2013-05-04 14:54:53

Ukweli kuhusu marekebisho ya kina ndani ya Kanisa!


Baba Mtakatifu Francsiko hivi karibuni aliteuwa kikundi cha Makardinali wanane kutoka sehemu mbali mbali za dunia, kitakachomsaidia kupata mawazo ya kufanya marekebisho ya uongozi wa Kanisa la Kiulimwengu pamoja na kuangalia uwezekano wa kufanya mabadiliko kwenye Waraka wa kichungaji, “Pastor Bonus” mchungaji mwema. RealAudioMP3

Hii ni sehemu ya utekelezaji wa mawazo yaliyotolewa na Makardinali wakati wa mikutano yao elekezi kabla ya uchaguzi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro. Uamuzi wa Baba Mtakatifu Francisko umezua hisia ambazo nyingine zimekwenda hata kinyume cha mawazo ya Baba Mtakatifu Mwenyewe, kila mtu akitaka kuweka walau chumvi kwa kile anacho amaini hasa kuhusiana masuala ya uongozi, mikakati na sera za uchumi wa Vatican na mageuzi katika ujumla wake.

Askofu mkuu Angelo Becciu, Katibu Mwambata wa Vatican katika mahojiano maalum na Gazeti la L’Osservatore Romano linalotolewa na kila siku mjini Vatican anabainisha kwamba, kuna baadhi ya waandishi wa habari wametia chumvi mno, kwani hadi sasa Baba Mtakatifu Francisko hajaonesha wazi utashi wake juu ya muundo wa Ofisi za wasaidizi wake wa karibu walioko mjini Vatican.

Kwa sasa Baba Mtakatifu anaendelea kusikiliza ushauri kutoka kwa watu mbali mbali, lakini atapenda kusikiliza zaidi ushauri makini utakaotolewa na Kundi la Makardinali wanane aliowachagua kwa ajili ya kazi hii nyeti ndani ya Kanisa. Kwa vile kuna haja ya kufanya mabadiliko katika Waraka wa Mchungaji mwema, kumbe, kunahitajika kwanza kabisa mwongozo makini utakaoelekeza mchakato mzima, ili yote yafanyike kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Kanisa la Kristo.

Askofu Becciu anasema, kuna baadhi ya watu wamekwenda mbali kiasi cha kusema kwamba, Baba Mtakatifu Francisko anatarajia kufunga Benki ya Vatican kwa vile haina umuhimu wowote, jambo ambalo si kweli kabisa. Kuna siku wakati wa Maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu iliyowashirikisha wafanyakazi kutoka Benki ya Vatican, alizungumzia kuhusu kiini cha maisha na utume wa Kanisa kwamba, kinajionesha kwa namna ya pekee katika uhusiano wa upendo kati ya Mungu na binadamu. Kumbe hata taasisi kubwa kama Benki ya Vatican haina budi kutoa mwelekeo huu ambao n ikiini na utambulisho wa Kanisa, vinginevyo haina maana ya kuwapo!

Mabadiliko yanayokusudiwa na Baba Mtakatifu Francisko yatakuja kwa wakati wake, lakini kwa sasa Wasaidizi wake wa karibu wanaendelea kutekeleza majukumu yao kama alivyowataka yeye mwenyewe. Wakuu wa “Curia” wanayo dhamana ya kuongoza Mabaraza ya Kipapa kwa kipindi cha miaka mitano, inapomalizika miaka hii, Baba Mtakatifu anakuwa na uamuzi wa kuuisha mkataba au kufanya uteuzi wa kiongozi mwingine. Baba Mtakatifu amesema kwamba, anahitaji muda wa kufanya tafakari ya kina pamoja na kusali ili kupata hali halisi ya uongozi wa Vatican kabla ya kufanya maamuzi yake.

Askofu mkuu Angelo Becciu anasema, Papa ndiye kiongozi mkuu wa Kanisa Katoliki na mwenye uamuzi wa mwisho. Makardinali walioteuliwa kumshauri hawa wanabaki kuwa ni washauri, hiki ni kielelezo makini kinachoonesha jinsi ambavyo Baba Mtakatifu Francisko anavyotaka kutekeleza wajibu wake wa kuongoza, kufundisha na kuwatakatifuza watu wa Mungu.

Makardinali hawa wamepewa dhamana ya kumashauri Baba Mtakatifu katika utekelezaji wa utume wake kwa Kanisa la kiulimwengu. Mabadiliko ya muundo wa Curia usiwe ni “kiwingu” cha kutaka kupotosha utashi na dhamiri nyofu ambayo imeoneshwa na Baba Mtakatifu Francisko katika kuleta mabadiliko ndani ya Kanisa, kama walivyoshauri pia Makardinali wakati wa mikutano yao elekezi kabla ya uchaguzi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Ushauri unapaswa kufahamika mintarafu taalimungu kama inavyofafanuliwa na Mama Kanisa. Askofu mkuu Angelo Becciu anasema, hata katika ngazi ya Parokia na Majimbo, Kanisa limeweka utaratibu wa kuwa na washauri , ambao baada ya kutoa ushauri wao, maamuzi yanafanywa na Mhusika mkuu, kama ni Jimbo, basi yanafanywa na Askofu, kama ni katika ngazi ya Parokia, basi Paroko husika anatekeleza utume wake kadiri ya Sheria na Kanuni za Kanisa.

Ushauri huu ni huduma ili kusoma alama za nyakati, ili kutambua Roho Mtakatifu anataka nini kutoka kwa Kanisa wakati huu wa Mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo. Uongozi ndani ya Kanisa ni huduma!








All the contents on this site are copyrighted ©.