2013-04-19 11:22:36

Siku ya Nne ya Sarakasi Kimataifa kwa mwaka 2013


Kardinali Antonio Maria Veglio', Rais wa Baraza la Kipapa la wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum, anaungana na Jumuiya ya Wanasarakasi Kimataifa katika Maadhimisho ya Siku ya Nne ya Sarakasi Kimataifa, hapo tarehe 20 Aprili 2013 chini ya udhamini wa Mtoto wa Mfalme Stephanie wa Montecarlo. Hayo yamo kwenye ujumbe ambao Kardinali Veglio' amemtumia Dr. Urs Ilz, Rais wa Shirikisho la Wanasarakasi Ulaya na Duniani katika ujumla wake.

Anawashukuru wote waliowezesha kufanikisha tukio hili ambalo linawakusanya Wanasarakasi kutoka pembe mbali mbali za dunia na hivyo kuvuka vikwazo vya kitamaduni na kijamii, ili kujenga Jumuiya moja ya Kimataifa. Maadhimisho haya ni changamoto kwa watu wenye mapenzi mema kukuza na kudumisha mshikamano wa kidugu, ushuhuda unaotolewa na kuhifadhiwa kwa namna ya pekee na Jumuiya ya Wanasarakasi.

Ni Maadhimisho yanayoonesha umoja na majadiliano; uwazi na ukarimu mambo yanayowagusa watu wenye umri tofauti wanaounda Jumuiya hii na kuwa ni sehemu ya utambulisho na wito wake. Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, Mwezi Desemba 2012 alipata nafasi ya kukutana na kuzungumza na Wanasarakasi wa Kimataifa mjini Vatican, aliwapongeza kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa familia, watoto wadogo, watu wenye ulemavu; huduma kwa wagonjwa pamoja na kuwathamini wazee kama sehemu ya amana na urithi mkubwa katika mafanikio ya michezo yao.

Ni Jumuiya inayojikita katika majadiliano ya kina, urafiki na mshikamano wa kazi kama timu moja Huu ndio utajiri na amana inayooneshwa na Wanasarakasi kutoka sehemu mbali mbali za dunia katika Maadhimisho ya Siku ya Nne ya Sarakasi Kimataifa. Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, kwa wakati ule aliwapongeza kwa weledi na ufanisi mkubwa wa shughuli zao kimichezo, jambo ambalo linahitajika hata katika ulimwengu mamboleo.

Kardinali Veglio' anasema kwamba, Mama Kanisa anatambua mchango wa Wanasarakasi, lakini kwa namna ya pekee, vikundi vinavyoendelea kuchangia kwa hali na mali katika kuwasaidia watu waliofikwa na: vita, maafa pamoja na majanga kutoka sehemu mbali mbali za dunia. Vikundi hivi vimekuwa ni faraja kwa watoto, wazee, kiasi cha kuwakirimia na kuwaonjesha amani na utulivu wa ndani, furaha na upendo.

Baba Mtakatifu Francisko, katika mahubiri mwanzo wa utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro alikazia umuhimu wa waamini kuwa ni vyombo vya matumaini mapya, kwa kulinda, kuheshimu na kutunza kazi ya uumbaji, ili kuendeleza; heshima, urafiki na mafao ya wengi. Kanisa linawaangalia Wanasarakasi kwa moyo wa matumaini kutokana na ukweli kwamba wanajitahidi kutumia karama na vipaji vyao kwa ajili ya ujenzi wa Jumuiya ya Kimataifa na mshikamano wa dhati kati ya watu na Jamii zao.







All the contents on this site are copyrighted ©.