2013-05-11 07:33:23

“Mitandao ya Kijamii: milango ya ukweli na imani; nafasi mpya za Uinjilishaji”.


Maendeleo ya sayansi na teknolojia ya habari yameanzisha “Jukwaa” na uwanja ambao watu kutoka sehemu mbali mbali za dunia wanashirikishana mawazo, habari na maoni; hapa ni mahali ambapo watu wanajenga mahusiano mapya sanjari na uundaji wa Jumuiya mpya. RealAudioMP3
Hivyo ndivyo Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, anavyoandika kwenye ujumbe wa Siku ya 47 ya Mawasiliano Duniani kwa mwaka 2013 inayoadhimishwa tarehe 12 Mei 2013 kwa kuongozwa na kauli mbiu “Mitandao ya Kijamii: milango ya ukweli na imani; nafasi mpya za Uinjilishaji”.
Baba Mtakatifu anasema, ikiwa kama njia hizi zitatumika kwa busara na uwiano mzuri zinaweza kuhamasisha majadiliano ambayo yakiendeshwa kwa heshima, kwa kuzingatia utu wa mtu; uwajibaki na ukweli zinaweza kuchangia mchakato wa ujenzi wa amani kati ya watu na hivyo kudumisha utulivu katika Familia ya Binadamu. Ubadilishanaji wa habari unaweza kwa hakika kuwa kweli ni mawasiliano yanayolenga kujenga urafiki pamoja na kurahisisha muungano kati ya watu.
Ikiwa kama Mitandao ya kijamii inapewa changamoto hii kubwa katika Jamii ya binadamu, wadau wakuu wanapaswa kujibidisha kuhakikisha kwamba, wanakuwa wakweli kwa kutambua kwamba, nafasi hizi zinatumiwa si tu kwa ajili kushirikishana mawazo na habari bali pia wahusika wenyewe.
Maendeleo ya mitandao ya Kijamii yanahitaji majitoleo: hapa watu wanajenga mahusiano na urafiki; wanatafuta majibu ya maswali yao msingi; wakiburudishwa pamoja na kuhamasishwa kushirikisha kipaji chao cha akili na ujuzi. Mitandao hii inaendelea kuwa ni sehemu ya vinasaba vya Jamii, kwa kuwawezesha watu kukutana katika masuala ya msingi. Mitando ya Kijamii inarutubishwa kutokana na mang’amuzi yanayobubujika kutoka katika sakafu ya moyo wa mwanadamu.
Baba Mtakatifu anasema, utamaduni wa mitandao ya Kijamii na mabadiliko katika mtindo wa mawasiliano ni changamoto kubwa kwa wale wanaotaka kuzungumzia kuhusu ukweli na tunu msingi za maisha ya binadamu. Jambo hili linaonekana kuwa na ushawishi mkubwa kutokana na umaarufu wa mtu au mvuto alionao na wala si katika mantiki ya mjadala uliopo kwenye Jukwaa. Wakati mwingine sauti yenye amani na utulivu inaweza kumezwa na mafuriko ya habari kiasi kwamba, inashindwa kutoa mvuto unaokusudiwa.
Mitandao ya Kijamii inahitaji kwa namna ya pekee: majitoleo ya watu wanaotambua fika umuhimu wa tunu za majadiliano zinazosimikwa katika uwezo wa mtu kufikiri pamoja na mpangilio wa mantiki; kwa ajili ya watu wanaotaka kuunda hotuba na maelezo yanayopania kudumisha mchakato wa mawasiliano. Kongamano na Majadiliano yanaweza kustawi ikiwa kama watatambua tofauti zao katika tamaduni pamoja na kuthamini tamaduni za watu wengine ili kutoa fursa ya kuweza kutajirishwa nazo kwa kutambua kwamba zinafumbata: wema, ukweli na uzuri.
Baba Mtakatifu anabainisha kwamba, mitandao ya Kijamii inakabiliwa na changamoto ya kuifanya kuwa ni shirikishi kiasi kwamba, itaweza kunufaika na uwepo wa waamini wanaotaka kushirikisha ujumbe wa Yesu na tunu msingi za utu na heshima ya binadamu zinazotangazwa katika Mafundisho ya Yesu. Waamini wanatambua kwamba, Habari Njema ya Wokovu inapaswa kufahamika katika ulimwengu wa mtandao kwani hili pia ni jambo msingi katika mang’amuzi ya wengi.
Mazingira ya mtandao yanagusa uhalisia wa mang’amuzi ya kila siku katika maisha ya mwanadamu, na kwa namna ya pekee miongoni mwa vijana wa kizazi kipya. Mitandao ya Kijamii ni matokeo ya mwingiliano wa binadamu yanayoleta mwelekeo mpya katika masuala ya mawasiliano yanayojenga uhusiano: kwa kuzingatia uelewa huu wa mazingira linakuwa ni jambo msingi kuweza kuwepo mahali hapo.
Kuna haja ya kuwa na uwezo wa kutumia lugha mpya itakayosaidia kufikisha utajiri wa Injili katika akili na mioyo ya watu wote. Katika mazingira ya mtandao maandishi kwa kawaida yanasindikizwa na picha pamoja na sauti. Mawasiliano makini kama ilivyokuwa kwenye mifano iliyokuwa inatolewa na Yesu katika mafundisho yake yanapaswa kushirikisha kipaji cha ufahamu na mguso kwa wale wanaotaka kutoa mwaliko wa kukutana na Fumbo la Upendo wa Mungu.
