Mateso, kifo na ufufuko wa Yesu Kristo ni kiini cha Imani ya Kanisa
Siku ya tatu alifufuka kutoka katika wafu, ni sehemu ya Kanuni ya Imani ambayo Baba
Mtakatifu Francsiko ametafakari pamoja na waamini, mahujaji na wageni waliofika mjini
Vatican siku ya jumatano, tarehe 10 Aprili 2013 ili kusikiliza Katekesi yake kama
sehemu ya mwendelezo wa Katekesi za Maadhimisho ya Mwaka wa Imani. Baba Mtakatifu
anawaalika waamini kujitaabisha kufahamu kwa kina maana ya ufufuko katika maisha na
kwa ajili ya wokovu.
Mateso, kifo na ufufuko wa Yesu anasema Baba Mtakatifu
ni kiini cha Imani ya Kanisa, kwani ni matendo yanayoonesha ushindi wa Kristo dhidi
ya dhambi na mauti na kwa njia hii, Kristo anawafungulia waamini njia ya maisha mapya.
Kwa kuzaliwa upya katika Sakramenti ya Ubatizo; waamini wanapokea mapaji ya Roho Mtakatifu
na hivyo kufanyika waana wateule wa Mungu. Kwa njia hii, Mwenyezi Mungu anakuwa ni
Baba yao!
Anawahudumia kama watoto wake wateule, anawafahamu fika na kuwasamehe
dhambi zao wanapotopea katika dhambi, anawakumbatia na kuendelea kuwapenda hata pale
wanapomponyoka. Baba Mtakatifu Francisko anakazia kwamba, Ukristo si tu kufuata amri
na maagizo, bali ni changamoto ya kuwa wapya na kuishi katika upya wa maisha kwa kuwa
ndani ya Kristo; kwa kufikiri na kutenda na hatimaye, kugeuzwa na upendo wa Yesu!
Maisha
haya mapya hayana budi kurutubishwa kila siku kwa kusikiliza na kulitafakari Neno
la Mungu, Sala, kwa kushiriki kikamilifu Sakramenti za Kanisa hasa Sakramenti ya Upatanisho
na Sakramenti ya Ekaaristi Takatifu inayomwilishwa katika Matendo ya Huruma. Mwenyezi
Mungu anapaswa kuwa ni kiini cha maisha ya waja wake.
Kwa njia ya ushuhuda
wa uhuru katika maisha, furaha na matumaini yanayobubujika kutokana na ushindi wa
Kristo Mfufuka dhidi ya dhambi na mauti; waamini wanaweza kutoa huduma makini duniani;
kwa kuwasaidia jirani zao kuona mwanga wa ukombozi unaotoka kwa Mwenyezi Mungu.
Baba
Mtakatifu akizungumza na waamini na mahujaji katika lugha mbali mbali, amewapongeza
wanafunzi wa kijeshi kutoka Chuo cha Kijeshi cha NATO kwa huduma katika kukuza misingi
ya amani na ushirikiano wa kimataifa. Kristo aliyeteswa, akafa na kufufuka kutoka
katika wafu anawawezesha waamini kuwa ni watoto wateule wa Mungu, changamoto ya kuwashirikisha
wengine furaha hii inayobubujika kutoka kwa Kristo mwenyewe pamoja na kuendelea kuwa
wapya katika maisha ya Kikristo.
Kamwe waamini wasikatishwe tamaa na ubaya
unaowazunguka bali watambue kwamba, yote ambayo wameambiwa na Kristo yanalenga kuwapatia
amani ya ndani. Ulimwenguni watakuwa na dhiki, lakini wanapaswa kujipa moyo, kwani
Kristo mwenyewe ameushinda ulimwengu. Amewatakia wote amani kutoka kwa Kristo Mfufuka.
Mwishoni,
Baba Mtakatifu amewashukuru na kuwapongeza Maaskofu na Waamini wao wanaofanya hija
ya maisha ya kiroho hapa mjini Vatican kama sehemu ya Maadhimisho ya Mwaka wa Imani.
Anawatakia wafanyakazi wanaoteseka kutokana na kukosa mishahara yao kupatiwa ufumbuzi
wa haraka. Hija ya waamini katika Makaburi ya Mitume iwe ni sehemu ya mchakato wa
kuimarisha imani, matumaini na mapendo.
Baba Mtakatifu anawataka Vijana wajifunze
kujenga utamaduni wa kusikiliza; wagonjwa wapate faraja kutoka kwa Kristo na wanandoa
wapya watambue na kuona uwepo endelevu wa Mungu kati yao!