2013-04-13 08:11:57

Mwezi mmoja tangu Papa Francisko achaguliwe kuliongoza Kanisa Katoliki!


Baada ya waamini na watu wote wenye mapenzi mema kusali na kufunga kwa ajili ya kuwasindikiza Makardinali waliokuwa kwenye mchakato wa uchaguzi wa Papa Mpya, hatimaye, tarehe 13 Machi 2013 usiku, moshi mweupe ukaonekana; uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro ukafurika kwa umati wa watu kutoka sehemu mbali mbali za dunia, lakini bado kilibakia kitendawili ni nani aliyechaguliwa?

Kardinali Polycarp Pengo, Rais wa Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki Afrika na Madagascar katika mahojiano na Radio Vatican aliwataka watu kutomwekea kizingiti Roho Mtakatifu na kwamba, uchaguzi wa Papa lilikuwa ni tukio la Kikanisa.

Hatimaye, jina likatangazwa na watu wakamwona Papa Francisko, akitabasamu na kuwapungia mkono, akiwa amevaa Msalaba wake wa siku zote kama Kardinali kutoka Buenos Aires. Baada ya kuzungumza maneno machache ya shukrani, aliinamisha kichwa kuomba sala kutoka kwa waamini na watu wenye mapenzi mema waliokuwa wamefurika kwenye Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro, kwa kitambo kidogo, ukimya ukatawala na watu wakasali kwa ajili yake.

Siku iliyofuatia, Baba Mtakatifu Francisko asubuhi na mapema aliondoka kwenda kutoa heshima zake kwa Bikira Maria Mama wa Mungu na Kanisa kwenye Kanisa kuu la Bikira Maria mkuu, lililoko mjini Roma pamoja na kulipa deni la pango kwa kipindi chote alichokuwa amekaa kwenye nyumba ya Makleri, Roma.

Jioni, Baba Mtakatifu Francisko akaadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya Kanisa akishirikiana na Makardinali wote walioshiriki katika mchakato wa uchaguzi wa Papa mpya kwenye Kikanisa cha Sistina, kilichoko hapa mjini Vatican. Katika mahubiri yake alikazia mambo makuu: kutembea kwa pamoja, wakijitahidi kujenga Kanisa la Kristo kwa njia ya ushuhuda unaokumbatia Fumbo la Msalaba, kama kielelezo cha Wafuasi wa Kristo.

Tarehe 15 Machi 2013, Baba Mtakatifu akakutana na kuzungumza na Makardinali walioshiriki kwenye Conclave, akawashukuru wote na kupata nafasi ya kuzungumza na kila mmoja wao. Aliwataka Makardinali kusimama kidete na kamwe wasikatishwe tamaa na ukakasi pamoja na magumu ya maisha bali waendelee kumtumainia Roho Mtakatifu anaendelea kulitegemeza Kanisa. Aliwataka kuwa na ujasiri wa kubainisha mbinu mpya za Uinjilishaji, ili Kristo aweze kufahamika, kuabudiwa, kupendwa na kutumikiwa.

Tarehe 16 Machi 2013, Baba Mtakatifu alipata fursa ya pekee kukutana na hatimaye kuzungumza na umati mkubwa wa waandishi wa habari kutoka sehemu mbali mbali za dunia, waliokuwa wamefurika hapa mjini Vatican kufuatilia hatua kwa hatua mchakato wa uchaguzi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro. Akawaambia kwamba, amepewa changamoto ya pekee ya kutowasahau maskini, akaona Jina Francisko wa Assisi lilikuwa linaendana kabisa na utume wake mpya kama Khalifa wa Mtakatifu Petro: changamoto ya kutoa kipaumbele cha kwanza kwa maskini; amani pamoja na utunzaji bora wa mazingira.

Nembo ya utume wa Baba Mtakatifu Francisko inasomeka kwa maneno ya Kilatini "Miserando atque eligendo" "akamtazama kwa jicho la huruma, akamchagua" Ni maneno ya Mtakatifu Beda katika mahubiri yake juu ya wito wa Mathayo mtoza ushuru. Baba Mtakatifu ameendelea kukazia kuhuu huruma na upendo wa Mungu usiokuwa na mipaka kwa waja wake. Mungu ni mwingi wa huruma, kamwe hachoki kusamehe, changamoto kwa waamini kujifunza utamaduni wa kusamehe na kuwa na huruma.