Tunatambua kwamba, Ukristo umekuwa na utajiri mkubwa wa alama na vielelezo: kwa mfano Msalaba, Picha, Sanamu za Bikira Maria, Pango la Noeli, Madirisha ya Makanisa yaliyopambwa kwa vioo vyenye picha za rangi. Sehemu kubwa ya amana ya urithi wa mwanadamu imetengenezwa na wasanii pamoja na wanamuziki waliotamani kuelezea kweli za imani.
Baba Mtakatifu anasema, waamini katika mitandao ya Kijamii wanaonesha ukweli kwa kushirikisha undani wa chemchemi ya furaha na matumaini yao: imani kwa Mwenyezi Mungu mwingi wa huruma na mapendo, aliyejifunua kwa njia ya Yesu Kristo. Wanashirikisha ukweli huu kwa njia ya imani na ushuhuda wao kwa jinsi wanavyowasiliana, chaguzi, vipaumbele na hukumu zao mintarafu Injili, hata kama haijaelezwa kinaga ubaga.
Ushuhuda huu unajionesha kwa mtu kujitoa nafsi yake kwa ajili ya wengine wanaposhirikisha kwa utulivu na adabu maswali na mashaka yao wanapoendelea na mchakato wa kutafuta ukweli na maana ya maisha. Ukuaji wa majadiliano katika mitandao ya Kijamii kuhusiana na imani inaonesha umuhimu na ukuu wa dini katika mihadhara na maisha ya Kijamii.
Baba Mtakatifu anasema kwamba, kwa wale waliopokea zawadi ya imani kwa moyo mkunjufu, upendo mkuu, ukweli na maana ya maisha; mambo ambayo pia yanapatikana katika mitandao ya Kijamii wanatambua kwamba yanapatikana kwa Yesu Kristo. Ni kawaida kwa watu wenye imani kutaka kuishirikisha kwa heshima na taadhima kwa wote wanaokutana nao katika Jukwaa la Mtandao. Ikumbukwe kwamba, jitihada za Waamini kushirikisha Injili zitazaa matunda yanayokusudiwa watambue kwamba, hapo kuna nguvu ya Neno la Mungu inayogusa mioyo ya watu kabla hata ya jitihada zinazofanywa na binadamu.
Hata katika mitandao ya Kijamii kuna sauti kali na yenye mamlaka inapaswa kuoneshwa hasa pale ambapo sauti zisizoweza kuvumilika zinapotaka kutawala, kwa kuwa makini zaidi katika maamuzi kwani wakati mwingine Mwenyezi Mungu anazungumza katika sauti nyororo isiyokuwa na nguvu wala vitisho. Ikumbukwe kwamba, binadamu anatamani kupenda na kupendwa sanjari na kupata maana ya maisha, hamu ambayo kimsingi imewekwa na Mwenyezi Mungu mwenyewe katika moyo wa kila mtu ili uweze kuwashwa na mshumaa wa imani.
Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita katika ujumbe wake kwa siku ya 47 ya Mawasiliano Duniani kwa Mwaka 2013 anabainisha kwamba, mitandao ya Kijamii ni njia za Uinjilishaji na kikolezo cha maendeleo endelevu; ni kichocheo cha umoja na mshikamano miongoni mwa Jumuiya za Waamini. Mitandao inasaidia kushirikishana rasilimali katika maisha ya kiroho na kiliturujia; kwa kusali pamoja na wale wanaoshirikishana na kumegeana imani.
Mawasiliano ya kweli na shirikishi yanayohusiana na masuala pamoja na mashaka ya wale wanaoacha imani, yawasukume waamini kutambua na kuonja umuhimu wa kuboresha imani kwa njia ya sala na tafakari; kwa kutambua uwepo wa Mungu na kwa njia ya matendo ya huruma yanayoonesha imani katika matendo.
Kuna baadhi ya mitandao ya Kijamii inayotoa fursa kwa ajili ya sala, tafakari pamoja na kushirikishana Neno la Mungu. Kuna mitandao mingine inayoweza pia kutumika kwa ajili kufungua malango kwa masuala mengine ya kiimani. Watu wengi wanaendelea kugundua kwamba, licha ya kukutana hapo awali kwenye mtandao, lakini bado kuna umuhimu wa kukutana ana kwa ana; kuwa na mang’amuzi ya Jumuiya na hata wakati mwingine kufanya hija za maisha ya kiroho; mambo ambayo ni muhimu sana katika hija ya imani.
Katika jitihada za kuhakikisha kwamba, Injili inaingia katika mitandao ya Kijamii, Waamini wanaweza kuwaalika watu kukusanyika pamoja kwa ajili ya sala au kushiriki katika Liturujia Kanisa au katika Kikanisa. Umoja na mshikamano wa kiimani ni mambo msingi kama sehemu ya kutolea ushuhuda wa imani na Injili ya Kristo, iwe ni duniani au katika mitandao ya Kijamii, daima wako karibu na wengine na wanaalikwa kuwaonjesha upendo wa Mungu watu wanaoishi miisho ya dunia. Kwa maneno haya, Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita anahitimisha ujumbe wake kwa Siku ya 47 ya Mawasiliano Duniani kwa Mwaka 2013.

Imeandaliwa na Padre Richard Mjigwa, C.PP.S.
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.









All the contents on this site are copyrighted ©.