Kardinali Jorge Bergoglio na Maadhimisho ya Mwaka wa Imani
Kutokana na ukosefu wa usalama, amani na utulivu, watu wengi wamejikuta wanafunga
milango ya nyumba na maisha yao kwa wageni na watu wasiowafahamu, ili kujihakikishia
usalama wa maisha.
Mlango uliofungwa
ni kielelezo makini cha maisha ya Jamii nyingi katika ulimwengu mamboleo, ni hali
halisi inayoyojionesha kwa sasa na kwa siku za usoni katika kukabiliana na changamoto
za maisha.
Mlango uliofungwa madhubuti ni kielelezo pia cha mtu kujifunga
katika undani wa maisha yake, zile ndoto, matumaini, mahangaiko na nyakati za furaha
zinafungwa na hivyo kushindwa kuwashirikisha majirani na watu wengine. Mlango uliofungwa
ni kielelezo cha moyo uliofungwa pia kwa watu wengine, kiasi kwamba watu wengi zaidi
wanashindwa kupita na hatimaye, kushiriki undani wa maisha ya mtu. Kimsingi, mlango
uliofunguliwa daima umekuwa ni kielelezo cha mwanga, urafiki, furaha, uhuru na uaminifu.
Katika maadhimisho ya Mwaka wa Imani, waamini wanapaswa kuzitafuta tena tunu
hizi msingi katika hija ya maisha yao ya imani, kwani mlango uliofungwa unaleta madhara
kwa wahusika kwa kuwatenga na wengine. Mlango wa Imani, ndiyo picha iliyotumiwa na
Baba Mtakatifu Benedikto wa kumi na sita katika Waraka wake wa kichungaji kuhusu Maadhimisho
ya Mwaka wa Imani, “Porta Fidei”. Anawaalika waamini kupitia katika mlango huu ili
waweze kupata mambo msingi katika maisha yao ya kiimani kwa kuanza maisha mapya.
Hivi
ndivyo Kardinali Jorge Bergoglio ambaye kwa sasa ni Baba Mtakatifu Francisko alivyowaandikia
waamini wake katika Maadhimisho ya Mwaka wa Imani. Mlango wa Imani ni taswira inayowarudisha
waamini katika Kanisa la Mwanzo, lilipofungua malango yake hata kwa watu wa Mataifa
wakabahatika kusikia Habari Njema ya Wokovu ikitangazwa masikioni mwao. Ndiyo ile
picha ya Yesu anayebisha hodi katika mlango wa moyo wa kila mwamini, akimfungulia,
ataweza kuingia na kukaa ndani mwake.
Imani ni neema na zawadi kutoka kwa
Mwenyezi Mungu. Mwamini anapopitia katika Mlango wa Imani anaanza hija ya maisha ya
uzima wa milele. Kwa bahati mbaya anasema Kardinali Bergoglio kuna malango yenye mvuto
na mashiko yanayowaahidia waamini mafanikio na raha tele, lakini baadaye yanakuwa
ni chanzo cha kuchanganyikiwa, mahangaiko, kukata tamaa na hatimaye kupoteza mwelekeo
kwa siku za usoni.
Mlango wa Imani daima uko wazi, humo Kanisa linaendelea
kutangaza Habari Njema ya Wokovu na kuwakirimia waamini neema inayowaletea mabadiliko
ya ndani katika maisha yao na Mlango huu ni Yesu Kristo ambaye ni njia, ukweli na
uzima na kwamba, Yeye ndiye yule Mchungaji mwema aliyeyamimina maisha yake kwa ajili
ya ukombozi wa ulimwengu.
Mwenyeheri Yohane Paulo wa pili alipokuwa anaanza
utume wake kama Khalifa wa Mtakatifu Petro, aliwaalika waamini na watu wote wenye
mapenzi mema kumfungulia Kristo malango ya maisha yao. Kw anjia ya ukarimu, wafuasi
wa Emmaus waliweza kumfungulia Yesu malango ya maisha yao, akaingia na kula pamoja
nao na hatimaye, wakabahatika kufafanuliwa Maandiko Matakatifu.
