Hakuna ufufuko pasi na Msalaba; Kupaa kwenda mbinguni bila ya utii kwa Mwenyezi Mungu!
Baba Mtakatifu Francisko, Jumatano tarehe 17 Aprili 2013, akiwa kwenye Uwanja wa Kanisa
kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, aliendelea na Katekesi katika Maadhimisho ya
Mwaka wa Imani kwa kuchambua Kanuni ya Imani, kipengele kinachozungumzia kuhusu Yesu
Kupaa mbinguni. Katika Kanuni ya Imani waamini wanasali kwamba "Akapaa mbinguni, amekaa
kuume kwa Baba.
Mwinjili Luka anawaalika waamini kulitafakari fumbo la Kupaa
kwa Bwana mbinguni mintarafu maisha ya Yesu hapa duniani, lakini kwa namna ya pekee,
kwa kupanda kwenda Yerusalemu ili kukabiliana uso kwa uso na Fumbo la Msalaba; yaani:
mateso, kifo na ufufuko wake kama kielelezo cha utii kwa mapenzi ya Baba yake wa mbinguni.
Mwinjili Luka anakazia mambo makuu mawili: kabla ya kurudi ili kushiriki katika
utukufu wa Baba yake wa Mbinguni, Yesu Mfufuka aliwabariki wafuasi wake. Hapa Baba
Mtakatifu Francisko anabainisha kwamba, Yesu anajionesha kuwa ni Kuhani wa milele.
Ni Mungu kweli na mtu kweli, anayeendelea kuwaombea wafuasi wake mbele ya Baba yake
wa mbinguni.
Jambo la pili anasema Baba Mtakatifu ni kwamba, Mwinjili Luka
anasimulia jinsi ambavyo Mitume wa Yesu walivyorudi mjini Yerusalemu wakiwa na furaha
kubwa. Walitambua kwamba, hata kama Yesu Mfufuka alikuwa ametoweka mbele ya macho
yao kimwili, lakini bado anaendelea kuliongoza Kanisa lake, hadi ukamilifu wa dahari.
Baba Mtakatifu anawaalika waamini wanapoendelea kulitafakari Fumbo la Kupaa
kwa Bwana mbinguni, wawe pia ni mashahidi wa furaha ya ufufuko wa Kristo, uwepo wake
endelevu miongoni mwa wafuasi wake na ushindi wa Ufalme viwe ni vielelezo vya utakatifu
na upendo.
Baba Mtakatifu Francisko ametambua uwepo wa Maaskofu kutoka Uingereza,
Mapadre na Majandokasisi kutoka Chuo Kikuu cha Kipapa cha Amerika ya Kaskazini pamoja
na mahujaji kutoka katika nchi zinazozungumza lugha ya Kiingereza.
Amewahakikishia
waamini kwamba, hata katika magumu na mahangaiko yao ya ndani, watambue kwamba, Yesu
Kristo Mfufuka yuko pamoja nao daima katika hija na familia, mahali pa kazi; nyakati
za furaha na majonzi, ili ulimwengu uweze kuonja upendo wa Mungu.
Baba Mtakatifu
Francisko amewapongeza waamini kutoka katika Madhabahu ya Mtakatifu Andrea Bobola
yaliyoko Varsavia, Poland, waliofika mjini Roma ili kumwimbia Mwenyezi Mungu utenzi
wa sifa na shukrani kwa Maadhimisho ya Jubilee ya miaka 75 tangu Mtakatifu msimamizi
wao alipotangazwa kuwa Mtakatifu. Mtakatifu Bobola alikuwa ni Padre Myesuit na Mfia
dini.
Ni Padre aliyejitosa kimaso maso kwa ajili ya imani na upatanisho wa
Kanisa na ndugu katika imani. Maombezi yake mbele ya Mwenyezi Mungu yalisaidie Kanisa
kuwa na umoja na amani.
Baba Mtakatifu pia ametambua uwepo wa Mapadre na Watawa
wanaofanya kumbu kumbu ya Miaka 75 tangu mwanzilishi wao Mtakatifu Giovanni Leonardi
alipotangazwa kuwa Mtakatifu. Anawataka waamini kutoa maisha yao kwa ajili ya huduma
ya Injili.
Amewaombea vijana na wanafunzi waliokuwa wamefurika kwa wingi kwenye
Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro mjini Vatican, ili wawe tayari kujitoa bila
ya kujibakiza kwa ajili ya kumfuasa Kristo; wagonjwa wapokee mahangaiko yao kwa utulivu
na wanandoa wapya waendelee kukua na kukomaa katika utakatifu, wakijitahidi kufuata
mfano wa Familia Takatifu ya Yesu, Maria na Yosefu.