2013-04-25 10:29:51

Ekaristi Takatifu ni kiini cha maisha na utume wa Kanisa


Baraza la Maaskofu Katoliki Costa Rica hivi karibuni limeadhimisha Kongamano la Nne la Ekaristi Takatifu Kitaifa, lililoongozwa na kauli mbiu ""Ekaristi Takatifu. Mkate wa maisha ya watu wetu". Baba Mtakatifu Francisko katika ujumbe ulioandikwa kwa niaba yake na Kardinali Tarcisio Bertone, Katibu mkuu wa Vatican, aliwatakia kheri na baraka washiriki wote wa kongamano kwa kutambua kwamba, Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu ni kiini cha maisha na utume wa Jumuiya ya Wakristo.

Baba Mtakatifu kwa namna ya pekee aliwaalika wajumbe kufanya tafakari ya kina na kusali zaidi, kwani Ekaristi Takatifu ni kiini cha maisha ya Kanisa; mahali ambapo waamini wanatolea sadaka ya shukrani na sifa, tayari kujitosa kimasomaso kwa ajili ya kushiriki katika mchakato wa Unjilishaji mpya, dhamana inayovaliwa njuga na Mama Kanisa katika Mapambazuko ya Millenia ya Tatu ya Ukristo.

Maadhimisho ya Ekaristi Takatifu yajenge na kuimarisha umoja miongoni mwa waamini; wajitahidi kujichotea neema na baraka kutoka mbinguni ili kushiriki katika ujenzi wa dunia inayosimikwa katika misingi ya haki, amani, upendo, mshikamano na upatanisho mintarafu ujumbe kutoka kwa Kristo mwenyewe.

Baba Mtakatifu Francisko amewaweka waamini wote nchini Costa Rica chini ya ulinzi na usimamizi wa Bikira Maria na Malaika, wanapoendelea na hija ya maisha yao kuelekea mbinguni kwa Baba. Baba Mtakatifu amewapatia wote baraka zake za kitume. Ujumbe wa Baba Mtakatifu katika Maadhimisho haya ulisomwa kwa niaba yake na Askofu mkuu Piero Marini, Rais wa Tume ya Kipapa ya Makongamano ya Ekaristi Takatifu Kimataifa.







All the contents on this site are copyrighted ©.