2013-04-30 11:18:54

Weekeni mikakati na sera makini kuzuia magonjwa na ajali kazini


Taarifa ya Shirika la Kazi Duniani, ILO inaonesha kwamba, kila mwaka kuna watu zaidi ya millioni mbili duniani wanaofariki dunia kutokana na magonjwa wanayoyapata wakiwa kazini. Idadi hii ni kubwa zaidi kuliko hata ile ya watu wanaofariki dunia kutokana na ajali barabarani. Itakumbukwa kwamba, Jumuiya ya Kimataifa, hapo tarehe 28 Aprili 2013 imeadhimisha Siku ya Afya na Usalama Kazini.

Kumekuwepo na ajali nyingi kazini ambazo zinapelekea vifo vya wafanyakazi. Shirika la Kazi Duniani linakadiria kwamba, kila mwaka walau kuna wafanyakazi zaidi ya millioni 160 wanaoambukizwa magonjwa wakiwa kazini. Hii inatokana na ukweli kwamba, watu wengi wanafanya kazi katika mazingira duni hata pengine kinyume cha utu na heshima ya binadamu. Magonjwa kazini hayajapata kipaumbele cha kutosha kiasi kwamba, watu wanaendelea kupoteza maisha kila siku, jambo ambalo kamwe haliwezi kuvumiliwa.

Kuna haja ya Serikali na sekta binafsi kujipanga kwa kuibua mbinu mkakati zitakazosaidia kuzuia magonjwa na ajali kazini. Kuna mamillioni ya wafanyakazi ambao maisha yao yako hatarini, kumbe hili si jambo la kupuuziwa bali linapaswa kuwekewa mikakati madhubuti sanjari na kuzuia ajali kazini. Hali hii pia inachangia kwa namna ya pekee katika kuzorota kwa uchumi pamoja kuendelea kupukutisha nguvu kazi ambayo ingetumika kwa ajili ya uzalishaji na utoaji wa huduma.







All the contents on this site are copyrighted ©.