2013-05-13 08:06:09

Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani: Papa kutinga Brazil ili kuungana na vijana! Yaani...!


Baba Mtakatifu Francisko kwa mara ya kwanza kuanzia tarehe 22 hadi tarehe 28 Julai 2013, atafanya hija ya kichungaji Rio de Janeiro, Brazil ili kushiriki katika Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani inayoongozwa na kauli mbiu “Basi enendeni, mkawafanye mataifa yote kuwa wanafunzi” Mt. 28:19. RealAudioMP3

Miezi minne tangu alipochaguliwa kuwa ni Khalifa wa Mtakatifu Petro, Baba Mtakatifu Francisko anarudi tena Amerika ya Kusini, kwa kutembelea Brazil ambayo ina idadi kubwa ya Wakatoliki duniani. Baba Mtakatifu anatarajiwa kuwasili mjini Rio de Janeiro jioni ya Jumatatu, tarehe 22 Julai 2013 na kupokelewa na Mwenyeji wake kwenye Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Antonio Carlos Jobim wa Rio de Janeiro, na atabaki nchini humo kwa muda wa siku saba. Jioni Baba Mtakatifu atamtembelea Rais wa Brazil Dilma Rousseff.

Jumanne, tarehe 23 Julai 2013 baada ya safari ndefu, atapata mapumziko mafupi kwenye makazi ya Sumarè, mjini Rio de Janeiro.

Jumatano, tarehe 24 Julai 2013 itakuwa ni siku maalum kabisa ambayo Baba Mtakatifu Francisko ataitumia kwa ajili ya kufanya hija ya maisha ya kiroho kwa Bikira Maria Mkingiwa Dhambi ya Asili wa Aparecida. Hapa ataadhimisha Ibada ya Misa Takatifu.

Baadaye mchana, Baba Mtakatifu Francisko na msafara wake watapata chakula cha mchana pamoja na Maaskofu na Waseminari kwenye Seminari ya Yesu mchungaji mwema ya Aparecida. Baba Mtakatifu jioni, atatembelea na kufungua Hospitali ya Mtakatifu Francisko inayotoa huduma kwa wagonjwa wa afya ya akili.

Alhamisi, tarehe 25 Julai 2013, Baba Mtakatifu ataanza siku kwa kuadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwenye makazi yake ya muda hapo Sumarè mjini Rio de Janeiro. Asubuhi atakaribishwa na kupewa ufunguo wa mji wa Rio de Janeiro pamoja na kubariki bendera za Olympic.

Atatembelea Jumuiya ya Varginha na baadaye jioni, hapo shughuli ya kuwakaribisha vijana kutoka sehemu mbali mbali za dunia, itaanza kucharuka, kiashilio cha Ufunguzi wa Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013. Shughuli hii itafanyika kwenye ufukwe maarufu wa Copacabana ulioko mjini Rio de Janeiro.

Ijumaa, tarehe 26 Julai 2013, Baba Mtakatifu ataianza siku hii kwa Ibada ya Misa Takatifu na baadaye atashiriki katika kuwaungamisha baadhi ya vijana watakaoshiriki katika Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani. Tukio hili linafanyika kwenye Uwanja wa Quinta da Boa. Atasalimiana na baadhi ya vijana wanaotumikia adhabu yao gerezani na mchana atasali na vijana Sala ya Malaika wa Bwana. Mchana atapata fursa ya kukutana na kuzungumza na Kamati ya Maandalizi ya Siku ya Vijana na Wafadhili.

Siku hii itapambwa kwa vijana kupata chakula cha mchana na Baba Mtakatifu Francisko. Jioni vijana watashiriki pamoja na Baba Mtakatifu kuadhimisha Njia ya Msalaba kwenye ufuko wa Copacabana.

Jumamosi, tarehe 27 Julai 2013 majira ya asubuhi, Baba Mtakatifu Francisko ataadhimisha Ibada ya Misa takatifu pamoja na Maaskofu watakaokuwa wanahudhuria Siku ya 28 ya Vijana Duniani pamoja na Mapadre, Watawa na Majandokasisi, kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Sebastian. Baadaye atakutana na kuzungumza na wa viongozi wa Serikali, Kisiasa na Kijamii nchini Brazil.

Maaskofu wa Brazil na msafara wa Baba Mtakatifu kwa pamoja watapata chakula cha mchana kwenye Kituo cha Elimu cha Sumarè mjini Rio de Janeiro. Jioni Baba Mtakatifu atashiriki katika mkesha wa Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani katika Uwanja wa Campus Fidei.

Jumapili tarehe 28 Julai 2013, kitakuwa ni kilele cha Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani kwa Ibada ya Misa Takatifu na baadaye atasali Sala ya Malaika wa Bwana. Baba Mtakatifu atapata chakula cha mchana na msafara wake na jioni atakutana na kuzungumza na Kamati ya Uratibu ya Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Amerika ya Kusini.

Baba Mtakatifu atakutana pia na vijana wa kujitolea kwenye Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani na baadaye ataelekea Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Galeào/ Antonio Carlos Jobim wa Rio de Janeiro, tayari kuagana na vijana pamoja na wenyeji wake. Hivi ndivyo Baba Mtakatifu Francisko atakavyokuwa anakunja jamvi la Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013.

Anatarajiwa kuwasili mjini Roma kwenye Uwanja wa Ciampino majira ya mchana. Kama kawa, Idhaa ya Kiswahili Radio Vatican itahakikisha kwamba, “inakula nawe sahani moja” ili kukujuza yale yatakayokuwa yanajiri katika Maadhimisho ya Siku ya 28 ya Vijana Duniani kwa Mwaka 2013.

Itakumbukwa kwama, Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili katika utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro alibahatika kutembelea Brazil mara nne; yaani kunako mwaka 1980, 1982, 1991, 1997. Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto XVI, kunako mwaka 2007 alitembelea mji wa San Paulo na Aparecida, makao makuu ya Mkutano wa tano wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Amerika ya Kusini ambao pia Kardinali Jorge Mario Bergoglio alishiriki pia.








All the contents on this site are copyrighted ©.