2013-04-19 08:03:26

Papa asema ameguswa na mahangaiko ya wanawake wa Argentina


Baba Mtakatifu Francisko anasema yuko karibu na akina mama wote waliopoteza watoto na wapendwa wao wakati wa utawala wa kidikteta wa nchini Argentina. Anawataka wanawake wa Argentina kupiga moyo konde, kuwa na ujasiri na matumaini mapya katika maisha yao na anawaomba kwa namna ya pekee kusali pia kwa ajili ya maisha na utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Ni ujumbe ulioandikwa kwa niaba ya Baba Mtakatifu Francisko na Monsinyo Antoine Camilleri,Katibu mwambata anayeshughulikia uhusiano wa kimataifa mjini vatican kama jibu la barua kutoka kwa wanawake wa Argentina wanaojulikana kama "Madri di Plaza de Mayo".

Baba Mtakatifu anawaalika wanawake wa Argentina kumsindikiza katika utume wake na kwa namna ya pekee, aweze kuchangia kwa katika mchakato wa kupambana na baa la umaskini duniani pamoja na kuleta faraja kwa wote wanaoteseka kiroho na kimwili.

Baba Mtakatifu katika ujumbe huu anawapongeza wale wote wanaojitosa katika mchakato wa kuwajengea maskini uwezo ili kukabiliana na changamoto mbali mbali za maisha; ni vyema kufahamu matatizo yao, kuwaelewa na kuwasaidia kupata ufumbuzi wa changamoto hizi pale inapowezekana.

Baba Mtakatifu anawataka viongozi wa Jumuiya ya Kimataifa kujifunga kibwebwe kutafuta kwanza kabisa mafao ya wengi pamoja na kupambana kufa na kupona dhidi ya umaskini, kwa kutumia njia muafaka zinazojali usawa na mshikamano wa kidugu.







All the contents on this site are copyrighted ©.