2013-04-18 11:03:34

Tokeni kifua mbele kumtangaza na kumshuhudia Kristo Mfufuka!


Mama Kanisa anawajibu na dhamana ya kuwakuza na kuwalea watoto wake katika misingi ya imani, maadili na utu wema, tayari kutoa ushuhuda wa imani hii kwa Kristo na Kanisa lake; wakitoka kifua mbele kwenda kutangaza Habari Njema ya Wokovu, ili watu waweze kumfahamu, kumpenda na kumtumikia Kristo, ili siku moja waweze kufika kwake mbinguni.

Huu ndio muhtsari wa tafakari ya kina iliyotolewa na Baba Mtakatifu Francisko katika Maadhimisho ya Ibada ya Misa Takatifu iliyofanyika kwenye Kikanisa cha Domus Sanctae Marthae na kuhudhuriwa na Wafanyakazi wa Benki ya Vatican. Itakumbukwa kwamba, tangu Baba Mtakatifu alipochaguliwa kuwa Khalifa wa Mtakatifu Petro ameendelea bado kuishi na kusali na waamini mbali mbali kwenye Kikanisa cha Domus Sanctae Marthae kama sehemu ya kufahamiana pia na wafanyakazi mbali mbali wanaotoa huduma mjini Vatican.

Mwanzoni, Wakristo wa mwanzo walibahatika kuishi kwa amani, umoja na upendo kati yao, wakishirikishana na kumegeana utajiri wa Neno la Mungu na kazi ya mikono yao. Lakini madhulumu yalipoanza kujitokeza, walijikuta wakisambaratika sehemu mbali mbali za dunia ya wakati ule na huu ukawa ni mwanzo wa Uinjilishaji wa Mataifa. Baba Mtakatifu Francisko anakumbusha kwamba, daima Kanisa limeendelea kujengeka na kuimarika katika misingi mikuu mitatu: amani, upendo na madhulumu.

Ni wakristo waliokuwa wamebatizwa na kuimarishwa kwa njia ya Roho Mtakatifu, waliojitosa ulimwenguni ili kuwainjilisha walimwengu, wakati ambapo Mitume wa Yesu na viongozi wengine wa Kanisa walikuwa mjini Yerusalemu wakipambana na dhuluma hizi mbele ya viongozi wa Serikali. Wakristo walikuwa wamebeba ndani mwao amana ya imani, iliyowafanya kuaminiwa na wenyewe kuwa na uwezo wa kutenda miujiza na watu wengi wakajazwa furaha ya kusikia Habari Njema ya Wokovu ikitangazwa masikioni mwao.

Ile nguvu ya Ubatizo na Roho Mtakatifu viliwajaza Wakristo wa mwanzo ujasiri wa pekee kabisa, kiasi kwamba, wakachangamotishwa Kuinjilisha kwa ari na moyo mkuu. Neno la Mungu katika kipindi hiki cha Pasaka kuhusu maisha ya Wakristo wa kwanza, liwe ni changamoto ya kutoka kwa ujasiri kutangaza Injili ya Kristo kwa maneno, lakini zaidi kwa njia ya ushuhuda wa maisha, daima wakijitahidi kuwa ni waaminifu kwa Kristo, Roho Mtakatifu na Kanisa.

Baba Mtakatifu anaonya kwamba, Kanisa si kama "Babysitter" aliyepewa dhamana ya kubembeleza mtoto na hatimaye, kusinzia na kulala usingizi mzito. Wakristo wamepewa dhamana na wajibu wakati walipopokea sakramenti ya Ubatizo, changamoto iliyoko mbele yao ni kutekeleza wajibu na dhamana hii kwa ari na ujasiri mkuu.







All the contents on this site are copyrighted ©.