2013-05-03 15:43:24

Papa Francisko akutana na kuzungumza na Rais wa Lebanon na ujumbe wake!


Rais Michel Sleiman wa Lebanon na ujumbe wake, Ijumaa tarehe 3 Mei 2013 amekutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu Francisko pamoja na viongozi waandamizi wa Vatican chini ya uongozi wa Kardinali Tarcisio Bertone, Katibu mkuu wa Vatican.

Viongozi hawa wawili pamoja na mambo mengine, wamekazia umuhimu wa ujenzi wa utamaduni wa majadiliano na ushirikiano kati ya Jumuiya ambazo zinatofautiana kikabila na kidini, ambao kimsingi ni utajiri unaojenga Jamii ambayo inapaswa kujikita kutafuta mafao ya wengi, maendeleo na utulivu wa taifa. Kuna haja kwa Seikali ya Lebanon kuunda Serikali mpya itakayopewa dhamana ya kukabiliana na changamoto zinazoendelea kujitokeza kitaifa na kimataifa.

Baba Mtakatifu Francisko pamoja na Rais Michel Sleiman wamejadili pia kuhusu kinzani na mgogoro wa kivita unaoendelea nchini Syria; hali ya wakimbizi wanaoendelea kufurika nchini Lebanon pamoja na nchi jirani; watu ambao kwa sasa wanahitaji msaada wa kiutu, huku wakiungwa mkono na Jumuiya ya Kimataifa. Wameunga mkono utashi wa kisiasa unaopania kuanzisha tena mchakato wa mazungumzo kati ya Israeli na Palestina kama njia ya kujenga na kudumisha amani na utulivu katika Ukanda wa Mashariki ya Kati.

Viongozi hawa wawili kwa pamoja wameangalia pia hali ya Wakristo ilivyo huko Mashariki ya Kati pamoja na mchango wa Kanisa mintarafu Waraka wa Kichungaji uliotolewa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, Kanisa Mashariki ya Kati, ambao kwa sasa ni Waraka rejea kwa Jumuiya za Kikatoliki na Jamii mbali mbali huko Mashariki ya Kati.







All the contents on this site are copyrighted ©.