2013-04-23 07:45:02

IMF na WB watangaza vita dhidi ya baa la umaskini hadi kufikia mwaka 2030!


Shirika la Fedha Kimataifa na Benki ya Dunia kwa pamoja, wameamua kulivalia njuga baa la umaskini wa kipato duniani ili ifikapo mwaka 2030 liwe limepunguzwa walau kwa asilimia 3% ya idadi ya watu duniani.

Hii ni sawa na watu billioni mbili. Hayo yamo kwenye taarifa ya pamoja iliyotiwa mkwaju na Mashirika haya fedha kimataifa katika mkutano wa wanachama uliojadili kuhusu maendeleo endelevu kwa kuzijumuisha nchi wanacahama 25.

Wadau wa maendeleo wanabainisha kwamba, mkakati huu unapania kuweka historia kwa Jumuiya ya Kimataifa katika mapambano dhidi ya baa la umaskini duniani. Hadi sasa kuna jumla ya watu billioni moja, laki mbili na hamsini ambao bado wanaogelea kwenye umaskini wa kutupwa, kadiri ya takwimu za Benki ya Dunia zilizotolewa kunako mwaka 2010.

Lakini wachunguzi wa masuala ya maendeleo wanasema, pengine takwimu hizi hazioneshi hali halisi ilivyo kwani kumekuwepo na maendeleo makubwa katika harakati za utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo ya Millenia ifikapo mwaka 2015. Itakumbukwa kwamba, kwenye miaka ya 1990 baa la umaskini lilikuwa linawaandama asilimia 43% ya idadi ya watu duniani.

Viongozi wakuu wa Mashirika ya Fedha Duniani wanaonesha matumaini ya kuweza kufanikiwa kupunguza baa la umaskini ifikapo mwaka 2030. Ili kufanikisha mikakati hii kuna haja kwa Serikali mbali mbali kuwa sera makini zinazozalisha na kulinda fursa za ajira kwa wananchi wake.

Idadi ya watu wasiokuwa na fursa za ajira duniani kwa sasa imefikia watu millioni 198, kati yao kuna vijana millioni 74; hali ambayo Shirika la Kazi Duniani linasema kwamba, kwa hakika idadi hii inatisha.







All the contents on this site are copyrighted ©.