2013-04-19 07:40:08

Mtumishi wa Mungu Padre Nicolo' Rusca kutangazwa kuwa Mwenyeheri


Kardinali Angelo Amato, Mwenyekiti wa Baraza la Kipapa la kuwatangaza waamini kuwa wenyeheri na watakatifu, tarehe 21 Aprili, 2013, Jumapili ya nne ya Kipindi cha Pasaka, maarufu kama Jumapili ya Kristo mchungaji mwema, kwa niaba ya Baba Mtakatifu Francisko, anatarajia kumtangaza Mtumishi wa Mungu Padre Nicolo’ Rusca kuwa Mwenyeheri katika Ibada ya Misa Takatifu itakayofanyika kwenye Kanisa la Sondrio mahali ambako kwa miaka thelathini aliwahudumia waamini kama Kasisi mkuu. RealAudioMP3

Wakati wa machafuko ya kidini kati ya Wakatoliki na Madhehebu ya Kipentekoste katika miaka ya 1600, alikamatwa, akafungwa na kuteswa sana gerezani na hatimaye, akauwawa kikatiliki kutokana na chuki za kidini dhidi ya Imani ya Kanisa Katoliki. Akimwelezea Mwenyeheri Padre Nicolo’ Rusca, Baba Mtakatifu Francisko anasema kwamba, ni kiongozi na mchungaji mwema, aliyejitoa bila ya kujibakiza, akatekeleza wajibu na utume wake wa kuwahudumia Kondoo wake mintarafu mapenzi ya Kristo, kiasi hata cha kuyamimina maisha yake kwa ajili ya imani kwa Kristo na Kanisa lake.

Mwenyeheri Padre Nicolo’ Rusca alizaliwa kunako mwaka 1563 huko Canton Ticino, Kaskazini mwa Italia. Baada ya karne nne, Mama Kanisa ametambua ushujaa, ari na imani thabiti na sasa anamtangaza kuwa ni Mwenyeheri kama sehemu ya mchakato wa kumtangaza kuwa Mtakatifu wakati utakapowadia kama kielelezo cha imani thabiti. Miaka mingi imepita, lakini bado watu wengi wanamkumbuka kutoka na utakatifu wa maisha ambao kamwe haukuweza kupitwa na wakati.

Kardinali Amato anasema kwamba, Mwenyeheri Padre Nicolo’ ni kielelezo cha mwamini ambaye alijitoa bila ya kujibakiza, akasimama kidete kutolea ushuhuda wa imani yake kwa Kristo na Kanisa lake kwa njia ya madhulumu. Jambo hili linaonesha maana na umuhimu wa mwanga wa imani na ile kiu ya kutaka kufahamu ukweli kuhusu Mwenyezi Mungu. Hata katika matukio ya kibinadamu, Mwenyezi Mungu anaendelea kujifunua kwa watu wake, ili waweze kuutambua na kuushuhudia ukweli.

Mwenyeheri Padre Nicolo’ ameuwawa kutokana na chuki za kidini, changamoto kwa waamini wa dini mbali mbali kujenga na kudumisha misingi ya haki, amani, upendo na mshikamano. Kwa pamoja waendeleze majadiliano ya kidini na kiekumene, kwa kujikita katika upatanisho wa kweli unaojionesha kwa namna ya pekee katika maisha ya waamini wenyewe.

Watu wajenge utamaduni wa kuheshimiana, kuthaminiana na kusaidiana wakitambua kwamba, wote wameumbwa kwa sura na mfano wa Mungu, tofauti zao za kidini ziwe ni cheche ya upendo na mshikamano wa dhati. Wakristo washikamane kutangaza Habari Njema ya Wokovu kwa njia ya ushuhuda wa maisha yao pamoja na kujitahidi kuvunjilia mbali kuta za utengano ambazo bado zinaendelea kuleta ukakasi katika maisha.

Kardinali Angelo Amato anakumbushia kwamba, watakatifu ni mashujaa wa imani waliyotolea maisha yao kwa ajili ya Kristo na Kanisa lake. Ni mashujaa wanaoendelea kuwachangamotisha waamini kutambua na kuthamini uwepo wa Mungu katika hija ya maisha yao ya kila siku: Waoneshe jambo hili kwa njia ya ushuhuda wa maisha adili, manyofu na matakatifu. Kila mwamini anaalikwa kuwa ni Mtakatifu.








All the contents on this site are copyrighted ©.