Rais Uhuru Kenyatta na Makamu wa Rais William Ruto wana kesi ya kujibu!
Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa limetupilia mbali ombi lililokuwa limetolewa
na Serikali ya Kenya kutaka Umoja wa Mataifa kufuta kesi inayomkabili Rais Uhuru Kenyatta
na wenzake kuhusiana na machafuko ya kisiasa yaliyojitokeza nchini humo mara baada
ya uchaguzi mkuu uliofanyika kunako mwaka 2007 na kusababisha watu zaidi ya 1,200
kupoteza maisha yao na wengine wengi kukosa makazi kwa kuhofia usalama wa maisha na
mali zao.
Wanadiplomasia waliojadili mwenendo wa ombi hili kutoka katika Baraza
la Usalama la Umoja wa Mataifa wanasema, Baraza hilo halina mamlaka ya kusitisha kesi
ambayo imekwishafunguliwa kwenye Mahakama ya Kimataifa ya uhalifu wa kivita. Rais
Uhuru Kenyatta na Makamu wa Rais William Ruto wanakana makosa haya na kwamba, kesi
hii inatarajiwa kuendelea tena kuanzia mwezi Julai, 2013.