Watanzania wanaomboleza kifo cha Prof. Michael wambali
Waziri mkuu wa Tanzania Mizengo Pinda ameongoza mamia ya waombolezaji kuuaga mwili
wa aliyekuwa Mhadhiri wa Shule Kuu ya Sheria ya Chuo Kikuu Cha Dar es Salaam, na wakili
maarufu Profesa Michael Wambali ambaye alifariki dunia Aprili 4, 2013 katika hospitali
ya Taifa Muhimbili kutokana na majeraha aliyoyapata kwenye ajali ya gari. Shughuli
ya kuuaga rasmi mwili wa marehemu Profesa Wambali ilifanyika Jumatatu, Aprili 8, 2013
kwenye ukumbi wa Nkrumah, Chuo Kikuu cha Dar es Salaam kabla ya kupelekwa kanisani
kwa misa maalum. Akizungumza na waombolezaji hao kabla ya kutoa heshima za mwisho,
Waziri Mkuu alisema mchango wa Prefesa Wambali kwenye fani ya sheria ni mkubwa mno
na hauelezeki. “Kama walimu wenzake wangeamua kuhesabu idadi ya wanafunzi ambao Profesa
Wambali aliwafundisha, ni dhahiri kuwa idadi yao ingekuwa kubwa kuliko tunavyoweza
kufikiria,” alisema. “Juzi tu tarehe 29 Machi, ametimiza miaka 59 ya kuzaliwa
na siku sita baadaye akaaga dunia, lakini katika kipindi cha miaka yake 59 ni miaka
32 ambayo aliitumia hapa chuoni. Hapa tulipo wapo Majaji, Mawakili wa Serikali na
wa kujitegemea, mahakimu na wengine wako mikoani wameshindwa kufika hapa leo… lakini
wote hawa wamefundishwa na Prof. Wambali katika kipindi cha miaka 32 aliyokaa hapa
chuoni,” alisema. Alisema fani ya sheria imepoteza kiongozi makini na mfano wa
kuigwa. “Tumepoteza kiongozi mzuri na makini siyo kwa Chuo Kikuu cha Dar es Salaam
peke yake bali ni kwa Tanzania yote,” aliongeza. Aliwasihi wanafamilia waikubali
hali ya kuondokewa na mpendwa wao, wajipe matumaini kwamba mwenzao ametangulia na
akawataka waendelee kumuombea kwa Mungu ili ampokee huko mbinguni. Kwa wanafunzi
wa wafanyakazi wa Shule Kuu ya Sheria, Waziri Mkuu alikuwa na haya ya kusema: “Ingawa
Profesa Wambali ameondoka, ninaamini bado ataendelea kuwa nasi kwani ametuachia kazi
zake nyingi za kimaandishi ambazo zitatumiwa na wengine katika siku zijazo. Tukienzi
hilo, tutakuwa tunaendeleza yale aliyokuwa akiyasimamia.” Naye Mkuu wa Chuo Kikuu
Huria cha Tanzania, Dk. Asha-Rose Migiro ambaye aliwahi kufanya kazi na Profesa Wambali
miaka ya 80, wakati akitoa nasaha zake alisema alifanya naye kazi ofisi moja na waliwahi
kufundisha masomo ya aina moja. Dk. Migiro alisema kila aliyewahi kuwa mwanafunzi
wa Prof. Wambali hawezi kuacha kumkumbuka. “Hatuwezi kumrudisha kwa sasa ila kila
aliyewahi kuwa mwanafunzi wa Profesa Wambari atamkumbuka daima. Mike ameondoka lakini
atabakia mioyoni mwetu. Kila tutakapoona familia yake ama kuona kuona kazi zake za
taaluma, tutaendelea kuonana naye,” alisema.