2013-04-20 07:49:36

Ujumbe wa siku ya 50 ya kuombea Miito Mitakatifu ndani ya Kanisa kwa Mwaka 2013


Miito ni alama ya matumaini yanayosimikwa katika imani ndiyo kauli mbiu inayoongoza maadhimisho ya Jubilee ya miaka hamsini tangu Papa Paulo wa sita alipoanzisha rasmi Siku ya Kuombea Miito Duniani, inayoadhimishwa tarehe 21 Aprili 2013, sanjari na Maadhimisho ya Jubilee ya miaka hamsini ya Mtaguso Mkuu wa Pili wa Vatican na Mwaka wa Imani. Mavuno ni mengi lakini watenda kazi katika shamba la Bwana ni wachache. RealAudioMP3

Mama Kanisa anatambua uhaba wa miito ya Kipadre kielelezo wazi cha imani na upendo unajionesha katika maisha ya mtu binafsi, Parokia na Jumuiya za Kijimbo; hiki ni kipimo cha uhai wa Familia za Kikristo. Pale ambapo kuna idadi kubwa ya miito ya kipadre na kitawa hapo kwa hakika anasema Papa Paulo wa sita kuwa watu wanaoishi Injili kwa moyo wa ukarimu.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika ujumbe wake kwa Siku ya Kuombea Miito Duniani kwa Mwaka 2013 anasema kuwa kila mwaka ifikapo Jumapili ya nne ya kipindi cha Pasaka, waamini hukusanyika kwa ajili ya kuombea miito mitakatifu ndani ya Kanisa, changamoto kwa waamini kuonesha moyo wa ukarimu. Hili ni tukio ambalo limetoa kipaumbele cha pekee katika kuombea miito ya Kipadre na kitawa, kama chemchemi ya tasaufi, sala na mikakati ya kichungaji inayotekelezwa na waamini.

Baba Mtakatifu anaonesha matumaini makubwa kwa siku za usoni; matumaini ambayo yanapaswa pia kuongoza hali halisi ya maisha kwa nyakati hizi ambazo haziridhishi na zinaonesha mapungufu. Matumaini ya Kanisa kama ilivyokuwa kwa Waisraeli katika Agano la Kale, walipokuwa wanakabiliana na hali ngumu ya maisha hasa nyakati zile walipokuwa uhamishoni, walikumbuka ahadi za Mwenyezi Mungu kwa Mababa wa Imani, walionesha matumaini makubwa kiasi hata cha kuwashangaza.

Ndivyo ilivyotokea kwa Abraham alipoambiwa na Mwenyezi Mungu kwamba, atakuwa ni Baba wa Mataifa na kwa hakika Mungu Mwenyezi aliweza kutekeleza Agano lake kwa uaminifu mkubwa licha ya dhambi, gharika, kukombolewa kutoka utumwani na safari ya Waisraeli Jangwani kwa miaka arobaini.

Mwenyezi Mungu ameendelea kuwa ni mwaminifu kwa Agano Jipya na la Milele lililofanywa na Mwanaye Mpendwa Yesu Kristo kwa njia ya damu yake azizi; kwa kuteswa, kufa na kufufuka kutoka katika wafu. Mwenyezi Mungu katika nyakati za shida na magumu anaonesha nguvu yake katika historia ya ukombozi kwa kuibua watu ambao waliamsha matumaini kwamba, siku moja wataweza kuifikia Nchi ya Ahadi. Kwa hakika Mwenyezi Mungu hawezi kuwaacha waja wake anaendelea kuwa mwaminifu kwa neno lake. Hiki ndicho kiini cha matumaini ya Kanisa, katika hali njema au ugumu wa maisha.

Mwenyezi Mungu anaimarisha matumaini ndiyo maana mwamini anaweza kuimba na Mzaburi kwa kusema kwamba, moyo wangu unaweza kupata kitulizo kwa Mwenyezi Mungu kwani tumaini lake linatoka kwake. Kuwa na matumaini ni sawa na kujiaminisha kwa Mwenyezi Mungu ambaye ni mwaminifu ana anatekeleza Agano lake. Imani na matumaini ni fadhila ambazo zina uhusiano wa karibu. Imani ni neno la msingi katika Biblia kiasi kwamba wakati mwingine Imani na Matumaini yanaonekana kuwa ni maneno yanayoweza kutumika kwa pamoja

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, katika Ujumbe wake kwa Siku ya hamsini ya kuombea Miito Duniani kwa Mwaka 2013 anabainisha kwamba, uaminifu wa Mungu unajikita kwa namna ya pekee katika upendo ambao ameumimina kwa njia ya Roho Mtakatifu, ukajionesha kwa njia ya Kristo na kwamba unahitaji kupata jibu la uhakika kutoka kwa waamini ili kuweza kuishi kwa ukamilifu zaidi. Matumaini yanarutubishwa na upendo wa Mungu kwa waja wake unaowakirimia ujasiri na matumaini katika hija ya maisha yao, kiasi hata cha kuweza kujiamini kwa siku za usoni, katika historia na miongoni mwa watu wengine.

Baba Mtakatifu anapenda kuwakumbusha vijana umuhimu wa upendo wa Mungu unaojionesha tangu kuumbwa kwa ulimwengu na utakaofikia ukomo wake nyakati za mwisho, atakapokamilisha kazi ya ukombozi. Kanisa lina imani thabiti kwa njia ya Kristo Mfufuka anayeendelea kufanya hija ya wafuasi wake ambao wamezama katika shughuli mbali mbali, wakiwa na matarajio na mahitaji yao. Lakini Kristo anaendelea kuwaita na kuwakaribisha ili kuishi pamoja naye kwani ana uwezo wa kuzima kiu ya matumaini yao ya ndani.

