2013-04-23 09:06:56

Kampeni ya chanjo kuokoa maisha ya watoto wadogo!


Shirika la Kuhudumia Watoto la Umoja wa Mataifa, UNICEF, tarehe 24 Aprili 2013 linaanza Kampeni ya chanjo kwa kipindi cha juma zima ili kupunguza vifo vya watoto wadogo vinavyoendelea kutokea sehemu mbali mbali za za dunia, lakini kwa namna ya pekee Barani Afrika na nchi nyingine zinazoendelea duniani. Lengo ni kuokoa maisha ya watoto kati ya millioni mbili hadi tatu kila mwaka. Hii ni changamoto kubwa kwa Jumuiya ya Kimataifa.

Katika kipindi cha mwaka 2011, jumla ya watoto millioni 22.4 walipatiwa chanjo, ikiwa ni ongezeko la watoto millioni moja, ikilinganishwa na watoto waliochanjwa katika kipindi cha mwaka 2010. UNICEF inasema, mikakati yake inakwamishwa na baadhi ya nchi wanachama ambazo zimeshindwa kuchangia ili kufanikisha kampeni hii.

Kati ya nchi 193 wanachama wa UNICEF ni nchi 152 ambazo zimechangia hadi sasa. Watoto wanaotoka kwenye familia maskini ndio wanaopoteza maisha kwa kukosa huduma za chanjo, ikilinganishwa na familia zenye uwezo mkubwa kiuchumi au zile zinazoishi vijijini.

Serikali husika zinapaswa kuwa na sera na mikakati madhubuti ili kwamba, chanjo iweze kutolewa kwa wote bila ubaguzi. Kampeni hii inawashirikisha pia watu wenye mapenzi mema ambao wanaweza pia kuchangia ili kuokoa maisha ya watoto wengi sehemu mbali mbali za dunia.







All the contents on this site are copyrighted ©.