2013-04-20 08:00:57

Familia ni amana ambayo haina mbadala!


Baraza la Maaskofu Katoliki Ureno linaangalisha kwamba, familia ni tunu ambayo haina mbadala ni chemchemi na mhimili mkuu wa nguvu kazi: kiroho, kijamii na kiuchumi kwa taifa lolote lile. Ni taasisi nyeti na ambayo inapaswa kupewa kipaumbele cha kwanza. RealAudioMP3

Katika kukabiliana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa, kuna haja kwa Jamii kuonesha mshikamano wa dhati na familia ili ziweze kutekeleza wajibu na dhamana yake katika Kanisa na Jamii kwa ujumla wake. Mshikamano huu ujengeke kati ya vijana wa kizazi kipya na wazee ambao ni hazina kubwa katika Jamii na kamwe wasiwatenge na kuwabeza.

Mshikamano huu ni muhimu sana hasa kwa wale watu ambao amepoteza fursa za kazi kutokana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa na kwa sasa wanakabiliana na hali ngumu ya uchumi. Changamoto hii imetolewa hivi karibuni na Baraza la Maaskofu Katoliki Ureno katika mkutano wake wa Mwaka uliofanyika mjini Lisbon.

Mshikamano wa upendo uanzie ndani ya Familia yenyewe kwa ndugu na jamaa kusaidiana na hatimaye kuvuka mipaka na kuwagusa majirani na Jamii katika ujumla wake. Familia za Kikristo zinaalikwa kwa namna ya pekee kuwa kielelezo cha upendo na mshikamano na wale wote walioathirika kutokana na myumbo wa uchumi kimataifa. Sera na mikakati ya kuinua uchumi nchini Ureno imegonga mwamba kwani taasisi za fedha na uzalishaji zilijikita katika kutafuta faida kubwa wakasahau kuwekeza katika Familia na matokeo yake ni kuzorota kwa ulaji na utoaji wa huduma za kijamii.

Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, katika ujumbe wake kwa Maadhimisho ya Siku ya Amani Duniani kwa Mwaka 2013, alionya kwamba, katika kipindi cha miaka ya hivi karibuni, kumeibuka ubinafsi, ulaji wa kutisha na sera nyingi za kiuchumi zinatafuta faida kubwa hata kwa gharama ya maisha ya watu. Kumekuwepo na ushindani usiokuwa na tija na matokeo yake ni kuzorota kwa uchumi.

Maaskofu Katoliki Ureno wanakumbusha kwamba, mafanikio yanapatikana kwa kufanya kazi kwa juhudi, akili na maarifa. Mshikamano wa kidugu na mafao ya wengi ni mambo yanayopaswa kupewa msukumo wa pekee katika sera na mikakati ya maendeleo endelevu inayozingatia mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili. Familia ziwe ni kitovu cha upendo, kwa watu kukaribishana na kusaidiana.

Viongozi watambue kwamba, madaraka waliyo nayo ni dhamana ambayo wamekabidhiwa na umma kwa ajili ya kutoa huduma ya upendo na mshikamano hasa kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii. Hawa ndio wagonjwa, wazee na wote wenye kuhitaji msaada kutoka katika Jamii. Viongozi wahakikishe kwamba, wanatumia vyema rasilimali ya nchi ili kuleta maboresho katika sekta ya elimu, afya na maendeleo endelevu.

Maaskofu Katoliki Ureno wanasema kwamba, ili Familia iweze kutekeleza wajibu wake barabara katika Kanisa na Jamii, haina budi kuheshimiwa, kuthaminiwa na kuwezeshwa kwa hali na mali. Takwimu za hivi karibuni zinaonesha kwamba, Ureno ni kati ya nchi zenye idadi ndogo sana ya watoto wanaozaliwa duniani. Kuna mwingiliano mkubwa kati ya idadi ya watu na uhusiano wa kijamii.

Kuna haja ya kuwekeza zaidi katika Familia si katika hali ya kujisikia, bali kwa kujitoa kimasomaso kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Familia. Kwa hakika wanasema Maaskofu Katoliki wa Ureno kuna haja ya kuwekeza pia katika Injili ya Uhai.








All the contents on this site are copyrighted ©.