Mwaka wa Imani
ni fursa ya kumshukuru Mungu kwa zawadi ya Sakramenti ya Ubatizo ambayo inawawezesha
waamini kuwa ni wana wateule wa Mungu na ndugu zake Kristo. Maadhimisho ya Mwaka wa
Imani yasaidie kujenga na kuimarisha umoja miongoni mwa Wakristo; iwe ni fursa ya
kutubu na kuongoka na changamoto ya kuwa watakatifu, ili kuyatakatifuza malimwengu
kwa njia ya ushuhuda makini wa imani katika matendo, ili kuweza kupata furaha ya kweli
katika maisha.
Waamini wajitaabishe kuifahamu imani kwa kina na mapana; wajitahidi
kuiungama kwa vinywa na matendo yao adili; kuishuhudia katika maisha na vipaumbele
vyao katika maisha ya hadhara, daima wakijitahidi kuwa ni Wamissionari katika kutangaza
Habari Njema ya Wokovu.
Mwaka wa Imani anasema Kardinali Bergoglio uwasaidie
waamini kuweza kukabiliana na changamoto mbali mbali katika maisha na utume wa Kanisa,
daima wakitambua kwamba, Mwenyezi Mungu yuko pamoja nao! Iwe ni nafasi murua ya kuboresha
mawasiliano kati ya watu ndani ya Jamii; kwa kuheshimiana na kuthaminiana; kwa kupendana
na kusaidiana, daima kwa kutafuta mafao ya wengi. Roho Mtakatifu awasaidie waamini
kuchuchumilia haki na utakatifu wa maisha; kuendelea kurithisha imani na matumaini
kwa vijana wa kizazi kipya.
Waamini wajitahidi kufanya kazi katika mazingira
bora, kwa kulinda na kuheshimu utu wa binadamu, ili kila mtu aweze kupata utimilifu
wa maisha. Mwaka wa Imani iwe ni fursa ya kusimama kidete kulinda na kutetea uhuru
wa kidini kwa kwa kuishi na kutenda kwa haki; kwa kupenda na kutenda wema.
Mwaka
wa Imani uwe ni mwanya wa kusameheana na kujenga urafiki katika tabasamu kwa kuwajali
wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii; watu ambao hawana thamani mbele ya macho
ya wengi! Kwani hawa ndio wale ambao Yesu mwenyewe anawaita kuwa ni ndugu zake. Ni
wakati muafaka wa kuadhimisha zawadi ya maisha, ili kuungana na hatimaye, kuwa wamoja
katika Kristo katika Maadhimisho ya Fumbo la Ekaristi Takatifu, ili kujenga na kuuimarisha
Ufalme wa Mungu.
Ni changanmoto na mwaliko wa kuumwilisha Mtaguso Mkuu wa
Pili wa Vatican na Mafundisho yaliyotolewa na Shirikisho la Mabaraza ya Maaskofu Katoliki
Amerika ya Kusini na Caribbean; Kanisa lijitahidi kufungua malango yake kwa watu wanaoishi
katika mazingira magumu lakini zaidi kwa watu wa nyakati hizi wenye kiu na hamu ya
kutaka kumwona Mungu katika hija ya maisha yao, kwa kusikiliza Habari Njema ya Wokovu.
Hii ni changamoto kwa Kanisa kujikita katika utume wa Kanisa kwa njia ya ushuhuda
wa maisha yanayojikita katika sala, kazi na utume, daima likiwa na mwelekeo wa Kimissionari.
Maadhimisho ya Mwaka wa Imani ni nafasi ya kupyaisha maisha ya waamini katika Kristo
Mfufuka.
Kardinali Jorge Mario Bergoglio katika barua yake ya Maadhimisho
ya Mwaka wa Imani, anawaalika waamini na watu wote wenye mapenzi mema kumwendea Bikira
maria, Mama wa Mungu ili aweze kuwasindikiza katika mapambazuko mapya ya imani sanjari
na kumwomba Roho Mtakatifu aweze kulishukia na kukaa na Kanisa, tayari kwenda kutangaza
matendo makuu ya Mungu katika maisha ya wanawadamu.
Imehaririwa na Padre Richard
Mjigwa, C.PP.S. Idhaa ya Kiswahili ya Radio Vatican.