2013-04-29 10:44:16

Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro wageuka na kuwa kama ile Siku ya Pentekoste!


Askofu mkuu Rino Fisichella Rais wa Baraza la Kipapa la Uhamasishaji wa Uinjilishaji Mpya akiwatambulisha Wakristo 44 waliopewa Sakramenti ya Kipaimara na Baba Mtakatifu Francisko kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, alisema, wamesindikizwa na Wazazi, Mapadre pamoja na Makatekista waliowaandaa kwa ajili ya kupokea Sakramenti za Kanisa kama sehemu ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani.

Huu ni mwaliko kwa kila mwamini kukuza na kuimarisha ile Imani aliyopokea wakati wa Sakramenti ya Ubatizo. Kundi hili la Wakristo 44 linawawakilisha vijana kutoka sehemu mbali mbali za dunia watakapokea Sakramenti ya Kipaimara wakati wa Maadhimisho ya Mwaka wa Imani. Wao kama ilivyo kwa waamini wengine, watapokea Mapaji ya Roho Mtakatifu, tayari kwenda sehemu mbali mbali za dunia, kumshuhudia Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu kama ilivyokuwa Siku ile ya Pentekoste.

Askofu mkuu Rino Fisichella anasema kwamba, waamini wanaalikwa kwa namna ya pekee kutubu na kuongoka ili kuweza kupokea Neno la Mungu na neema zake zinazoleta mageuzi na maisha mapya kwa kuwakirimia Mapaji Saba ya Roho Mtakatifu.

Waamini walioimarishwa kwa Sakramenti ya Kipaimara wanachangamotishwa na Mama Kanisa kuendelea kufanya hija ya furaha na matumaini kama alama hai ya upendo na huruma ya Mungu kwa waja wake.







All the contents on this site are copyrighted ©.