2013-04-30 07:52:40

Utu na heshima ya mwanadamu ni kipimo tosha kabisa cha heshima ya kazi!


Tarehe Mosi, Mei, wafanyakazi sehemu mbali mbali za dunia wanaadhimisha Siku yao sanjari na Siku kuu ya Mtakatifu Yosefu mfanyakazi aliyejitaabisha kuhakikisha kwamba, Familia Takatifu inapata mahitaji yake msingi. Kutokana na umakini wake katika masuala ya kazi, Kanisa limemweka Mtakatifu Yosefu kuwa ni msimamizi wa Wafanyakazi kwani linatambua kwamba, utu wa mwanadamu ndicho kipimo cha heshima ya kazi. Hii ndiyo thamani kubwa ya kazi kiimadili. RealAudioMP3

Kazi ni wajibu na utambulisho wa mwanadamu na kwamba, nguvu kazi inapaswa kupewa kipaumbele cha pekee. Kuna uhusiano wa pekee kati ya nguvu kazi na mtaji. Jambo hili linaweza kueleweka zaidi ikiwa kama wafanyakazi wanashiriki katika umiliki, usimamizi na faida. Kwa muhtasari haya ni kati ya mambo yanayotiliwa mkazo katika mfaundisho Jamii ya Kanisa kuhusiana na dhana ya kazi.

Baraza la Maaskofu Katoliki Canada katika Maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani hapo tarehe Mosi, Mei, 2013, linawaalika wafanyakazi na watu wenye mapenzi mema kuhakikisha kwamba, katika maandamano, semina, makongamano na mikutano watakayofanya kama sehemu ya Maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani wajitahidi kuweka ladha ya imani katika matukio yote haya, ili kuamsha hisia ya utajiri na rasilimali ya nchi kugawanywa katika mizani sawa pamoja na kuishirikisha Jamii katika mikakati na sera za maendeleo ya nchi.

Maaskofu wanawataka wafanyakazi kusimama kidete kupinga mabadiliko yatakayokuwa na athari kubwa katika maisha ya wafanyakazi na familia zao nchini Canada. Kuna haja kufanya mabadiliko ya dhati katika mifumo ya uchumi na mashirika na taasisi za fedha ambayo kwa sasa kutokana na ukiritimba na sera tenge yamepelekea wafanyakazi wengi kukosa fursa za ajira na hivyo kujikuta wanatumbukia katika dimbwi la umaskini wa kipato, kihali na maisha ya kiroho.

Baraza la Maaskofu Katoliki Canada linaonesha uhusiano wa dhati kati ya imani na mshikamano wa upendo na udugu unaopaswa kuoneshwa miongoni mwa wafanyakazi, kwa kuonesha mantiki mpya inayojikita katika mshikamano wa upendo unaovuka ubinafsi na hivyo kuwafanya waweze kusaidiana kwa hali na mali. Ni mshikamano unaopania kukuza na kumwendeleza mtu mzima: kiroho na kimwili; kwa kutafuta mafao ya wengi, huku wakijitahidi kulinda na kutunza mazingira ambayo kimsingi ni sehemu ya kazi ya uumbaji.

Baraza la Maaskofu Katoliki Canada linahitimisha ujumbe wake katika Maadhimisho ya Siku ya Wafanyakazi Duniani, kwa kuwataka wafanyakazi kuonesha mshikamano ili kujenga na kuimarisha utawala wa sheria unaosimikwa katika maadili na utu wema, kuanzia katika ngazi ya kitaifa hadi kimataifa. Lengo ni kuendeleza demokrasia ya kweli na haki. Maaskofu wanawatakia wafanyakazi wote: furaha, amani na utulivu wanaposherehekea Siku ya Wafanyakazi Duniani kwa Mwaka 2013.








All the contents on this site are copyrighted ©.