2013-04-13 11:14:56

Chuo kikuu kinapaswa kuwa ni mahali pa matumaini kwa vijana wa kizazi kipya


Kardinali Tarcisio Bertone katibu mkuu wa Vatican katika maadhimisho ya Siku ya Chuo Kikuu cha Kikatoliki cha Moyo Mtakatifu wa Yesu, Jumapili, tarehe 14 Aprili 2013, amewasilishana salam na matashi mema kutoka kwa Baba Mtakatifu Francisko anayewataka wadau mbali mbali kuendeleza ari na moyo uliopelekea hata Padre Agostino Gemelli, akaanzisha Chuo hiki, ambacho kina umaarufu wa pekee nchini Italia kutokana na rejea yake kwa majiundo makini kwa vijana wa kizazi kipya katika medani mbali mbali za maisha.

Maadhimisho haya yanayofanyika kila mwaka, yawe ni kielelezo anasema Kardinali Bertone cha: umoja na mshikamano na wadau mbali mbali pamoja na vitivo vilivyoko chini ya Chuo Kikuu cha Moyo Mtakatifu wa Yesu; daima wakiendelea kuwa waaminifu kwa malengo na utambulisho wa Chuo Kikuu cha Kikatoliki katika kuwaandaa vijana ili kukabiliana na changamoto mbali mbali za maisha kwa njia ya majiundo makini, tafiti, semina na machapisho yanayotolewa Chuoni hapo. Msukumo wa pekee ni kuwa karibu na vijana hasa wakati huu wanapokabiliana na athari za myumbo wa uchumi kimataifa.

Kardinali Bertone anakumbusha kwamba, mtikisiko huu umewagusa vijana wengi kiasi kwamba, wale wanaojiunga na vyuo vikuu nchini Italia wamepungua kwa kiasi na wengi wanaohitimu masomo yao hawana uhakika wa kupata fursa za ajira. Zote hizi ni changamoto zinazopaswa kufanyiwa kazi kwa kina na mapana ili kupatiwa ufumbuzi wake kwa ajili ya ustawi na maendeleo ya Italia na watu wake. Kuna haja ya kuendeleza mshikamano na Kanisa pamoja na vyama vya kitume katika utekelezaji wa majukumu yake.

Kanisa limejitahidi kutoa kipaumbele cha pekee katika maisha na utume wa vijana, likiwataka kukabiliana na changamoto za maisha yao katika misingi ya imani, kwa kushiriki kikamilifu katika maisha na utume wa Kanisa pamoja na kujizatiti katika masomo kwani hili ndilo jambo la kwanza linalopaswa kupewa msukumo wa pekee.

Kardinali Bertone, anasema, Baba Mtakatifu Francisko anawaalika vijana kuwa na ari na matumaini mapya na kwamba, Chuo kikuu ni mahali ambapo vijana wanatua nanga ya matumaini yao kwa ustawi na maendeleo ya leo na kesho iliyo bora zaidi. Utu na heshima ya binadamu, mafao ya wengi; uwiano mzuri kati ya imani na uwezo wa mwanadamu wa kufikiri na kutenda ni kati ya mambo yanayopaswa kupewa kipaumbele cha kwanza, pamoja na kuzingatia maadili katika tafiti kama sehemu ya majiundo makini ya vijana wa kizazi kipya.







All the contents on this site are copyrighted ©.