2013-05-01 11:56:16

Mtu asiyefanya kazi amepoteza utu na heshima yake!


Jamii ambayo haiwezi kutoa fursa ya ajira kwa watu wake na badala yake, inawanyonya kwa kuwaptia ujira kidogo haiwatendei haki watu wake. Ni sehemu ya mahubiri yaliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko wakati wa Maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu kwenye Kikanisa cha Domus Sanctae Marthae kilichoko mjini Vatican, Mei Mosi, 2013, kumbu kumbu ya Mtakatifu Yosefu Mfanyakazi. Ibada hii imehudhuriwa na wasichana wazazi wanaopewa hifadhi kwenye Jumuiya ijulikanayo kama "Il Ponte".

Maandiko Matakatifu yanaonesha kwamba, Mtakatifu Yosefu alikuwa ni Seremala kiasi kwamba, hata Yesu akaitwa ni Mwana wa Seremala. Mwenyezi Mungu alifanya kazi ya uumbaji kwa siku sita na siku ya saba akapumzika, kielelezo kwamba, kazi inampatia mwanadamu utu na heshima yake. Inasikitisha kuona kwamba, watu wanathamini zaidi vitu kuliko hata utu na heshima ya binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Waajiri wengi wanatafuta faida kubwa hata kwa gharama ya maisha ya wafanyakazi wao.

Wanasiasa kwa upande wao wanatafuta madaraka kuliko hata ustawi na maendeleo ya wananchi wanaowaongoza. Baba Mtakatifu anasema kwamba, kwa mwelekeo kama huu Jamii nyingi zimejikuta zikigonga mwamba kwa kutothamini utu wa mwanadamu na dhamana ya kazi katika maisha ya watu. Kwa mtu ambaye hana fursa ya kufanya kazi kwa hakika amepoteza utu na heshima yake.

Huu ni mwaliko kwa Jamii kuhakikisha kwamba, inaboresha hali ya maisha ya wafanyakazi pamoja na kupambana kufa na kupona na madhulumu yanayoendelea kufanyika katika maeneo ya kazi.







All the contents on this site are copyrighted ©.