2013-04-13 10:28:27

Balozi Mpya wa Vatican apokelewa kwa shangwe nchini Kenya


Askofu mkuu Charles Daniel Balvo, Balozi wa Vatican nchini Kenya, Ijumaa asubuhi aliwasili rasmi nchini Kenya kuanza utume wake kama Balozi wa Vatican kwa kusema kwamba, anayo furaha kubwa kutekeleza utume na dhamana yake miongoni mwa Familia ya Mungu Barani Afrika na kwa namna ya pekee, nchini Kenya.

Anasema kabla ya kuondoka mjini vatican alipata nafasi ya kukutana na kusalimiana na Baba Mtakatifu Francisko. Waamini na watu wenye mapenzi mema sehemu mbali mbali za dunia wamempokea kwa mikono miwili Baba Mtakatifu Francisko na wengi wanaonesha kuguswa na maisha na unyenyekevu wake.

Baba Mtakatifu amekuwa akiadhimisha Ibada za Misa Takatifu pamoja na kutembelea makundi mbali mbali ya watu kama njia ya ujenzi wa Jumuiya inayoinjilisha kwa njia ya ushuhuda wa maisha halisi. Baba Mtakatifu amemtia moyo kwa utume wake mpya nchini Kenya.

Kardinali John Njue, Rais wa Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya ni kati ya viongozi wakuu wa Kanisa waliofika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Jomo Kenyatta kumpokea Askofu mkuu Charles daniel Balvo, aliyeteuliwa na Baba Mtakatifu mstaafu Benedikto wa kumi na sita mapema mwezi Januari kuwa Balozi Mpya wa Vatican nchini Kenya.

Kardinali Njue anasema, Balozi wa Vatican amewasili wakati muafaka kwani Baraza la Maaskofu Katoliki Kenya linaanza mkutano wake wa Mwaka. Ni matumaini yake kwamba, Askofu mkuu Balvo ataweza kupata nafasi ya kukutana na kuzungumza na Maaskofu Katoliki wa kenya wakati wa mkutano wao. Kanisa nchini Kenya linamkaribisha Balozi wa Vatican kwa mikono miwili ili kujenga na kudumisha umoja, udugu na mshikamano wa Kikristo.







All the contents on this site are copyrighted ©.