Maandiko Matakatifu na Mapokeo ya Kanisa yameshikamana na kushirikiana kwani yote
mawili yanabubujika kutoka katika chemchemi ya Kimungu
Uvuvio wa Roho Mtakatifu na ukweli katika Maandiko Matakatifu ni mada nyeti inayogusa
undani wa maisha ya Kanisa zima kwani utume na maisha yake yote yanafumbatwa katika
Neno la Mungu ambalo ni dira ya taalimungu na uwepo wa Kikristo. Maandiko Matakatifu
ni ushuhuda wa Neno la Mungu uliowekwa katika maandishi na kuwa ni sehemu ya kumbu
kumbu ya Kanuni ya tukio la Ufunuo.
Kwanza kabisa Neno la Mungu linatangulia
na baadaye unafuatia ushuhuda ambao ni Biblia. Imani ya Kanisa inafumbatwa si tu katika
Biblia bali katika Historia ya Wokovu inayojikita katika Nafsi ya Yesu Kristo, Neno
wa Mungu aliyefanyika mwili pamoja na kutambua kazi ya Roho Mtakatifu anayeliongoza
Kanisa ili liweze kufahamu ukweli wote.
Ni maneno ya Baba Mtakatifu Francisko
wakati alipokutana na kuzungumza na Wajumbe wa Tume ya Kipapa ya Biblia waliokuwa
wanafanya mkutano wao wa Mwaka, wakiongozwa na mada "Uvuvio wa Roho Mtakatifu na Ukweli
wa Biblia". Baba Mtakatifu amewashukuru wajumbe hawa kwa kazi kubwa waliyoifanya wakati
wote huu.
Anasema, kuna haja ya kuwa na ufahamu mpana zaidi wa Mapokeo hai
ya Kanisa ambayo kwa njia ya Roho Mtakatifu na Mamlaka rasmi ya ufundishaji katika
Kanisa; Mama Kanisa ametambua na kutamka wazi kwamba, Vitabu vya Kanuni ni Neno la
Mungu linalotangazwa kwa Watu wake; kamwe hajaacha kulitafakari na kuendelea kugundua
utajiri wake. Mtaguso mkuu wa Pili wa Vatican katika hati yake ya kichungaji Neno
la Mungu, "Dei Verbum" unabainisha kwamba, "Kwa kweli hayo yote yanayohusu jinsi ya
kufasiri Maandiko Matakatifu yapo chini ya uamuzi wa Mama Kanisa ambaye hutimiza amri
ya Mungu na huduma yake ya kuhifadhi na kulifahamu Neno la Mungu." DV. 2.
Baba
Mtakatifu Francisko anaendelea kusema kwamba, "Kwa hiyo Mapokeo Matakatifu na Maandiko
Matakatifu yameshikamana pamoja na kushirikiana. Kwa sababu yote mawili yanabubujika
kutoka katika chemchemi ileile ya Kimungu na hivyo huungama na kuwa ni kitu kimoja
na kuelekea lengo moja. Kwa kweli, Maandiko Matakatifu ndilo Neno la Mungu ambalo
liliandikwa kwa uvuvio wa Roho wa Mungu. Neno la Mungu lililokabidhiwa kwa Mitume
wa Kristo Bwana na Roho Mtakatifu linarithishwa li zima na Mapokeo Matakatifu kwa
waandamizi wao, ili wakiangazwa na Roho wa ukweli, kwa njia ya kuhubiri kwao, walihifadhi
kiaminifu, walifafanue na kulieneza. Hivyo Kanisa halichoti uhakika wake juu ya mambo
yote yaliyofunuliwa kutokana na Maandiko Matakatifu peke yake. Kwa hiyo Maandiko Matakatifu
na Mapokeo matakatifu lazima yapokelewe na kuheshimiwa kwa hisia sawa, za uchaji na
heshima." DV. 9.
Baba Mtakatifu anaendelea kusema kwamba, wachambuzi wa Neno
la Mungu hawana budi kuwa makini kwa kuhakikisha kwamba, wanaliweka katika imani ya
Kanisa. Tafsiri ya Maandiko Matakatifu si juhudi za kisayansi za mtu binafsi, bali
zinapaswa kuendana na ukweli wa Mapokeo hai ya Kanisa. Maandiko Matakatifu yamekabidhiwa
kwa Jumuiya ya Waamini na kwa Kanisa la Kristo ili kurutubisha imani na kutoa dira
ya maisha ya upendo. Kumbe kuna haja ya kuheshimu na kuthamini Maandiko Matakatifu
pamoja na Mapokeo Matakatifu katika Familia ya Mungu.
Baba Mtakatifu amehitimisha
hotuba yake kwa wajumbe wa Tume ya Kipapa ya Biblia kwa kuwashukuru na kuwapongeza
kwa juhudi na kazi kubwa na yenye thamani waliyoitenda. Yesu Kristo Neno wa Mungu
aliyefanyika Mwili, akafungua mioyo na akili za wafuasi wake ili waweze kuyafahamu
Maandiko Matakatifu, awaongoze daima katika utume wao.
Bikira Maria, kielelezo
cha unyenyekevu na utii kwa Neno la Mungu, awafundishe kupokea katika utimilifu wake
utajiri mkubwa unaofumbatwa katika Maandiko Matakatifu, dhamana inayopaswa kutekelezwa
si tu katika tafiti, bali katika sala na maisha yao yote kama waamini, hasa wakati
huu, Mama Kanisa anapoendelea kuadhimisha Mwaka wa Imani, ili kwamba, utume wao usaidie
mwanga wa Maandiko Matakatifu kung'ara mioyoni mwa waamini.