Bila imani Kanisa litaonekana kuwa kama dala dala iliyokatika usukani!
Maadhimisho ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, miaka hamsini iliyopita, lilikuwa
ni tukio kubwa katika maisha na utume wa Kanisa; tukio ambalo liliibua udadisi mkubwa
kutoka kwa Wakristo na watu mbali mbali waliokuwa wanafuatilia maisha na utume wa
Kanisa kwa wakati huo. Kila mtu alikuwa na matumaini pamoja na wasi wasi ambao ungeweza
kuibuliwa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican. Yote haya yamepita
na watu wanazidi kusonga mbele, kiasi kwamba, hata kizazi cha wakati huu kina wasi
wasi, matarajio yake. Lakini, jambo la msingi ambalo linapaswa kukumbukwa daima ni
changamoto iliyotolewa na Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican iliyowataka waamini
na watu wote wenye mapenzi mema, kusoma alama za nyakati, ili kuweza kutenda kadiri
ya matarajio na wasi wasi za watu. Mtaguso mkuu ilikuwa ni fursa kwa Kanisa kuweza
kupembua alama za nyakati ili kuwajengea watu matumaini kwa njia ya ushuhuda kwa Yesu
Kristo Mkombozi wa Ulimwengu. Ni sehemu ya tafakari ya kina iliyotolewa na Kardinali
Zenon Grocholewski, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la Elimu Katoliki wakati alipokuwa
anashiriki kwenye Kongamano la Kimataifa kuhusu Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican lililokuwa
limeandaliwa na Taasisi ya Kipapa ya Dharmaram Vidya Kshetram, Bangalore, India, kama
sehemu ya kumbu kumbu ya Maadhimisho ya Jubilee ya miaka 50 ya Mtaguso Mkuu wa Pili
wa Vatican. Anasema, furaha, mateso, mahangaiko, matumaini na vipaumbele vya watu
ni sehemu ya maisha na utume wa Mama Kanisa ulimwenguni, kwa sababu Kanisa linafanya
hija ya maisha na binadamu hatua kwa hatua. Kanisa linaendelea kuwatia shime binadamu
kutoogopa wala kukata tama, kama Yesu alivyowaambia mitume wake, walipomwona akitembea
juu ya Bahari, wakashikwa na mshangao mkubwa. Waamini hawana sababu ya kuogopa magumu
na vitisho vya dunia hii, bali wanapaswa kusimama kidete kwa kujishikamanisha na Kristo,
ili waendelee kuwa kweli ni mashahidi wa matumaini kwa wote waliokata tamaa ya maisha!
Kanisa liwaoneshe watu mwanga wa tunu msingi za maisha adili. Ilikuwa ni hamu ya
Papa Yohane wa ishirini na tatu kuhakikisha kwamba, Kanisa linatoa mafundisho ambayo
kwa hakika yanagusa undani wa mwanadamu: kiroho na kimwili; kila mtu akijitahidi kutekeleza
wajibu na dhamana yake ndani ya Kanisa na Jamii kwa ujumla. Haki, amani, upendo na
mshikamano ziwe ni silaha za ujenzi wa Ufalme wa Mungu hapa duniani. Kwa njia
ya kweli za Kiinjili ambazo ni urithi mkubwa wa Mama Kanisa, basi liwasaidie walimwengu
kutambua na kuzimwilisha tunu hizi katika medani mbali mbali za maisha. Waamini wanahamasishwa
kwenda sehemu mbali mbali za dunia, ili kutangaza Habari Njema ya Wokovu. Sinodi zilizofuatia
mara baada ya Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican anasema Kardinali Grocholewski, zimeendelea
kufafanua Utajiri, Mapokeo na Mafundisho Tanzu ya Kanisa, ili yaweze kufahamika kwa
waamini na watu wenye mapenzi mema, kama sehemu ya mchakato wa kuyatakatifuza malimwengu. Baba
Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, wakati huo akiwa ni kati ya wataalam wa Mtaguso
Mkuu wa Pili wa Vatican anasema kwamba, wajumbe wa Mabaraza ya Maaskofu Katoliki kutoka
sehemu mbali mbali za dunia walifika wakiwa na mawazo yao na yale ambayo walipenda
Kanisa liyapatie kipaumbele cha kwanza. Lakini, kwa bahati njema, wote walijikuta
wakiwa darasani ili kujifunza kile ambacho Roho Mtakatifu alikuwa anawataka kutenda
kwa ajili ya Kanisa na Ulimwengu kwa ujumla, wakijikita zaidi na zaidi katika kuleta
mabadiliko ya dhati kwa kusoma alama za nyakati. Walitambua kwamba, Kanisa ni
moja; Takatifu, Katoliki na la Mitume. Lina Mapokeo na Urithi ambao unapaswa kuendelezwa
na wala hakuna sababu ya kujitenga na Mapokeo ambayo Kanisa limeyasimamia tangu kuanzishwa
kwake. Bila Imani, Kanisa lingeonekana kuwa kama “daladala iliyokatika usukani au
chumvi ambayo imekosa ladha. Hii ni changamoto ya kuendelea kutoa ushuhuda wa imani
tendaji ambayo Kanisa limepokea kutoka kwa Kristo na kuirithisha kwa watu wa vizazi
vyote. Mababa wa Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican, wakasiamam imara kutangaza: Mafundisho
ya Kanisa katika nyanja mbali mbali, wakionesha pia uhuru wa Kanisa, ili kuwasaidia
Walimwengu kutembea katika mwanga wa imani, matumaini na mapendo. Kwa maneno haya
Kardinali Zenon Grocholewski amehitimisha mchango wake katika Kongamano la Kumbu kumbu
ya Jubilee ya Miaka 50 ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican.