2013-04-30 07:29:02

Majadiliano ya kidini ni sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji mpya!


Vijana wa Kiislam na Kikristo wanakabiliana na changamoto kubwa katika ujenzi wa misingi ya haki, amani na utulivu katika jamii zao hasa wakati huu ambapo Jumuiya ya Kimataifa inashuhudia kwa kiasi kikubwa athari za myumbo wa uchumi kimataifa. RealAudioMP3
Jamii nyingi zinakabiliwa pia na athari za mmong’onyoko wa kimaadili na kiutu, mambo ambayo yanatikisa msingi ya maisha na utume wa Familia. Vijana wanatafuta utambulisho wao wa kidini katika ulimwengu mamboleo.

Hizi ni changamoto zinazofanyiwa kazi na Wawakilishi kutoka Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Barani Ulaya, kuanzia tarehe Mosi, Mei hadi tarehe 3 Mei, 2013 Jijini London. Ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia unaendelea kutoa changamoto mpya kwa Kanisa, kiasi kwamba, majadiliano ya kidini na waamini wa dini ya Kiislam ni jambo ambalo linapaswa kupewa msukumo wa pekee, ili kujenga na kuimarisha: misingi ya haki, amani, upendo mshikamano na utulivu.

Majadiliano ya kidini ni sehemu ya mchakato wa Uinjilishaji mpya unaofanywa na Mama Kanisa katika mapambazuko ya Millenia ya Tatu ya Ukristo. Waamini wanatumwa kumtangaza Kristo mkombozi wa ulimwengu; wakiheshimu na kuthamini uhuru wa kidini, kila mtu akiwa huru kutolea ushuhuda wa imani yake bila kificho.

Mkutano wa wawakilishi wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Barani Ulaya unaongozwa na kauli mbiu “Majadiliano na Utangazaji wa Habari Njema ya Wokovu”, unaratibiwa na Kardinali Jean Pierre Ricard, Askofu mkuu wa Jimbo kuu la Bordeaux.

Viongozi wengine wanaoshiriki ni pamoja Askofu mkuu Vincent Nichols, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Uingereza. Kardinali Jean Louis Tauran, Rais wa Baraza la Kipapa la Majadiliano ya Kidini ndiye anayefungua mkutano huu. Majadiliano na Uinjilishaji ni mada ambazo ziliwahi kujadiliwa kwa kina na mapana kunako mwaka 1991.

Katika mkutano huu, wajumbe watapata fursa ya kubadilishana mawazo, mang’amuzi pamoja na changamoto mbali mbali wanazokabiliana nazo katika maisha na utume wa Kanisa huko waliko. Umuhimu wa ujenzi wa utambulisho wa vijana kidini ni mada inayopembuliwa kwa mapana na marefu pamoja na kuangalia hali ya maisha ya Waamini wa dini ya Kiislam kutoka katika nchi mbali mbali za Ulaya mintarafu uhusiano na Wakristo.








All the contents on this site are copyrighted ©.