Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lajadili kuhusu: wanawake, amani na usalama
Askofu mkuu Francis Chullikatt, mwakilishi wa kudumu wa Vatican kwenye Umoja wa Mataifa,
hivi karibuni ameshiriki katika mkutano wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lililojadili
kuhusu wanawake, amani na usalama.
Anasema, tangu mwaka 2000 Umoja wa Mataifa
umekuwa ukifuatilia kwa umakini mkubwa kuhusu mchango wa wanawake katika kujenga na
kudumisha misingi ya haki na amani, jambo linalohitaji kuwajengea wanawake uwezo mkubwa
zaidi ili kuweza kukabiliana na changamoto mbali mbali katika Jamii zao.
Wanawake
wakiwezeshwa wanaweza kusaidia kuzuia vita, kujenga msingi wa upatanisho na maridhiano
ya Kijamii na kwamba, wao ni wadau wakuu na vyombo vya amani duniani.
Askofu
mkuu Chullikatt anasema inasikitisha kuona kwamba, bado wanawake wengi wanatumbukizwa
kwenye utumwa mamboleo, nyanyaso za kijinsia, biashara haramu ya binadamu pamoja na
matumizi haramu ya dawa za kulevya. Wanawake ni waathirika wakuu katika kinzani za
kikabila, kiuchumi na kisiasa na kidini. Baadhi ya watu wanaofanya vitendo hivi wakati
mwingine wanatoka kwenye Serikali, Vyombo vya Ulinzi na Usalama au kwenye Majeshi
ya kulinda amani ya Umoja wa Mataifa.
Hivi ni vitendo vinavyodhalilisha utu
na heshima ya binadamu na kwamba, kuna baadhi ya Jamii na Makundi ya watu wametumia
vitendo hivi kama silaha ya vita. Ujumbe wa Vatican kwenye Baraza la Usalama la Umoja
wa Mataifa unamesisitizia umuhimu wa kuzuia vitendo vya uvunjaji wa sheria; kwanza
kabisa kwa kuhakikisha kwamba, sababu ya vita na kinzani za kijamii zinabainishwa
na kutafutiwa ufumbuzi wa kudumu, kwani vita vingi ni kutokana na hali ngumu ya kiuchumi
na kijamii. Kuna haja ya kuwekeza katika elimu, maadili na utu wema pamoja na kuwa
na mwono sahihi kuhusu dhana ya wanawake katika Jamii.
Wahusika wa vitendo
hivi vya jinai wanapaswa kuchukuliwa hatua madhubuti kwa kufikishwa kwenye mkondo
wa sheria, ili haki iweze kutendeka. Pale ambapo Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa
linahusika moja kwa moja, basio hatua za haraka ziweze kuchukuliwa kwa kuzingatia
haki na usawa na wala si kusukumwa na sababu za kisiasa mambo ambayo yanaweza kukwamisha
juhudi za Umoja wa Mataifa katika kupambana na vitendo vinavyodhalilisha utu na heshima
ya binadamu.
Waathirika wa vitendo hivi wanapaswa kupewa fidia jambo ambalo
halikubainishwa kinaga ubaga kwenye taarifa ya Umoja wa Mataifa katika mkutano wa
Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa. Waathirika wahudumiwe kwa dhati ili kuponya
undani wa madonda haya yanayoacha kurasa chungu katika maisha ya waathirika wa vitendo
vya dhuluma za kijinsia. Jumuiya ya Kimataifa ijali na kuheshimu zawadi ya uhai na
kamwe isikimbilie kutoa ushauri unaokumbatia utamaduni wa kifo kwa kisingizio cha
mimba zisizotarajiwa.
Mama na mtoto wake ambaye bado yuko tumboni wahudumiwe,
wasaidiwe na kupatiwa elimu, ushauri pamoja na kupatiwa huduma mbali mbali zitakazomsaidia
Mama na mtoto wake: kiroho na kimwili. Pale inapowezekana juhudi zifanyike kutafuta
familia itakayoasi mtoto anayezaliwa katika mazingira magumu na dhuluma za kijinsia,
kwani maisha ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu.
Askofu mkuu Francis Chullikatt,
Mwakilishi wa kudumu wa Vatican kwenye Umoja wa Mataifa anahitimisha mchango wa ujumbe
wake kwenye mkutano wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kwa kutaka Jumuiya ya
Kimataifa kuwekeza zaidi katika kulinda na kudumisha misingi ya haki na amani miongoni
mwa Jamii na kwamba, amani ya kweli inabubujika kutoka katika moyo wa mwanadamu. Jamii
ijifunze kuenzi zawadi ya maisha kwa kusimama kidete kulinda na kutetea utu na heshima
ya kila binadamu aliyeumbwa kwa sura na mfano wa Mungu.