2013-04-15 15:53:17

Ujumbe kutoka Hispania wakutana na kuzungumza na Baba Mtakatifu Francisko mjini Vatican


Baba Mtakatifu Francisko, Jumatatu, tarehe 15 Aprili 2013 amekutana na kuzungumza na Bwana Mariano Rajoy Brey, Waziri mkuu wa Hispania pamoja na ujumbe wake. Baadaye, waliweza kukutana na kuzungumza pia na viongozi waandamizi kutoka Vatican chini ya uongozi wa Kardinali Tarcisio Bertone, katibu mkuu wa Vatican.

Viongozi hawa kwa pamoja wamejadili kwa kina mapana kuhusu hali ngumu inayowakabili wananchi wa Hispania kwa wakati huu, kama ilivyo pia kwa nchi nyingine za Jumuiya ya Ulaya, hali ambayo imepelekea ukosefu wa fursa za ajira kwa familia na idadi kubwa ya vijana ambao kwa sasa wanakosa matumaini kwa leo na kesho iliyobora zaidi.

Katika kipindi hiki kigumu, Kanisa limeendelea kutoa mchango wa pekee kwa kutumia Mashirika yake ya Misaada kama vile Caritas Hispania na mengineyo ili kuwasaidia watu walioathirika zaidi. Kwa pamoja wameona kwamba, kuna umuhimu wa kuendeleza majadiliano ya Kijamii kwa wahusika wote kwa kuheshimiana, kwa kutoa kipaumbele cha kwanza kwa tunu msingi za maisha ya kijamii na kiutu; haki, amani, upendo, mshikamano na mafao ya wengi.

Viongozi hawa wawili wamepongeza ushirikiano uliopo kati ya Hispania na Vatican, uliofikiwa kunako mwaka 1979, pande hizi mbili zilipowekeana sahihi mkataba wa ushirikiano, ambao umeendelea kudumishwa mwaka hadi mwaka. Wamegusia suala tata la ndoa na familia na umuhimu wa majiundo ya kidini. Taarifa inabainisha kwamba, Baba Mtakatifu pamoja na mgeni wake wamejadili pia masuala ya kimataifa na kwa namna ya pekee hali inavyojionesha Amerika ya Kusini.







All the contents on this site are copyrighted ©.