Majadiliano ya kidini ni muhimu sana katika kudumisha amani duniani
Migogoro, malumbano na kinzani za kidini ni kati ya mambo yanayoendelea kuhatarisha
amani, upendo na mshikamano katika Jumuiya ya Kimataifa. Hii ni migogoro inayofuka
moshi kuanzia katika Jamii za watu na hatimaye, kuwasha moto mkubwa wa kinzani na
migogoro ya kidini kimataifa.
Katika miaka ya hivi karibuni, kinzani kati
ya waamini wa dini ya Kiislam na Kikristo imeendelea kusikika sehemu mbali mbali za
dunia, kila upande ukidai kunyanyasika! Lakini ukweli wa mambo ni kwamba, kuna baadhi
ya watu wanaopenda kutumia migogoro na kinzani za kidini kwa ajili ya mafao yao binafsi,
hali ambayo inaleta maafa makubwa kwa Jamii husika.
Padre Makari Habibi, katibu
muhtasi wa Papa Tawadros wa Pili, Patriaki wa Kanisa la Kiorthodox la Kikoptic nchini
Misri anasema, kuna haja kwa Serikali ya Misri kuhakikisha kwamba, inalinda na kuheshimu
uhuru wa kidini kama nguzo msingi ya kulinda na kudumisha misingi ya haki, amani na
utulivu miongoni mwa Jamii. Hii inatokana na ukweli kwamba, asilimia kubwa ya wananchi
wa Misri ni waamini wa dini ya Kiislam na waamini wa dini nyingine ni asilimia kidogo.
Mashambulizi dhidi ya waamini wa dini nyingine kwa kisingizio cha imani kali
ni jambo ambalo kamwe haliwezi kuvumiliwa na wapenda amani duniani. Sheria inapaswa
kuchukua mkondo wake kwa watu wanaovunja sheria za nchi kwa kufanya vitendo vya jinai
vinavyohatarisha usalama wa maisha na mali za wananchi. Vyombo vya ulinzi na usalama
viwe makini kuhakikisha amani na utulivu vinadumishwa ili kila mwananchi aweze kutekeleza
wajibu wake kikatiba, kwani hii ndiyo Sheria Mama inayolinda uhuru wa kila mtu.
Viongozi
wa dini wapewe fursa ya kufundisha dini shuleni. Padre Makari Habibi anasema, umefika
wakati kwa Serikali ya Misri kutoa nafasi kwa Kanisa la Kiorthodox la Kikoptik Misri
kuanza kufundisha dini shuleni kama sehemu ya mchakato wa majadiliano ya kidini miongoni
mwa wanafunzi. Ni jambo ambalo haliwezi kukubalika kwa Kanisa la Kikoptik kuendelea
kuwekwa pembezoni mwa Jamii ya wananchi wa Misri.
Kinzani na migogoro ya kidini
ni kielelezo cha ukosefu wa utawala bora unaozingatia sheria na maadili ya uongozi,
kwani kuna baadhi ya viongozi wanaendeleza chuki na uhasama wa kidini kwa ajili ya
mafao yao ya kisiasa. Watu wanaopandikiza mbegu za chuki na uhasama wanapaswa kushughulikiwa
na vyombo vya sheria mapema kabisa na wala wasingojee hadi mambo yanapoharibika na
hivyo kuanza kurushiana mpira wa uwajibikaji.
Waamini wa Kanisa la Kikoptik
nchini Misri, wanapaswa pia kupata uwakilishi katika taasisi zinazoendeshwa na kusimamiwa
na Serikali na kamwe wasitengewe kana kwamba, wao si wananchi wa Misri wenye haki
na wajibu wa kutekeleza. Mchakato wa kutafuta wawakilishi katika Bunge la Misri
unatarajiwa kuanza hapo tarehe 22 Aprili na kuhitimishwa mwezi Juni 2013. Hadi sasa
kuna uwakilishi mdogo sana wa waamini wa Kanisa la Kikoptik nchini Misri kadiri ya
taarifa zilizotolewa na Shirika la Habari za Kimissionari, FIDES.