2013-04-24 08:23:53

Maadili, haki msingi za binadamu na uwiano wa maendeleo endelevu!


Mafundisho Jamii ya Kanisa Katoliki ni nyenzo muhimu sana katika Uinjilishaji kwani inapania kwa namna ya pekee kuyatakatifuza malimwengu kwa kuweka mahusiano ya kibinadamu na ya jamii katika mwanga wa Injili. Kanuni za Mafundisho Jamii ya Kanisa zinatokana na sheria asili zinazoimarishwa na kukomazwa katika imani ya Kanisa kwa njia ya Injili ya Kristo inayoshuhudiwa katika matendo.

Kanisa ni mahiri sana katika kuyashughulikia masuala yanayohusu binadamu na linaendelea kuchanja mbuga kuelekea kwenye "mbingu mpya na nchi mpya". Kwa mujibu wa imani na kwa kujihusisha katika maisha halisi ya binadamu, jambo ambalo Kanisa linataka liwe wazi kwa kila mtu ili kusaidia mchakato wa watu kuishi kwa kuzingatia upeo wa maana halisi wa maisha. Binadamu anayeishi mintarafu hadhi ya utu wake anatoa utukufu kwa Mungu aliyewakirimia watu wote hadhi ya utu wa binadamu kwani wameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.

Ni kutokana na uelewa huu mpana Baraza la Maaskofu Katoliki Burkina Faso kwa kipindi cha miaka mitano sasa limekuwa likiandaa Juma la Tafakari ya Maisha Jamii linalosimamiwa na kuratibiwa na Tume ya Haki na Amani ya Baraza la Maaskofu Katoliki Burkina Faso. "Maadili, haki msingi za binadamu na maendeleo endelevu ya wananchi wa Burkina Faso: uwiano na matarajio katika mwanga wa Mafundisho Jamii ya Kanisa" ndiyo kauli mbiu iliyoongoza maadhimisho haya kwa mwaka 2013.
Lengo la Maadhimisho ya Juma la Tafakari ya Maisha Jamii wanasema Maaskofu ni kuliwezesha Kanisa kutekeleza wajibu na dhamana yake katika maendeleo ya wananchi wa Burkina Faso mintarafu haki msingi za binadamu, utu na heshima ya binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu. Serikali ya Burkina Faso imelishukuru na kulipongeza Kanisa kwa ushiriki wake katika kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima ya binadamu pamoja na kuwajengea uwezo wananchi ili kupambana kikamilifu na hali yao ya maisha.

Tume ya haki na amani ya Baraza la Maaskofu Katoliki Burkina Faso inasema, hizi ni fursa zinazopania kutoa majiundo endelevu kwa waamini ili waweze kukua na kukomaa katika imani, matumaini na mapendo. Lengo ni kuwajengea uwezo waamini na watu wenye mapenzi mema ili waweze kuwa ni chumvi na mwanga wa dunia unaopania kwa namna ya pekee kushiriki kikamilifu katika mchakato wa waamini walei kuyatakatifuza malimwengu.

Tafakari hizi zimewawezesha pia waamini kutambua na kushiriki katika mikakati ya Kanisa dhidi ya rushwa na ufisadi; umaskini na umuhimu wa waamini wa Kanisa Katoliki kushiriki kikamilifu katika maisha ya kijamii, kisiasa na kiuchumi, ili kuchangia kwa hali na mali, lakini zaidi kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao amini, yanayoonesha imani katika matendo.

Itakumbukwa kwamba, kanuni msingi za Mafundisho Jamii ya Kanisa zinakazia kwa namna ya pekee: mshikamano unaoongozwa na kanuni ya auni; mafao ya wengi; upendeleo wa pekee kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii; matumizi sahihi ya rasilimali kwa ajili ya wengi; haki na amani.







All the contents on this site are copyrighted ©.