Utakatifu na ukweli; upendo na mshikamano pamoja na Uinjilishaji mpya ndiyo changamoto
iliyopo kwa sasa!
Uchaguzi wa Baba Mtakatifu Francisko ni changamoto kubwa kwa waamini kutoka Amerika
ya Kusini kuchuchumilia utakatifu wa maisha; ukweli na umoja; upendo na mshikamano
pamoja na Uinjilishaji mpya. Haya ni mambo muhimu sana yanayopaswa kupewa msukumo
wa pekee katika mapambazuko ya Millenia ya tatu ya Ukristo.
Ni changamoto
inayotolewa na Kardinali Marc Ouellet, Rais wa Tume ya Kipapa ya Amerika ya Kusini,
kama sehemu ya kumbu kumbu ya mwezi mmoja tangu Baba Mtakatifu Francisko alipochaguliwa
kuliongoza Kanisa Katoliki. Huyu ni Papa wa kwanza kutoka Shirika la Wayesuit na Papa
wa kwanza kutoka katika nchi za Amerika ya Kusini.
Hili ni tukio la pekee
kabisa katika historia ya Kanisa Katoliki. Kutokana na ukweli huu, waamini na wananchi
kutoka Amerika ya Kusini wanapaswa kujisikia kuwa karibu zaidi na Khalifa wa Mtakatifu
Petro, ili Amerika ya Kusini iweze kuwa ni chemchemi ya matumaini mapya. Wajiunge
na kutengeneza mnyororo wa sala kwa ajili ya kumwombea Baba Mtakatifu Francisko katika
maisha na utume wake kwani kwa hakika anahitaji sala na sadaka yao.
Uwe ni
mwendelezo wa maombi yanayoendelea kutolewa na Baba Mtakatifu Francisko kwa watu mbali
mbali ili waweze kumsindikiza katika Sala zao. Baba Mtakatifu aweze kuwa karibu zaidi
na waamini aliokabidhiwa kwake na Kristo kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, akitoa kipaumbele
cha kwanza kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii ili waweze kuonja
na kufarijika na huruma na upendo unaobubujika kutoka kwa Kristo Mkombozi wa ulimwengu.
Kardinali
Marc Ouellet anawachangamotisha Maaskofu Katoliki kutoka Amerika ya Kusini kujiuliza
ndani mwao maana na dhamana ya utume wao Amerika ya Kusini, sehemu ambayo ina nafasi
ya pekee katika moyo wa Baba Mtakatifu Francisko. Ni mwaliko na changamoto ya kupiga
moyo konde na kusonga mbele kwa matumaini huku wakimtangaza na kumshuhudia Kristo
aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu. Mwishoni, anawaalika Maaskofu kuonesha
upendo na mshikamano wa dhati kwa Baba Mtakatifu Francisko.