2013-04-12 07:23:57

Tafakari ya Neno la Mungu, Jumapili ya tatu ya Kipindi cha Pasaka


Mpendwa mwana wa Mungu tunaendelea katika furaha ya Pasaka, furaha kwa ajili ya kukombolewa toka katika utumwa wa shetani. Tayari tuko Dominika ya tatu ya Kipindi cha Pasaka, na ujumbe wa Neno la Mungu kwa kifupi unatuambia kuwa, Neno la Kristo mfufuka linaongoza Jumuiya ya Kikristo. RealAudioMP3

Mpendwa tunaona katika Somo la kwanza kuwa Jumuiya ya kwanza ya Kikristo ilikabiliana na upinzani mkubwa lakini wakitii Neno la Mungu wanasima kidete na wanabaki imara pamoja na mateso watakayoteseka. Tunamwona Mtakatifu Petro kiongozi mkuu wa Jumuiya akisema, yatupasa kumtii Mungu kuliko binadamu. Kama ambavyo Kristo mbele ya Wayahudi alionekana mkorofi, ndivyo ambavyo Mitume wanaonekana mbele ya Jumuiya hiyo. Pengine hata leo Wakristo tunaonekana hivyo mbele ya watu tunapodai haki na kutii ukweli wa Mungu.

Lakini, Je, ukweli ndo huo wa kuonekana wakorofi? Hapana, Mitume hawakuwa katika mlengo wa ukorofi bali katika kupambana na uovu kinyume na haki, kinyume na Injili ya wokovu, Injili ya ukweli. Kwa kuwa Bwana alimtii Baba yake na akaweza kwa njia ya utii huo kutupatia wokovu, vivyo na Mitume wakafuata nyayo zake, nasi yatupasa bila kurudi nyuma kuitikia mwaliko wa Mungu unaotujia kila siku kwa njia ya Neno lake.

Katika kutii lazima tutambue mambo muhimu ya kufanya, jambo la kwanza ni kwamba Yesu Kristo ndiye aliyechinjwa sadaka na yuko katika kiti cha enzi na kwa namna hiyo anao uwezo wote wa kujibu maswali na hoja zote zitokazo katka moyo wa mwanadamu. Yeye ni Mwanga wa kujua matukio yanayotukia katika historia. Jambo hili liliwaongoza Mitume na Jumuiya ya kwanza katika kukabiliana na upinzani katika utume wao wa kuendeleza kazi ya Bwana. Kwa kujua hilo waliweza kusema yatupasa kumtumikia Mungu na si shetani wala mwanadamu.

Katika Injili Bwana anawatokea mara ya tatu Mitume na bado hawamtambui! Hiki ni kichekesho. Katika Injili ya Luka 5: 1-11 alishawaambia kuwa mtakuwa wavuvi wa watu, inashangaza bado wako katika uvuvi! Kwa nini wanarudia kazi yao ya zamani? Laonesha hali ya mwandamu ya kutaka kurudi katika dhambi! Baada ya ufufuko alishawatokea mara ya kwanza na mara ya pili na bado hawajaweza kumtambua, ni kweli utambuzi wa Bwana unadai hatua kwa hatua na hivi watafikia kilele cha utambuzi wa Bwana baadaye.

Mpendwa, jambo hili si la ajabu kwetu, kwa maana nasi kila Dominika katika Misa Yesu yu pamoja nasi lakini bado wakati fulani anapotokea tunajikuta katika hali ya kutomtambua. Hata hivyo mwaliko kwetu unakujia kwa njia ya Neno lake ni kwamba lazima tuongozwe na Neno hilohilo ili kufikia ukamilifu wa ukweli.

Mpendwa msikilizaji, tunapoongozwa na Neno la Kristo mfufuka yatupasa kufikiri na kutafakari sana ili daima tupige hatua mbele badala ya kurudi nyuma. Katika Injili ya leo zipo alama ambazo Bwana anazitumia ili tupate kuelewa vema maongozi yake. Tunaona katika chombo yaani mtumbwi kuna watu saba, na namba saba katika Biblia ni namba huwakilisha ukamilifu, kumbe Mitume wanawakilisha wafuasi wa Kristo ambao wanapaswa wapambane na nguvu za giza katika umoja na ukamilifu wao.

