2013-05-02 14:41:37

Askofu msaidizi Titus Joseph Mdoe umeteuliwa na Mwenyezi Mungu kwa ajili ya kazi yake, nenda sasa wakati ni huu!


Kardinali Polycarp Pengo, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Dar es Salaam, tarehe Mosi, Mei 2013 amemweka wakfu Askofu msaidizi Titus Joseph Mdoe wa Jimbo kuu la Dar es Salaam katika Ibada ya misa iliyofanyika kwenye Viwanja wa Msimbazi.

Katika mahubiri yake Kardinali Polycarp Pengo, amesmhukuru kwa dhati Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita aliyemteua Padre Mdoe kuwa Askofu msaidizi wa Jimbo kuu la Dar es Salaam. Huu ni upendo ambao ameuonesha kwa namna ya pekee kwa Kanisa la Tanzania, kama alivyowahi kulipatia Jimbo kuu la Dar es Salaam maaskofu wasaidizi wawili kwa mara moja.

Baadaye akamteua mmoja wao na kumfanya kuwa Askofu wa Jimbo Jipya la Ifakara. Kabla ya kung’atuka kutoka madarakani amelipatia tena Jimbo kuu la Dar es Salaam, Askofu msaidizi ambaye ataendeleza kazi ya kufundisha, kuongoza na kuwatakatifuza watu wa Mungu.

Kardinali Pengo amesisitiza kwamba jambo la kwanza kabisa ambalo Askofu anapaswa kutambua ni kuwa uaskofu ni utumishi na wala si madaraka. Akiongelea kuhusu askofu mteule alimwambia kuwa Mungu amemteua kulichunga kundi lake si kwa sababu ya mastahili aliyo nayo bali ni kutokana na malengo ya Mungu mwenyewe.

Ameendelea kwa kusema kwamba, labda kuna watu ambao wanajisikia kufaa zaidi kushika wadhifa huo labda kwa sababu ni wakubwa zaidi na kimaumbile wanaonekana kama ndo wanaostahili zaidi; au pia kwa sababu wanayo elimu ya juu zaidi.. mambo yote haya, anasema kardinali, si maswali ambayo askofu Mdoe anapaswa kuyatafutia majibu.

Mwenyezi Mungu ana sababu zake zinazokwenda mbali na tofauti kabisa na mawazo hayo hasi ya kibinadamu. Kazi ya askofu Mdoe ni utumishi wake kwa watu wa Mungu Jimbo kuu la Dar es Salaam na mahali popote pale atakapotumwa na Mama Kanisa, ili kuwatangazia maskini habari njema ya wokovu

Naye Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda akitoa salaam za Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, amempongeza Askofu Mdoe kwa kuteuliwa na hatimaye kuwekwa wakfu kuwa Askofu msaidizi wa Jimbo kuu la Dar es Salaam. Amemtakia kheri na Baraka katika maisha na utume wake kama Askofu.

Kwa ujumla, Waziri mkuu amewasisitizia watanzania kuishi kwa upendo na uelewano kati yao; na kamwe chuki za kidini na kikabila zisikubalike katika jamii kwani haya ni mambo yanayohatarisha amani ya nchi ya watanzania kwa ujumla wao!. Watanzania wanapaswa kuheshimiana na kuthaminiana katika utofauti wa dini zao.

Vile vile amewashukuru viongozi wa dini kwa kuwa daima mstari wa mbele kutafuta yale yanayoleta umoja na mshikamano, na amewaomba viongozi hao, kuendelea kuwahimiza waamini wao umuhimu wa kuishi katika amani na kuheshimiana katika toufauti zao hasa zile za kidini, yote hayo yafanyike kwa nia njema ya kutafuta mafao ya wengi na maendeleo endelevu kwa watanzania wote.

Ibada hii ya Misa takatifu imehudhuriwa na Maaskofu wa Majimbo Katoliki Tanzania pamoja na viongozi wa kidini na kiserikali.

Imetayarishwa na Sr. Gisela Upendo Msuya.








All the contents on this site are copyrighted ©.