Uinjilishaji si mhemko wa kutaka kumbadili dini mtu bali ni utangazaji habari njema
ya upendo wa Injili kwa watu wote. Ni msisitizo uliotolewa na Papa Francisko , mapema
Jumatano wakati akiongoza Ibada ya Misa katika Kanisa ndogo la Mtakatifu Marta la
Vatican. Papa aliongoza Ibada hiyo kwa kusaidiana na Kardinali Fransisko Coccompalmerio
na Mons. Oscar Rizzi, ibada iliyohudhuriwa pia na Wafanyakazi wa Sectretariat Kuu
ya Utawala wa Mahakama ya Jimbo la Papa.
Papa alieleza, Wakristo wa leo,
hawana tofauti na Wakristu wa wakati wa Mtakatifu Paulo, alipozungumzia juu ya watu
wa mataifa, na kuwahimiza Wakristu kujenga madaraja ya watu kukutana na kuisikiliza
Injili , bila shurutisho au kulaani imani zingine au mtu yeyote. Ni katika moyo
huo wa Mtume Paulo, alisisitiza Papa Fransisko, Wakristu wa leo , wanatakiwa kuitangaza
Injili na kuileta mioyo ya watu wengi wanao wasikiliza kwa Kristu. Na hili linatufanya
sisi Wakristu, kuwa wajenzi wa madaraja na si kujenga kuta za kubagua wengine. Huo
ndiyo mtazamo kwa Mkristu wa kweli.
Papa aliendelea kusema, Mkristo lazima
kumtangaza Yesu Kristo kwa njia ambamo Yesu Kristo anakubalika, kupokewa, na si
kukataliwa na watu. Mtume Paulo alijua kwamba, kutangaza ujumbe wa Injili, si jambo
jepesi ,lakini aliufanya utume huo kwa imani kwamba, haitegemea nguvu yake, lakini
Yeye Mwenye Kristu, atakaye ifanya kazi hiyo. Na kwamba , kumtangaza Kristu ni kuutangaza
Ukweli, Ukweli unaoongoza kwenye ukweli wote'.
Hivyo Mkristu anayetafuta
kuitangaza Injili lazima atembee katika njia hii, ili watu wote wasikie. Aipeleke
habari njema ya Injili kwa watu wote. Papa alieleza na kutolea mfano wa utoto wake
ambamo alisikia Wakatoliki wakisema hatuwezi kwenda katika nyumba yao, kwa sababu
wao si wakatoliki au kwamba hatuwezi kuwatembelea hao kwa sababau hawakufunga ndoa
Kanisani , au hatuwezi kushirikiana nao kwa sababu wao ni masosharisti, au mapebari
n.k, Papa amesema huko ilikuwa ni kuwatenga watu. Ni Mkristu kujijengea ukuta badala
ya kujenga daraja la makutano. Papa alieleza na kumshukuru Mungu kwamba , wakati huu
sera hizo zimepitwa na wakati. Bwana amejenga madaraja zaidi ya makutano ya watu
na imani mbalimbali, Bwana ndiye mjenzi wa madaraja na Paulo aliliona hilo na kumwiga
Yesu kwamba kuitangza habari njema ni kujenga madaraja ya makutano na si kulazimisha
watu kuiongekea Injili. Na utangazaji huu wa Injili ya wokovu, ukweli na upendo, zaidi
hufanyika kwa shuhuda za maisha na si maneno matupu. Papa alimalizia homilia
yake kwamba, na fundisho tunalilopata kwa Mtume Paulo kwamba, safari hii ya Uinjilishaji,
hufanywa na Yesu Mwenyewe, maana ni Yeye aliyeona ni vyema kutumia njia ya unyenyekevu
wa maisha na uhuru wa dhamiri, na si kwa mabavu ya kulazimisha, maana yeye ndiye
uhakika asiyekuwa na haja ya kujihakikishia au kutafuta sababu ya kujihalalisha kwa
mara ingine. Papa ameasa, iwapo Kanisa litapoteza ujasiri wake huu wa kitume,
basi linakuwa ni Kanisa la ushindani, Kanisa la ukiritiba wa sheria, kanisa la majivuno,
lakini ndani mwake halina uhai, kwa sababu sababu limepoteza asili yake ya ujasiri
wa kwenda nje , ambapo kuna watu wengi wanaoendelea na maisha ya ibada kwa sanamu,
kuipenda dunia na mawazo dhaifu, au mambo mengi mengi. Papa alitolea ombi lake
kwa Mtume Paulo , ili aweze kuwa msaada leo hii katika kujenga ujasiri wa kitume,
na juhudi za Kiroho , katika hamu hii ya kuieneza Injili kwa ujasiri. Na aliomba msamaha
kwa Baba, iwapo makosa yanayoweza kufanyika katika juhudi hizi za kuitangaza habari
njema ya Injili. Bwana mara aingilie kati, ili Kanisa lake liendelee kusonga mbele
na njia na Uinjlishaji. Na kwamba wale wanaoacha kutembea katika njia hii kwa kuogopa
kukosea, hufanya makosa makubwa zaidi.