Ujenzi wa Kituo cha Familia Takatifu Kimataifa waanza
Mwenyeheri Yohane Paulo wa Pili katika Maadhimisho ya Siku ya Vijana Duniani iliyofanyika
mjini Rio de Janeiro kunako mwaka 1997, alisema kwamba, angependa kukumbukwa katika
uongozi wake kama mtu ambaye alijitoa kimasomaso kwa ajili ya kulinda na kutetea tunu
bora za maisha ya kifamilia. Hapo wazo la kuanzisha Kituo cha Familia Kimataifa mjini
Yerusalemu, likakua na kuanza kushika kasi taratibu.
Wazo hili likamwilishwa
na Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita, kunako tarehe 14 Mei 2009 wakati wa hija
yake ya kichungaji kwenye Nchi Takatifu; siku hiyo akaweka jiwe la msingi pale mjini
Galileya. Ujenzi ukaendelea kushika kasi na kwa namnaya pekee wakati wa Maadhimisho
ya Siku ya Saba ya Familia Kimataifa iliyofanyika Jimbo Kuu la Milano, mwezi juni
2012, mradi huu ukawa umeanza kutekelezwa rasmi.
Baraza la Kipapa la Familia
likaukabidhi mradi huu kwa Mheshimiwa Salvatore Martìnez, Rais wa Chama cha Kitume
cha Uamsho wa Roho Mtakatifu nchini Italia.
Haya yamesemwa na Askofu mkuu Vincenzo
Paglia, Rais wa Baraza la Kipapa la Familia katika uzinduzi wa Kituo cha Familia Takatifu
Kimataifa mjini Yerusalemu kitakachokuwa ni mfano na kielelezo cha ujenzi na uimarishaji
wa tunu msingi za maisha ya kifamilia.
Hapa watu wataweza kuchota kutoka katika
chemchemi ya Familia Takatifu, tasaufi ya maisha ya kifamilia, mikakati ya kichungaji
ya familia na kituo maalum cha kuonesha mshikamano wa upendo na familia ambazo zinakabiliana
na hali ngumu ya maisha: kiroho na kimwili.Huu ni mwendelezo wa mikakati ya Baraza
la Kipapa la Familia linalotaka kuwekeza zaidi katika majiundo ya maisha bora ya kifamilia,
ili familia ziweze kusimama kidete kulinda na kutetea dhamana na utume wao ndani ya
Kanisa na Jamii kwa ujumla.
Askofu mkuu Vincenzo Paglia anasema Familia inapaswa
kupewa kipaumbele cha kwanza, kwa kuhakikisha kwamba, Familia inapata fursa ya kusoma,
kutafakari na kulimwilisha Neno la Mungu katika matendo ya huruma. Kwa maneno mengine,
Neno la Mungu linapaswa kuwa ni kiini cha maisha ya kifamilia. Bila kuwa na familia
madhubuti, Jamii itaweza kuyumba sana.
Kwa bahati mbaya, katika ulimwengu
wa maendeleo ya sayansi na teknolojia na utandawazi familia imekuwa ni kati ya taasisi
zinazokabiliwa na kinzani kutoka kila upande, na matokeo yake, familia nyingi zimejikuta
zinaogelea katika migogoro na hali ya kukata tamaa kiasi cha kushindwa kutekeleza
dhamana na wajibu wake barabara.
Kwa upande wake, Dr. Salvatore Martìnez wakati
anazungumza na Waandishi wa Habari amebainisha kwamba, mradi huu unapania kumwilisha
kwa namna ya pekee, Mafundisho ya Kanisa kuhusu Familia, ili kujenga na kuimarisha
tunu bora za maisha ya kifamilia, kiutu na kijamii, ili familia za Kikristo ziweze
kujitosa kimasomaso katika azma ya Uinjilishaji mpya hasa katika Nchi Takatifu. Kwa
maneno mengine Kituo cha Kimataifa cha Familia Takatifu kinapania kuwa ni "Injili
ya Familia Kimataifa".
Ujenzi wa Kituo cha Familia Takatifu Kimataifa unatarajiwa
kukamilika katika kipindi cha miaka miwili na nusu, ikiwa kama mambo yote yatakawenda
kama ilivyopangwa kwa gharama ya Euro millioni kumi na mbili. Pamoja na kuwa na vyumba
vya mikutano kimataifa; Kituo hiki pia kitakuwa na Kikanisa chenye uwezo wa kuketisha
watu mia tano. Kituo pia kitakuwa na vyumba mia moja kwa ajili ya kutoa hifadhi kwa
familia zitakazokuwa zinafanya hija ya maisha ya kiroho kwenye Nchi Takatifu.
Dr.
Martìnez anasema kwamba, kwa hakika Kituo cha Familia Takatifu Kimataifa kitakuwa
ni mahali muafaka kabisa pa uenezaji wa Injili ya Familia Kimataifa. Tukio hili limehudhuriwa
na viongozi mbali mbali wa Kanisa kutoka katika Nchi Takatifu waliokuwa hapa mjini
Vatican.
Uamuzi wa Baraza la Kipapa la Familia kuwekeza katika Nchi Takatifu
ni changamoto ya kuendelea kuchota tunu msingi za maisha ya kifamilia kutoka katika
Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu, ili kujenga na kuimarisha misingi ya haki,
amani, upendo na mshikamano wa dhati, kwa kutambua kwamba, Familia ni chombo cha kwanza
cha kulinda na kutetea amani.