Tarehe 19 Machi 2013 Baba Mtakatifu Francisko aliadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kama mwanzo wa utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, Ibada ambayo ilikuwa na uwakilishi mkubwa wa viongozi wa dini, madhehebu na wale wa Serikali bila kuwasahau wawakilishi wa maskini kutoka Buenos Aires. Akawataka waamini na Viongozi wa Kimataifa kuwa ni watunzaji bora wa jirani zao na mazingira na kwamba, madaraka ni kwa ajili ya huduma kwa wanyonge. Kama Papa anatamani kuwa ni daraja linalounganisha watu mbali mbali sanjari na kulinda, kutetea na kudumisha misingi ya haki, amani na majadiliano.

Mkazo huu ulijionesha pia wakati Baba Mtakatifu alipokutana na kuzungumza na Wanadiplomasia na wawakilishi wa nchi na mashirika ya kimataifa hapa mjini Vatican.

Tarehe 23 Machi 2013 Baba Mtakatifu Francisko kwa mara ya kwanza akakutana na Papa mstaafu Benedikto wa kumi na sita, tukio ambalo litakumbukwa daima katika historia ya Kanisa Katoliki; ndugu wawili katika huduma kwa Kristo na Kanisa lake wakakumbatiana, wakasali, wakazungumza na kula kwa pamoja. Jumapili ya Matawi, Uwanja wa Kanisa kuu la Mtakatifu Petro ukafurika na umati wa vijana kutoka sehemu mbali mbali za dunia, akawaambia, kamwe wasikubali kupokonywa matumaini yanayobubujika kutoka kwa Kristo!

Alhamisi kuu, Baba Mtakatifu akaadhimisha Ibada ya Misa Takatifu kwa ajili ya kubariki Mafuta Matakatifu, akawataka Makleri wa Roma kutoka katika ubinafsi na undani wao, ili kwaendea wale walioko pembezoni mwa Jamii: kiroho na kimwili; huko ndiko kuna watu wengi wanaoteseka zaidi. Kwa njia hii, waamini wataweza kuwatambua na kumtambua Kristo kati yao! Alhamisi kuu jioni, akaadhimisha Misa Takatifu; kumbu kumbu ya Siku ile Yesu alipoweka Sakramenti Takatifu ya Daraja na Ekaristi Takatifu; sakramenti zinazomwilishwa katika huduma ya upendo. Papa Francisko, akawaosha miguu watoto wa gereza la watoto watukutu la Casal del Marmo lililoko mjini Roma.

Ijumaa kuu, katika Maadhimisho ya Njia ya Msalaba kuzunguka Magofu ya Colosseo mjini Roma, Baba Mtakatifu akawakumbusha waamini kwamba, Msalaba wa Yesu ni jibu la wema wa Mungu dhidi ya ubaya. Hii ni chemchemi ya matumaini ya Kikristo yanayotangaza upendo wa Mungu kwa njia ya Ufufuko wa Kristo aliyeshinda dhambi na mauti, ndivyo alivyowakumbusha waamini katika Kesha la Pasaka.

Akitoa baraka na ujumbe wake kwa mji wa Roma na Dunia kwa ujumla "Urbi et Orbi", akawaalika waamini kutoa nafasi kwa Yesu Kristo ili aweze kuwaletea mabadiliko ya ndani, ili waweze kuwa ni vyombo vya huruma ya Mungu, ili haki, amani upendo na mshikamano viweze kutawala dunia.

Katika Ibada za Misa Takatifu na waamini mbali mbali kwenye Kikanisa cha Domus Sanctae Martha amekazia kwa namna ya pekee: majadiliano ya kiekumene; kipaumbele kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii; changamoto ya Uinjilishaji mpya kwa njia ya ushuhuda wa maisha na kwamba, waamini walei wanachangamotishwa kuyatakatifuza malimwengu, daima wakijitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya huduma kwa Injili ya Kristo.

Baba Mtakatifu anawaalika waamini kutoogopa bali wamfungulie Kristo malango ya mioyo na maisha yao; wakitoka kifua mbele kumtangaza Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka katika wafu. Akiwa kwenye Kanisa kuu la Mtakatifu Yohane wa Laterano, Baba Mtakatifu anawaalika waamini kushikamana Askofu wao ili kuwashirikisha wengine ile furaha ya Kristo Mfufuka, kwani daima yuko pamoja nao katika hija ya maisha yao ya kila siku.

Kwa ufupi, Baba Mtakatifu Francisko ni mtu wa maneno machache, lakini matendo yake yanazungumza zaidi hata ya kile ambacho tumejaribu kuweka kwa muhtasari, Kanisa linapofanya kumbu kumbu ya Mwezi mmoja, tangu Baba Mtakatifu Francisko alipochaguliwa kuliongoza Kanisa Katoliki kama Khalifa wa Mtakatifu Petro.

Imehaririwa na Padre Richard Mjigwa, C.PP.S
Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.







All the contents on this site are copyrighted ©.