Vijana tumieni vyema fursa zilizopo kujiletea maendeleo endelevu!
Waziri Mkuu Mizengo Pinda amehimiza vijana wa Tanzania kuwa na uthubutu wa kujaribu
kuzifanyia kazi fursa zilizopo katika sekta tofauti kama vile ujasiriamali, kilimo,
viwanda, sanaa na utamaduni ambazo zinapatikana kwenye maeneo wanayoishi.
Alisema
kwa mujibu wa Sensa ya Makazi na Watu ya mwaka 2012, Tanzania ina idadi kubwa ya watu
wenye uwezo wa kufanya wazi, wanaofikia asilimia 52 ya watu wote, na wengi wao ni
vijana na asilimia 48 wanaobakia ni wazee na watoto. “Hivyo basi, nchi yetu inaweza
kupiga hatua kubwa za kimaendeleo kama kundi hili lote la vijana litaamua kutumia
kikamilifu fursa zilizopo nchini za kujiletea maendeleo,” alisisitiza.
Alikuwa
akizungumza na mamia ya vijana wa mji wa Dodoma na Dar es Salaam baada ya kupokea
maandamano ya kutangaza kampeni ya kupenda na kutumia bidhaa na huduma za Tanzania
maarufu kama “Made In Tanzania” yaliyofanyika kwenye Viwanja vya Mwalimu Nyerere mjini
Dodoma, Jumapili, Mei 12, 2013.
Kampeni hiyo ya Made in Tanzania inayoendeshwa
na kampuni ya Clouds Media Group ilianza Machi, mwaka huu, kwa lengo la kutambua watu,
bidhaa, mashirika, muziki na utamaduni wa Kitanzania na imelenga kutangaza bidhaa
na huduma za Tanzania.
Alisema wako watu walianza ujasiriamali kwa kuuza karanga
lakini walipanda hadi kuwa na biashara kubwa kwa sababu walitambua fursa zilizokuwepo
na wakazifanyia kazi bayana. “Kikubwa ni kuwa na dhamira na malengo, lakini fursa
ziko kwenye kilimo, viwanda, ufugaji nyuki, ufugaji kuku wa asili ama mapishi ya chakula,”
aliongeza.
Alisema anafurahishwa na mwamko uliopo hivi sasa kwa baadhi ya vijana
waliohitimu vyuo vikuu ambao wameamua kujiunga kwenye vikundi na kuanzisha miradi
yao. “Wako vijana waliohitimu ambao wameomba misaada Serikalini na wakaanzisha miradi
huko waliko. Wengine wako Igunga, Iramba, Tarime, Rufiji na Mkuranga,” alifafanua.
Alisema
wako walioamua kujihusisha na kilimo cha alizeti, na wengine wameamua kufuga kuku
wa asili na kuamua kuwauza Dar es Salaam ambako walibaini kuna soko la uhakika kwa
bei ya sh. 10,000/- hadi 15,000/- kwa kuku mmoja.
Alisema licha ya kudumisha
mapenzi ya dhati na kujenga uzalendo kwa nchi na watu wake, kampeni hiyo pia inalenga
kuonyesha ufahari wa yote yanayowazunguka Watanzania, ufahari ambao upo ndani ya kila
mmoja.
“Made in Tanzania kwa ujumla wake ni kampeni ambayo mmeileta mahsusi
kusaidia vijana kwa kuwahimiza kuona fursa za kiuchumi na za maendeleo zilizopo ambazo
zikitumiwa vizuri zitawezesha vijana na Taifa kwa ujumla kujikwamua kiuchumi na kuleta
maendeleo”.
Alisema kwa vile kampuni ya Clouds Media Group imeamua kwemnda
mikoa yote hapa nchini, haina budi kuvishirikisha vyombo vingine vya habari ili kampeni
hiyo iweze kuwa pana zaidi na kupata mwitiko wa kitaifa.
Akizungumzia kuhusu
kazi za wasanii hapa nchini, Waziri Mkuu alisema Serikali italinda uhalali wa kazi
za wasanii wa Tanzania na ndiyo maana ikaamua kuanzisha mfumo wa matumizi ya sticker
za Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA).
Mapema, akisoma risala mbele ya Waziri
Mkuu, Mkurugenzi wa Vipindi na Uzalishaji wa Clouds Media Group, Bw. Rugemalira Mutahaba
alisema kampuni yake kama chomcho cha habari wameamua kuendesha kampeni hiyo ili kuwaelekeza
vijana wa Kitanzania fursa zipi zilizopo, wafanye nini ili kuzipata na zaidi ya yote
kuwahimiza vijana hao wa wajifunze kuwa na uthubutu wa kutenda mambo bila woga.
Alisema
kampuni yake ilialika vijana 150 kutoka Dar es Salaam ili wafike Dodoma kujumuika
na vijana wenzao wa Dodoma ambao walishiriki semina maalum kuhusu fursa zilizopo nchini
iliyofanyika Chuo Kikuu cha Dodoma na kushirikisha vijana zaidi ya 2,000.