2013-04-11 15:09:38

Miaka 50 ya Waraka wa Amani Duniani iwe ni changamoto ya kujitoa bila ya kujibakiza kukuza na kudumisha upatanisho na amani


Baba Mtakatifu Francisko, Siku ya Alhamisi, tarehe 11 Aprili 2013 amekutana na kuzungumza na wajumbe wa Mfuko wa Papa unaogharimia shughuli mbali mbali za kichungaji kadiri ya matakwa na utashi wa Khalifa wa Mtakatifu Petro. Kwa namna ya pekee, Baba Mtakatifu amewshukuru wajumbe kwa sala na matashi mema waliyomwonesha tangu alipochaguliwa kuliongoza Kanisa.

Anatambua mchango mkubwa wa Mfuko huu katika kusaidia kusukuma mbele utume wa Khalifa wa Mtakatifu Petro. Anawashukuru kwa namna ya pekee kwa kuchangia maendeleo na ustawi wa Makanisa katika nchi za Kimissionari; kwa kusaidia majiundo makini na endelevu kwa Makleri na Watawa bila kusahau msaada ambao wamekuwa wakitoa kwa ajili ya ujenzi wa makazi na huduma kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.

Mfuko wa Papa umechangia maboresho ya huduma ya elimu sanjari na kutoa fursa za ajira kwa watu wengi sehemu mbali mbali za dunia. Mahitaji ya Familia ya Mungu yanazidi kuongezeka maradufu na kwamba, wao wamekuwa mstari wa mbele katika kuchangia jitihada za Mama Kanisa katika mapambano dhidi ya umaskini wa hali na maisha ya kiroho unaomwandama mwanadamu katika ulimwengu mamboleo pamoja na kuchangia ukuaji wa mshikamano wa upendo na amani.

Baba Mtakatifu Francisko anaomba kwamba, Kumbu kumbu ya Maadhimisho ya Jubilee ya Miaka 50 ya Waraka wa Kichungaji, Pacem In Terris, Amani Duniani, iwe ni changamoto ya kujitoa bila ya kujibakiza kwa ajili ya kukuza na kudumisha upatanisho na amani katika ngazi mbali mbali za maisha ya mwanadamu.

Anawatakia kheri, baraka na huruma ya Mungu, wakati huu Mama Kanisa anapoendelea kuadhimisha Kipindi cha Pasaka, ili kiweze kuwa ni chemchemi ya furaha inayobubujika ndani mwao kwa kutambua zawadi nyingi ambazo wamekirimiwa na Mwenyezi Mungu katika hija ya maisha yao; daima wakitamani kuendelea kuwahudumia jirani zao wanaoogelea katika shida na mahangaiko mbali mbali.

Baba Mtakatifu Francisko anahitimisha hotuba yake kwa kuwakumbusha wanachama wa Mfuko wa Papa kwamba, wao wanachangia kwa namna ya pekee mshikamano wa kiroho na Khalifa wa Mtakatifu Petro. Anawaomba kuendelea kusali kwa ajili ya utumishi wake ndani ya Kanisa, lakini zaidi, waendelee kuombea toba na wongofu wa ndani, ili uzuri na ukweli wa Kiinjili uweze kupenya akili na mioyo ya watu. Amewaweka wanachama wa Mfuko wa Papa chini ya ulinzi na maombezi ya Bikira Maria Mama wa Kanisa pamoja na kuwapatia baraka zake za kitume.








All the contents on this site are copyrighted ©.