2013-04-09 11:52:02

Papa kutembelea kituo cha kuwahudumia wakimbizi na wahamiaji mjini Roma


Baba Mtakatifu Francisko anatarajiwa kutembelea Kituo cha Kuhudumia Wakimbizi kinachoendeswa na Shirika la Wayesuit hapa Roma, kama kielelezo cha mshikamano na wahamiaji na wageni wanaokabiliwa na changamoto mbali mbali katika maisha wanapokuwa ugenini.

Taarifa hii imetolewa na Shirika la Habari la ANSA baada ya kuthibitisha habari hizi kutoka kwa Padre Giovanni La Manna, Mkurugenzi wa Kituo cha Kuhudumia Wakimbizi cha Wayesuit kilichoko mjini Roma. Padre la Manna anasema, mara ya kwanza aliposikia simu ikidai kwamba inatoka kwa Papa Francisko hakuamini na kwa kitambo kidogo alipigwa na bumbuwazi.

Itakumbukwa kwamba, wakati wa baraka na ujumbe wake kwa mji wa Roma na Dunia kwa ujumla, Baba Mtakatifu aligusia kwa namna ya pekee umuhimu wa kusimama kidete kulinda na kutetea haki, amani, upendo na mshikamano. Kunako mwaka 1980 Padre Pedro Arrupe, Mkuu wa Shirika la Wayesuit kwa wakati huo, alianzisha Shirika la Kuhudumia Wakimbzi, ambalo hadi sasa linatekeleza utume wake katika nchi 40. Limekuwa mstari wa mbele kutetea haki msingi za wakimbizi, wahamiaji na watu wasiokuwa na makazi maalum.

Jijini Roma, kituo hiki kinatoa chakula kwa ajili ya wakimbizi na wahamiaji. Kitendo cha Baba Mtakatifu Francisko kutembelea Kituo cha Kuwahudumia Wakimbizi cha Wayesuit ni kielelezo cha mshikamano wa Kanisa kwa maskini na wote wanaosukumizwa pembezoni mwa Jamii.







All the contents on this site are copyrighted ©.