuwa ni alama makini ya upendo wa Mungu na vyombo vya amani katika medani mbali mbali za maisha.

Baba Mtakatifu anakumbusha kwamba, shule zinazomilikiwa na kuendeshwa na Kanisa Katoliki zina nafasi ya pekee katika jamii na kwamba, dhamana hii inapaswa kutekelezwa kwa kushirikiana na Familia sanjari na kutambua nafasi yake katika Jamii husika.

Anawataka vijana kujitahidi kuuiga mfano wa Bikira Maria ili waweze kuwa ni faraja kwa wale wanaomboleza na amani kwa wenye majonzi na wapweke. Wagonjwa wametakiwa kupokea hali yao ya ugonjwa kwa imani, huku wakijiachilia mikononi mwa Mwenyezi Mungu na wanandoa wapya wadumishe uaminifu wao kama kikolezo cha furaha ya kweli.







All the contents on this site are copyrighted ©.