2013-04-22 08:18:36

Changamoto zinazoikabili Jumuiya ya Kimataifa kuhusiana na uhuru wa kuabudu


Uhuru wa kuabudu katika ulimwengu mamboleo ni mada iliyochambuliwa na washiriki wa kongamano la kimataifa kuhusu uhuru wa kidini lililofanyika mjini Vatican kwa kuandaliwa na Wanamtandao wa ”Technology, Entertainment, Design”, TED chini ya udhamini wa Baraza la Kipapa la Utamaduni. RealAudioMP3

Kongamano hili limehudhuriwa na watu kutoka medani mbali mbali za maisha, taaluma na imani.

Kardinali Gianfranco Ravasi, Rais wa Baraza la Kipapa la Utamaduni katika mada yake amesisitiza swala la jamii ya binadamu kujifunza kuishi pamoja kama ndugu na kinyume chake ni maangamizi ya pamoja. Maneno haya yanaonesha umuhimu wake hasa katika nyakati hizi. Anasema kwamba, uhuru wa kuabudu si jambo la hiari bali ni jambo la lazima na ni kati ya haki msingi za binadamu.

Katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia, utamaduni wa kuishi pamoja na watu wenye imani tofauti ndilo jibu la msingi katika zama hizi za mwingiliano wa watu wanaotoka nchi mbali mbali kila mtu akiwa na mila na desturi zake.

Kanisa Katoliki linaamini misingi ya uhuru wa kuabudu na haliwezi kufanya tofauti na hivyo kwa kuwa hali hiyo ndiyo inayoleta amani katika jamii. Uhuru wa kuabudu ni kiini cha mafundisho yake katika jamii kama linavyofundisha kwenye hati inayo husu hadhi ya mwadamu (Dignitate Humanae) inayosisitiza uhuru wa mtu kuabudu, na kwamba jambo hili halipaswi kuchanganywa na mmabo ya siasa kwa kuzingatia ukweli unaotokana na Mafundisho ya Yesu mwenyewe kwamba ni vyema kumpa Kaisari kilicho cha Kaisari na kumpa Mungu kilicho cha Mungu bila kuchanganya.

Mambo haya yanapotenganishwa hayamaanishi kwamba mwanadamu amegawanyika, bali yanaonesha hali ya kuziheshimu amari za kidunia na papo hapo kutoa kipaumbele kwa mambo yanayohusu dhamiri ya mtu mwenyewe. Katika mada yake ameendelea kusisitiza swala la uhuru wa mikusanyiko kwa ajili ya mambo ya ibada ambayo yanahusisha kufundisha, kuhubiri, kushuhudia pamoja na kushiriki katika mchakato wa Uinjilishaji mpya.

Kardinali Ravasi anasema kwamba, bado kuna nchi nyingi duniani ambako serikali zinazuia uhuru wa mtu kuabudu jambo ambalo ni kinyume si tu cha haki msingi za binadamu bali pia ni kukosa kuheshimu uhuru na hadhi aliyo nayo kila mwadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu; na nchi zingine zinabagua dini za wananchi wao na kuwawekea vikwazo vya makusudi ili wasiweze kuabudu. Sehemu mbalimbali za dunia kuna baadhi ya serikali zinajichukulia madaraka ya kuzuia mikusanyiko ya ibada na badala yake wanazipatia kipaumbele shughuli zingine za kijamii.

Baadhi ya Serikali zinajiingiza hata kwenye maswala ya maisha ya kila siku ya wananchi wao na mara pengine ni Serikali inaamua kuruhusu au kutoruhusu shughuli za kiibada kufanyika. Kuna watu wanatishiwa maisha kwa ajili ya imani yao, hasa wale ambao idadi yao ni ndogo zaidi. Kuna baadhi ya nchi ambako baadhi ya watu hawaruhusiwi kufanya sala binafsi wala kufundisha dini ya Kikristo, wafanyakazi wanalazimishwa kufuata mitazamo kinyume kabisa na dhamiri zao na hata wakati mwingine wanalazimishwa kukumbatia utamaduni wa kifo kwa vuitisho vya kufukuzwa kazi. Dhamana ya dini katika jamii yoyote ile ni kujenga jamii inayoishi kwa mshikamano na pendo na si kujenga chuki na misigano ya maisha.


Rabbi mkuu David Rosen wa Jumuiya wa Kiyahudi nchini Ireland, akitoa mchango wake katika Kongamano hilo ameelezea kwamba, kuna haja ya waamini wa dini mbali mbali kukuza mahusiano ya karibu katika kufahamiana; kuzifahamu imani za wengine na kuziheshimu.

Watu wa imani mbalimbali wataweza kufanya kazi kwa pamoja ikiwa wataweza kuondoa hisia hasi ambazo mara nyingi zinajengeka kwenye jamii kuhusu waamini wa dini tofauti. Uhuru wa kuabudu katika ulimwengu wa leo, unaonekana kutetereka kutokana na hali ya watu kutofahamiana na badala ya kutafuta mambo ambayo yanayojenga, kila mtu anajiona kuwa bora zaidi kuliko mwingine na mjuaji zaidi, mambo ambayo kimsingi yanasababisha chuki na uhasama ndani ya Jamii.

Anasema kwamba, katika maisha na utume wake kama Rabbi sehemu mbali mbali, na baada ya kushinda hali ya kujiona kwamba imani yake ilikuwa ya maana zaidi kuliko imani za wengine ambazo hata hakuzifahamu kabla, aliweza kushirikiana na baadhi ya viongozi wa dini mbalimbali kwa ajili ya kusaidia kuanza mchakato wa majadiliano ya kidini, ili kuweza kuleta maelewano katika jumuiya mbalimbali za waamini.