Yesu anaendelea kuishi katika Jumuiya ya Waamini ambao ni Kanisa na anawaita watu kwa nyakati mbali mbali kumfuasa. Kwa kukubali wito wake kuna maanisha kwamba, hakuna tena uwzekano wa kufuata njia nyingine. Hiki ni kitendo cha kutoa utashi wao kwa ajili ya kutekeleza utashi wa Kristo; kwa kutoa kipaumbele cha kwanza katika medani mbali mbali za maisha: ndani ya familia, sehemu za kazi, na katika mambo binafsi. Ni mwaliko wa kujitoa bila ya kujibakiza ili kuunganika na Fumbo la Utatu Mtakatifu pamoja na jirani zao. Umoja wa maisha katika yesu ni mahali ambapo mwamini anaweza kuonja tumaini na utimilifu wa maisha na uhuru kamili.

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita anaendelea kusema kwamba, miito ya upadre na maisha ya kuwekwa wakfu yanapata chimbuko lake kwa mang’amuzi ya mtu anayekutana na Yesu katika hija ya maisha yake; ni chimbuko la majadiliano ya kweli na thabiti na Kristo, ili kuingia katika utashi wake. Ni muhimu kuendelea kukua katika mang’amuzi ya imani, yanayofahamika kuwa ni uhusiano wa dhati kabisa na Yesu na kuwa makini kusikiliza sauti yake inayozungumza kutoka katika undani wa mtu.

Mchakato unaomwezesha mtu kutoa jibu chanya kwa wito kutoka kwa Mungu unawezekana tu katika Jumuiya za Kikristo ambamo imani inamwilishwa kwa ukamilifu kabisa; mahali ambapo ushuhuda wa ukarimu unajidhihirisha kwa kujishikamanisha na Injili; kwa kuonesha umuhimu wa utume unaowaongoza watu kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Ufalme wa Mungu, kwa kulishwa na Sakramenti za Kanisa, hususan Ekaristi Takatifu na maisha ya sala. Sehemu hii ya mwisho inapaswa kuonesha uhusiano wa mtu binafsi na Mungu aliye hai. Kwa upande mwingine, sehemu hii haina budi kuongozwa na Sala kuu ya Kanisa, Watakatifu na katika Sala ya Liturujia ambamo Kristo anawafundisha waamini kusali vyema.

Baba Mtakatifu anawaalika waamini kujenga utamaduni wa kusali daima kama njia ya kukuza imani ya Jumuiya za Kikristo kwa kuamini kwamba, Mwenyezi Mungu kamwe hawezi kuwatupa waja wake na ataendelea kuwaongoza na kuchipusha miito ya upadre na maisha ya kitawa kama alama ya tumaini duniani. Mapadre na Watawa wanachangamotishwa na Mama Kanisa kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya Watu wa Mungu, katika huduma ya upendo kwa Injili na Kanisa kwa kuhudumia tumaini linalowezekana kwa kujiachilia wazi kwa ukuu wa Mungu.

Kwa njia ya ushuhuda wa imani na ari katika utume, wanaweza kurithisha hasa miongoni mwa vijana wa kizazi kipya hamu ya kujibu kwa ukarimu na kwa utayari wito wa Kristo unaowaalika kumfuasa kwa ukaribu zaidi. Mfuasi yeyote wa Kristo anapoamua kujitoa kikamilifu katika maisha na utume wa Kipadre au Maisha ya kuwekwa wakfu, Kanisa linashuhudia matunda ya ukomavu wa Jumuiya ya Kikristo, inayowawezesha kuamini na kuwa na matumaini kwa Kanisa katika siku za usoni; ili kuadhimisha Sakramenti ya Ekaristi Takatifu na Upatanisho.

Baba Mtakatifu anawaalika Mapadre kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya kuwaongoza katika hija ya maisha yao, kwa kuwasaidia kupambana na magumu, ili hatimaye, waweze kumtambua Yesu ambaye ni Njia, Ukweli na Uzima. Wawaambie kwa ujasiri wa Injili inavyopendeza kumtumikia Mwenyezi Mungu, Kanisa pamoja na kuwahudumia ndugu na jamaa zao. Wawepo Mapadre wanaoonesha matunda ya kujitoa bila ya kujibakiza kwa kuonesha utimilifu wa maisha yanayopata msingi wake katika Imani kwa Kristo ambaye aliwapenda upeo!

Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita anahitimisha ujumbe wake kwa Siku ya hamsini ya Kuombea Miito Duniani kwa kuonesha matumaini yake kwamba, vijana ambao wanaoneshwa mambo mengi kwa juu juu tu pamoja na kuwa na chaguzi nyingi katika maisha yao, wataweza kukuza hamu ya kuwa na kitu chema zaidi, malengo thabiti na uchaguzi makini na huduma kwa wengine kwa kumuiga Yesu.

Anawataka vijana wa kizazi kipya kutoogopa kumfuasa na kutembea katika nyayo zake zinazohitaji kwa namna ya pekee upendo na majitoleo ya ukarimu. Kwa njia hii wataweza kutumikia kwa furaha na kutolea ushuhuda wa ile furaha ambayo kamwe haiwezi kutolewa na Ulimwengu; watakuwa ni mwanga wa upendo wa Mungu na watajifunza kutoa ushuhuda wa tumaini lililoko ndani mwao!

Imehaririwa na Padre Richard Mjigwa, C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.