2013-04-15 10:56:45

Askofu mkuu Lebulu asema, amani inasimikwa katika ukweli, uhuru, upendo na msamaha!


Amani ni zawadi kutoka kwa Mwenyezi Mungu inayomwajibisha binadamu katika maisha na vipaumbele vyake. Kanisa linapoadhimisha Kumbu kumbu ya Jubilee ya miaka 50 tangu Baba Mtakatifu Yohane wa XXIII alipochapisha Waraka wa kichungaji, Pacem In Terris, Amani Duniani linakumbusha kwamba: Waraka huu ulibainisha haki na wajibu wa kila mtu katika kulinda na kutetea haki na amani duniani, kwa kusoma alama za nyakati. RealAudioMP3

Askofu mkuu Josephat Lebulu wa Jimbo kuu la Arusha Tanzania katika mahojiano maalum na Radio Vatican kuhusu kumbu kumbu ya Jubilee ya Miaka 50 ya Waraka wa Kichungaji wa Amani Duniani anasema, angependa kukazia mambo makuu manne: Ukweli, uhuru, upendo na msamaha dhana iliyokaziwa kwa namna ya pekee na Baba Mtakatifu Yohane Paulo wa pili, hakuna amani pasi na msamaha. Amani ya kweli inaonesha uhusino wa dhati kati ya mwanadamu na Muumba wake, Mazingira na watu wanaomzunguka.

Kuna uhusiano kati ya amani na uchumi, siasa na maendeleo endelevu yanyogusa mahitaji ya mtu mzima: kiroho na kimwili. Mambo yote haya yakiwekwa pamoja yanakuwa ni viashilia vya amani katika Jamii husika. Kwa vile binadamu wanakosa na kukosehana, kumbe, hawana budi kujenga utamaduni wa kusameheana ili kujenga na kuimarisha misingi ya haki na amani.

Askofu mkuu Lebulu anasema, katika kipindi cha miaka 50 iliyopita, amani imeendelea kukumbana na vitisho vingi. Hii ni amani inagusa maisha na utume wa Kanisa pamoja na Jamii kwa ujumla wake. Sababu msingi za kukosa amani ni: ubinafsi, uchu wa mali na madaraka; malumbano na kinzani za kidini na kwamba, upendo na ukweli ni tunu ambazo zimepungua kwa kiasi kikubwa katika Jamii nyingi, kiasi kwamba, watu wanaona hata hsida ya kusameheana. Lakini Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili anasema, kusamehe ni changamoto kwa watu wanaoishi katika ulimwengu wa utandawazi.

Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita katika Waraka wake wa Mlango wa Imani anasema imani haina budi kujikita katika mapendo, kwani amani ya kweli inategemea kwa namna ya pekee imani ya Jamii husika. Askofu mkuu Lebulu anasema kwamba, tunu hizi msingi katika maisha ya mwanadamu zinaendelea kupungua siku hadi siku.

Kanisa linapaswa kuwa ni ishala ya amani na sehemu ya mchakato wa mapambano dhidi ya umaskini wa kipato, hali na maisha ya kiroho. Kanisa lisaidie kumletea mwanadamu maendeleo endelevu, kila mtu atekeleze wajibu wake katika maboresho ya maisha ya mwanadamu ili: haki, amani, upendo na mshikamano wa kweli viweze kutawala duniani.







All the contents on this site are copyrighted ©.