Anasema kuwa, ikiwa kila mtu atajitahidi kuuona uwepo wa Mwenyezi Mungu ndani ya kila mwanadamu, hapo kwa hakika, ataweza kumheshimu na kumpenda na kuingia katika ushirikiano na yeye, hali ambayo haiwezi kuacha kuleta mabadiliko katika jamii; kwani jukumu la kila mmoja wao ni kuhakikisha kwamba haki, usawa na amani vinakuwepo katika ulimwengu mamboleo.

Rabbi Mkuu David Rosen anaendelea kusisitiza kwamba kama mtu anathamini amana za kibinadamu kama vile utu, ili aoneshe uaminifu katika kile anachokiamini anatakiwa kuwa tayari kuingia katika majadiliano ya kina na watu wengine bila kujali tofauti zao.

Hili linatokana na ukweli kwamba, ikiwa watu wanang’ang’ania ubinafsi wao na hali ya kutokuelewana, vitendo vya jinai vitaongezeka badala ya kukumbatia majadiliano ya kidini na kiekumene ambayo yanatija zaidi katika utamaduni wa dini mbalimbali. Mara nyingi, dini imetumika vibaya kwa ajili ya mafao ya watu binafsi, na hili linatokana na ukweli kuwa kila mtu anajisikia kuwa na madaraka ya kutumia dini kwa manufaa yake binafsi, jambo ambalo ni hatari sana.

Padre Edward Daleng wa Shirika la Waaugustiani kutoka mjini Jos, Nigeria ameelezea ni jinsi gani Shirika la kitawa la Mtakatifu Augostini linavyojitahidi kusaidia shughuli za majadiliano ya kidini kati ya waamini wa dini ya kiislam na wale wa dini ya Kikristo. Anaeleza kwamba kumetokea hali ya kutoaminiana katika jamii ya Wanaigeria baada ya matukio ya kujitoa mhanga nchini humo kuongezeka kwa kasi.

Ili kuondokana na hali hiyo ya kutoaminiana, anasema kwamba Shirika la Mapadre wa Agostiniani, kwa kushirikiana na baadhi ya mashirika yasiyo ya kiserikali yanayofanya kazi nchini humo, yameamua kulivalia njuga swala hilo ili kulipatia suluhu ya uhakika.

Anasema, kunako mwaka 2005 Mapadre hao wakishirikiana na mashirika mbali mbali walianzisha programu ya maendeleo jamii: kwa kuanza na kujenga shule za msingi ambamo wanafunzi wanaotoka kwenye familia za dini ya Kiislam na wale wa kutoka kwenye dini za Kikristo wanasoma pamoja na kucheza pamoja. Vile vile wamefanikiwa kujenga shule za sekondari ambamo pia wanafunzi wa dini hizo mbili wanasoma pamoja kwa amani na utulivu mkubwa; wakijifunza utamaduni wa kukubali na kupokea tofauti zao kwani hao ndio watakao kuwa viongozi wa nchi yao kwa kizazi kijacho,

Jambo hili linasaidia kukuza utamaduni mpya, utamaduni wa majadiliano na amani. Kuna vituo kwa ajili ya kuwawezesha akina mama kwa kuwapatia kozi mbalimbali zinazowasaidia kujiaajiri ili kukidhi mahitaji yao na ya familia zao; vituo ambavyo kila mwaka vinapokea idadi ya akina mama wapatao 250.

Hata katika vituo hivi, kina mama wanaofadika na huduma hizo ni wale wanaotoka kwenye imani mbalimbali zikiwemo za kikristo na kiislam. Wote wanajifunza mambo kwa pamoja na kushirikishana vipaji vyao bila ubaguzi wowote. Mambo haya yanaleta utamaduni mpya katika jamii kwani kina mama hawa wanaporudi majumbani mwao wanajaribu kuelezea mambo mazuri wanayojifunza kutoka katika vituo hivyo, na hili, taratibu linaleta mwelekeo mpya na utamaduni wa kuthaminiana kila mtu katika utofauti wa imani yake, kiasi kwamba, wanawake wanakuwa kweli ni vyombo vya amani, upendo na mshikamano katika Jamii.

Katika kutafuta jinsi ya kuwasaidia vijana ili waweze kuelekeza nguvu zao katika mambo yanayowajenga na kukuza utamaduni wa kuheshimu tofauti za wengine, Shirika la Mapadre pamoja na wadau wao wameunda timu ya mpira kwa wavulana, ambayo inaundwa na vijana wa dini ya Kiislam pamoja na ile ya Kikrsto. Timu hiyo pia imekuwa ni kichocheo kwa baadhi ya viongozi wa dini ya Kiislam na ile ya Kikrsto kuungana na kufanya kazi pamoja katika harakati za kutaka kuondoa hisia za kutoaminiana, kupokeana wala kuheshimiana.

Juhudi zote hizi zinalenga kuleta upatanisho kati ya makundi mbalimbali kwenye jamii ya wananchi wa Nigeria. Jambo hili, taratibu linaanza kuonesha mafanikio yake kwani watu wameanza kurudisha imani kati yao. Amehitimisha mada yake kwa kutumia maneno ya Mtakatifu Augustino, Askofu na Mwalimu wa Kanisa aliyesema kwamba “Yule ambaye kweli anapenda amani, anawapenda hata maadui wa amani.”

Imeandaliwa na Sr. Gisela Upendo Msuya.









All the contents on this site are copyrighted ©.