2013-04-24 15:43:26

Vitumieni Vipaji vyenu kwa manufaa ya wote - Papa ahimiza Vijana


Baba Mtakatifu Francisko, mapema Jumatano , baada ya kuzungukia maelfu ya mahujaji a wageni waliokusanyika katika uwanja wa Kanisa Kuu la Mtakatifu Petro la Vatican, akiwa katika gari dogo la wazi, alitoa Katekesi kama kawaida ya kila Jumatano.
Mafundisho ya Papa yameendelea kuzungumzia imani, leo yakilenga ujio wa pili wa Kristu "Yeye atakuja tena kwa utukufu, kuwahukumu walio hai na wafu".
Papa amesema, kama ilivyo historia ya binadamu, iliyoanza na kuumbwa kwa mwanaume na mwanamke kwa mfano wa Mungu,historia hiyo inatatimizwa na ujio wa Pili wa Kristu na hukumu yake ya mwisho.
Papa amekumbusha , kwa mara nyingi binadamu husahau misingi miwili ya historia hii na zaidi imani juu ya ujio wa pili wa Kristu na hukumu ya mwisho, ambavyo mara nyingi, vimeonekana kutoeleweka wazi kwa waamini. Yesu katika maisha yake hapa duniani, alilfundisha kwa kutoa mifano mingi, juu ya ujio wake wa mwisho.
Papa aliendelea kurejea maandiko mengi ya Injili, yanayosaidia kumzamisha mtu katika uelewa wa fumbo hili. Alitaja, mfano wa wanawali kumi , watano wenye busara na watano wapumbavu, na pia mfano wa hukumu ya mwisho , kama ilivyoelezwa katika Injili ya Mtakatifu Matayo( 24:29-31) (25: 113).
Anasema mifano hiyo inatukumbusha sisi kwamba ni lazima kiroho kuwa tayari kukutana na Bwana atakapokuja. Na mfano wa talanta, husisitiza wajibu wetu wa kutumia vipaji tulivyojaliwa kama zawadi kutoka kwa Mungu, kwa ajili ya kufanikisha faida kwa wengine wengi. Amehoji ni kwa jinsi gani, tumevitumia vipaji hivyo tulijaliwa bure na Mungu. Na kama ni haki kwa Mkristu , kufungua ndani ya moyo wake, neema na manufaa na mazuri yote ya kuishi na Kristu, bila ya kuwatangazia wengine.
Kwa ajili hiyo, Papa aliwageukia vijana waliokuwa miongoni mwa mahujaji na wageni , akisema, “ ninyi vijana wengi mliokusanyika hapa, mkiwa mmeianza tu hija ya maisha, je mmewahi kufikiria kwa jinsi gani, mnaweza kuvitumia vipaji mlivyojaliwa na Mungu, kwa ajili ya faida ya wengine, ndani ya kanisa na dunia yetu kwa ujumla.
Amewasisitizia wasifiche vipaji vyao, bali wajitokeze kwa ushupavu mkuu na waipanue mioyo yao, katika kuwahudumia wengine. Amesema, "Maisha mliyopewa si kwa ajili ya kuyafungia kwa uchoyo na ubinafsi lakini mmeyapewa kwa ajili ya kuhudumia wengine, na hasa wahitaji kama wazee na wagonjwa.
Baada ya Katekesi, Papa alisalimia na kutoa Baraka kwa makundi mabalimbali, wazee, wanadoa wapya na wagonjwa.








All the contents on this site are copyrighted ©.