2013-04-16 07:39:10

Jumuiya ya Kimataifa na changamotoza uhuru wa kidini


Uhuru wa kidini ni kati ya changamoto kubwa zinazoikabili Jumuiya ya Kimataifa kwa katika ulimwengu wa utandawazi na maendeleo ya sayansi na teknolojia. Ni mada ambayo itajadiliwa na wadau kutoka sehemu mbali mbali za dunia tarehe 19 Aprili 2013, tukio ambalo limeandaliwa na Kikundi cha Technology Entertainment Design, TED na kudhaminiwa na Baraza la Kipapa la Utamaduni.

Mkutano huu unaotarajiwa kuwa na mvuto mkubwa kwa wadau kutoka ndani na nje ya Italia utafanyika hapa mjini Roma. TED ni kati ya mitandao yenye idadi kubwa ya watu wanaoogelea huko kutafuta habari makini. Inasadikiwa kwamba, walau kila siku, kuna jumla ya watu zaidi ya millioni moja wanaotembelea katika tovuti hii.

Mkutano huu wa aina yake, unatarajiwa kufunguliwa na Kardinali Gianfranco Ravasi, Rais wa Baraza la Kipapa la Utamaduni. Ni mkutano unaowahusisha viongozi kutoka katika medani mbali mbali za maisha, wakiwa na ujuzi, mang’amuzi na mitazamo tofauti kuhusu: uhuru na dini.

Wajumbe watapembua kwa kina na mapana umuhimu wa Jamii kuendelea kujadili kuhusu uhuru wa kidini; tofauti kati ya uhuru na uhuru wa kidini; mchango wa dini katika maendeleo endelevu yanayogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili; uwezo wa mwanadamu kufikiri na kutenda. Wawezeshaji wakuu katika mkutano huu ni wale ambao wamechaguliwa kwa umakini mkubwa baada ya kufanya utafiti uliodumu kwa takribani mwaka mmoja.

Kardinali Gianfranco Ravasi atajadili kwa kina na mapana mchango unaotolewa na Baraza la Kipapa mitarafu majadiliano ya kidini na wale wasioamini, changamoto iliyotolewa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita, aliyelitaka Baraza la Kipapa la Utamaduni kuendesha majadiliano na watu mbali mbali ambao kimsingi hawana imani, lakini wangependa walau kufahamu habari za Mwenyezi Mungu.








All the contents on this site are copyrighted ©.