2013-04-26 10:41:07

Makanisa yanayo dhamana ya ujenzi wa nchi yao!


Dr. Olav Fykse Tveit, Katibu mkuu wa Baraza la Makanisa Ulimwenguni, amehitimisha ziara ya kichungaji nchini Sudan ya Kusini iliyompatia fursa ya kukutana na kuzungumza na viongozi wa Makanisa pamoja na viongozi wa Serikali.

Anasema, Makanisa nchini Sudan Kongwe na Sudan ya Kusini yana fursa ya pekee kabisa katika kuchangia mchakato wa maendeleo endelevu katika nchi hizi mbili hasa baada ya miaka kadhaa ya vita vya wenyewe kwa wenyewe sanjari na kuhakikisha kwamba, uhuru wa kidini unaheshimiwa na kuzingatiwa.

Kuanzia tarehe 23 hadi 25 Aprili 2013, Dr. Tveit alikuwa Sudan Kongwe na Sudan ya Kusini; nchi mbili zilizojitenga kunako 2011 kama sehemu ya utekelezaji wa makubaliano ya amani yaliyokuwa yamefikiwa kunako mwaka 2005 baada ya wananchi wa Sudan ya Kusini kupiga kura ya maoni. Anasema, Makanisa katika nchi hizi mbili yana dhamana ya kushiriki katika mchakato wa maendeleo kwa kuendelea kushirikiana na Serikali hasa katika kulinda na kudumisha amani, uhuru wa kuabudu na mshikamano.

Serikali kwa upande wake, inasema, itaendelea kufanya mazungumzo na viongozi wa Makanisa katika msingi wa kuaminiana ili kwa pamoja waweze kushiriki katika ujenzi wa Sudan na kwamba, Serikali itaendelea kuhakikisha kwamba, wanapata uhuru wa kuabudu kadiri ya Katiba ya nchi zao.

Dr. Tveit anasema kwamba, Makanisa yanadhamana ya kutangaza Injili, jambo ambalo linahitaji umoja na mshikamano wa Makanisa kutoka Sudan Kongwe na Sudan ya Kusini. Kwa njia hii, wataweza kutolea ushuhuda wa tunu msingi za maisha ya Kikristo na hivyo kukabiliana na changamoto zinazojitokeza mbele yao wakati huu wanapojielekeza zaidi katika ujenzi wa nchi baada ya vita vya wenyewe kwa wenyewe nchini Sudan.







All the contents on this site are copyrighted ©.