Nguvu za giza ambazo wanapaswa kupambana nazo zinaoneshwa kwa alama ya bahari. Na kwa namna hiyo kuwavua watu kama Bwana anavyosema ni kuwatoa katika nguvu za giza, ili waingie katika nguvu ya upendo. Hiyo ndiyo Pasaka yaani kumfuata Bwana ambaye yuko juu ya ardhi akiwaalika watu wamfuate. Mitume walivua samaki na kukosa, hili latuonesha hali ya kujitenga na Mungu haitupatii neema na zawadi mbalimbali za Kimungu bali kubaki katika baa la njaa yaani ukosefu wa neema zake, na kinyume chake ni kukaa na Mungu.

Mpendwa mwana wa Mungu, wanapomsikiliza Bwana na kusadiki wanapata samaki wengi na namba ya samaki waliowapata yaani 153 yatuonesha ukamilifu wa Jumuiya, na hivi kazi ya Jumuiya ya Kikristo ni kuvua watu wote pasipo kumbakiza hata mmoja na kwa namna hiyo kuwapeleka kwa Bwana.

Tunaendelea kuona alama nyingine ambazo ni za maana katika kuelewa na kulifuata Neno la Mungu. Bwana yuko nchi kavu na ametayarisha samaki na mkate, hii ni alama yakwamba mwisho wa safari Kristu amewatayarishia watoto wake chakula cha uzima, furaha ya mbinguni, furaha ya milele. Mitume saba waliokuwa katika chombo wanaleta samaki kwa Bwana, yaani ndivyo kila mmoja wetu atakavyodaiwa kuwasilisha kwa Mungu matunda ya kazi yake ya kitume hapa duniani. Mkate utaletwa na Bwana na si Mitume kumbe yeye ndiye Ekaristi Takatifu, ndiye atupatiaye Komunio ya uzima, chakula cha Mkristo akisafiri kwenda mbinguni.

Neno la Mungu ni zawadi na taa ya maisha yetu, hutupa mwongiozo na kwa njia yake tunapata mwongozo jinsi ya kusimamia taifa lake. Akitaka kumkabidhi Mt. Petro mamlaka ya juu katika Kanisa atamwita na kumwuliza mara tatu, alama ya ukamilifu, akisema Je Petro wanipenda? Na jibu la Mt. Petro ni jibu la upole na unyenyekevu ndiyo Bwana wewe wajua kuwa nakupenda.

Na kisha jibu hilo Bwana anamwambia lisha kondoo wangu! Bwana alimwuliza Bwana mara tatu akitaka kuthibitisha imani ya Mtume Petro na uongofu mkamilifu maana kabla ya mateso ya Bwana alimkana mara tatu! Anataka na kudai upendo usi ona sheria, upendo unaozidi yaani kujitoa pasipo kulazimishwa kwa ajili ya wengine. Katika wajibu huo wa Mt. Petro huko mbele umejaa mateso na kufungwa hata kufa msalabani kwa ajili ya Bwana na kondoo wake. Sisi tukiongozwa na Neno la Mungu wito wetu ni kuchunga familia ya watu wa Mungu.

Mpendwa msikilizaji nikutakie furaha ya Pasaka endelevu, ukiliweka Neno la Mungu mbele yako daima na hivi ukichunga kondoo uliokabidhiwa, ukijua kuwa kuna mateso katika maisha ya kumfusa Bwana kwa upendo mkamilifu, lakini tumaini likiwa katika Bwana na ukakika ni kwa nia ya Injili yake.

Tumsifu Yesu Kristo.

Tafakari hii imeletwa kwako na Pd. Richard Tiganya C.PP.S.








All the contents on this site are copyrighted ©.