2013-05-13 08:56:10

Askofu mkuu Justin Welby, Kiongozi mkuu wa Kanisa Anglikani kumsimika Askofu mteule Dr. Jacob E. Chimeledya mjini Dodoma


Rais Jakaya Kikwete wa Tanzania anatarajiwa kuwa mgeni rasmi katika Sherehe za kumsimika Askofu Mteule Dk. Jacob Erasto Chimeledya (56), wa Kanisa Anglikani, Dayosisi ya Dodoma zitakazofanyika Jumapili Ijayo kwenye Kanisa Kuu Dodoma itakayowahusisha viongozi wa ndani na nje.

Hayo yamesemwa katika Ibada ya Jumapili, Mei 12, 2013 na Katibu Mkuu wa Kanisa hilo Dicksoni Chilongani na kuthibitishwa na Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Dr. Rehema Nchimbi ambaye pia ni Mwenyekiti wa Kamati ya Ulinzi na Usalama mkoani Dodoma.

Akizungumza katika Ibada hiyo, Chilongani alisema, ili kuhakikisha yaliyojitokeza Arusha hayatokei Dodoma, hatua zote za ulinzi na usalama zimechukuliwa, na hivyo Kanisa limekubaliana na vyombo vya Usalama waumini watakaoingia Kanisani hapo wakaguliwe (Screened) na vyombo maalum.

“Kutokana na kuwa na ugeni wa Askofu Mkuu Justin Welby (57) ambaye ametawazwa rasmi kuwa Askofu Mkuu wa Cantebury Machi 2013 atamsimika Askofu Dk. Chimeledya, tahadhari zote zimechuliwa, hivyo msibebe mabegi makubwa maana mtapekuliwa na vyombo maalum”.alisema.

Akizindua Kanda ya Kwaya ya Uvuke na Kununua Kanda Moja kwa Sh. Laki Moja, Dk. Nchimbi alisema, pamoja na usalama kutoka kwa Mwenyezi Mungu waamini wanatakiwa kuwa na tahadhari hivyo amewaruhusu waamini hao kumpigia simu iwapo wataona chochote kisicho cha kawaida popote walipo.

Hata hivyo aliwataka wenye nyumba za wageni kuhakiki wateja wao na kuwatambua kwa taratibu na sheria za kazi yao, na akawageukia wazee wa Kanisa hilo kuonesha jinsi walivyo na wajibu wa kuwa Walinzi wa Kanisa la Mungu katika maeneo yao ya mitaa na kanisani.

Aidha Katika Uzinduzi huo, Dk. Nchimbi alisema, Kanda hizo zinakwenda Sokoni ili kuponya, kuokoa, kujenga Ndoa, kufundisha, na kuirejesha Jamii kufurahia Maisha Bora yaliyoko mikononi mwa mwa Mungu, ambayo Jamii itayaoata tu ikiwa na Uadilifu na Uchaji mbele za Mungu.








All the contents on this site are copyrighted ©.